KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Thursday 5 March 2015

UNDANI KUHUSU KUUNDWA KWA SOKO LA PAMOJA LA AFRIKA MASHARIKI

 NA BASHIRU ALLY

Kuna kila dalili kwamba baadhi ya Asasi za Kiraia (AZAKI) zinazoendesha shughuli zake katika nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) zimeanza kushiriki katika mjadala juu ya namna bora na endelevu ya utekelezaji wa wazo la kuundwa kwa soko la pamoja (common market) la Afrika Mashariki.

Makala haya  yanadadisi kwa muhtasari mwelekeo wa mjadala huo na athari zake kwa maendeleo endelevu ya EAC.

Makala haya yanaainisha pia masuala ya msingi yanayojadiliwa. Moja ya hoja nzito za mjadala huo ni kwamba kuundwa kwa soko la pamoja hakutakuwa na tija ikiwa uchumi wa nchi za EAC utaendelea kuwa duni na tegemezi.

Hii ni hoja nzito inayotakiwa kuchambuliwa kwa undani. Makala haya yanajaribu kufanya hivyo.

Watoaji wa hoja hiyo wanadai kuwa uchumi duni na tegemezi ni miongoni mwa vikwazo vikuu vya utekelezaji endelevu wa malengo ya EAC.

Wanadai kuwa bila kuwa na mfumo mbadala wa kisiasa na kiuchumi katika nchi wananchama wa EAC, soko la pamoja halitakuwa na manufaa kwa wananchi wengi, hasa wavujajasho, kwani matunda yake yatavunwa na wajanja wachache wenye uwezo wa kifedha na madaraka ya kisiasa.

Katika muktadha huu, jukumu kubwa la AZAKI ni kuchambua kwa undani hoja hii na hatimaye kubuni mbinu mbadala za kujenga mshikamano wa wavujajasho ili waweze kunufaika na matunda ya EAC.

Hoja iliyoainishwa hapo juu msingi wake ni historia ya ubeberu (imperialism) na pia muktadha wa sasa wa utandawazi wa kibepari (capitalist globalisation).

Kwa sababu za kihistoria, EAC ni chombo ambacho kimejengwa juu ya mfumo kandamizi wa ubepari wa kibeberu (imperialist capitalism) unaodhibitiwa na dola kuu za kibeberu hasa Marekani, Uingereza, Ujerumani na Ufaransa kwa kushirikiana na mashirika ya kimataifa ya fedha na biashara yaani Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Benki ya Dunia (WB) na Shirika la Biashara Duniani (WTO).

Ubeberu wa kibepari (imperialist capitalism) ulizaliwa Ulaya Magharibi katika karne ya 18 na baadaye kuenezwa kimabavu na kikatili katika nchi za Afrika kwa mtindo wa ukoloni. Historia hii ndiyo kiini cha kudidimia kwa uchumi katika nchi zote za JAM.

Hata baada ya miaka zaidi ya hamsini ya uhuru wa bendera (flag independence), dola kuu za kibeberu zimeendelea kudidimiza maendeleo ya nchi wanachama wa EAC kwa njia na mbinu za kijeshi, biashara, mikopo, misaada, teknolojia, siasa, diplomasia na uwekezaji.

Ndiyo maana hadi sasa uchumi wa nchi za EAC ni duni na tegemezi kwa nchi za kibeberu. Kwa mfano, sekta ya viwanda katika nchi hizo ni dhaifu na mchango wake kiuchumi ni mdogo.

Kwa kiwango kikubwa uchumi wa nchi hizi bado unategemea zaidi uuzwaji nje wa bidhaa ghafi za kilimo na madini.

Vile vile biashara ya nje inachukua nafasi kubwa na ya kipekee katika uchumi mzima  kwa sababu sekta ya uchuuzi na hasa uchuuzi wa bidhaa zilizoagizwa kutoka nje ndiyo unaochangamkiwa zaidi na wajasiriamali kwa sababu ya uhakika wa kuchuma faida kwa haraka.

Hata hivyo, uchuuzi unachangia kuua viwanda vya nchi za EAC na hivyo kupoteza fursa za ajira na mapato ya serikali.

Uchuuzi unaua pia ari ya uzalishaji wa chakula na bidhaa nyingine muhimu kwa mahitaji ya wakazi wa nchi wanachama wa EAC.

Vilevile, vitega uchumi vingi vinaelekezwa katika sekta za fedha, nyumba, mawasiliano, madini na uchuuzi wa bidhaa za anasa. Hizi ndizo sekta zinazowavutia zaidi wawekezaji wa nje na ndani kwa sababu kuna fursa za kuchuma faida kwa mtindo wa ’fastafasta’.

Jambo baya zaidi ni kwamba sehemu kubwa ya faida inayochumwa na wawekezaji wa nje inalimbikizwa nje ya nchi za EAC.

Bila shaka, wawekezaji wakubwa kutoka nje siyo ’wakombozi’ wala 'wabia wa maendeleo’ kwani kipaumbele chao ni kuvuna faida nono na siyo kuleta maendeleo endelevu ya nchi za JAM. 

Hata mitaji ya wananchi wa nchi za EAC haifui dafu kwa mitaji ya wawekezaji kutoka nje. Matokeo yake wawekezaji raia katika nchi za JAM wanalazimika kuwa mawakala au wabia wadogo wa wawekezaji wa nje.

 Kwa kiwango kikubwa, utegemezi wa mitaji kutoka nje ni kikwazo cha maendeleo endelevu katika nchi za EAC.

Hata wazalishaji wadogo katika sekta za kilimo, uvuvi, madini, mifugo na viwanda hawanufaiki na jasho lao na hata mazingira yao ya uzalishaji ni duni.

Katika hali hiyo, wenye mitaji mikubwa wanatumia hila kuwanyonya wazalishaji wadogo kwa kutumia mbinu chafu za kibiashara, mikopo, bei za pembejeo na bei za bidhaa na huduma muhimu kama vile elimu, nyumba, nishati na afya.
Unyonyaji wa aina hii unawezeshwa na sheria mbovu zinazotungwa na kusimamiwa na watumishi wa umma na wanasiasa ambao wanashinikizwa  na taasisi za kimataifa za kibeberu.

Ndoto za kuundwa, hatua kwa hatua, kwa Shirikisho la Afrika Mashariki haziwezi kutimia ikiwa muundo wa uchumi katika nchi wanachama wa EAC utaendelea kuwa na sifa zilizoainishwa hapo juu.

Hivi sasa hakuna dalili kwamba malengo na mikakati ya kiuchumi katika EAC yanaongozwa na dira ya ukombozi kama ilivyokuwa enzi za mapambano dhidi ya ukoloni na ukaburu. 

Mapambano ya ukombozi wa kiuchumi yametelekezwa.

Hata hoja nyingi za mjadala uliopo sasa juu ya mwelekeo wa EAC hazikosoi mfumo unaotamalaki sasa wa utandawazi wa kibepari ingawa mfumo huu ndio kikwazo kikuu cha maendeleo ya nchi wanachama wa EAC.
Mfumo wa utandawazi wa kibepari  ni kikwazo kwa sababu uchumi wa nchi wanachama wa EAC unaendelea kuwa chini ya himaya ya nchi za kibeberu.

Kwa hiyo, hoja kuu siyo hofu au shauku ya kuundwa kwa soko la pamoja la EAC bali ni mwelekeo tenge wa maendeleo ya nchi wanachama wa EAC na hasa namna nchi hizo zinavyoshindwa kusimamia na kuongoza mchakato wa mageuzi ya mifumo yao ya kiuchumi na kisiasa kwa maslahi ya wananchi wake.

Katika muktadha wa utandawazi wa kibepari, nchi wanachama wa EAC zinatakiwa kuwa na mikakati ya mageuzi katika mifumo yao ya kisiasa na kiuchumi inayowiana na inayooongozwa na dira ya ukombozi wa wavuja jasho.

Katika harakati za ukombozi wa kiuchumi, maendeleo ya kasi katika sekta za elimu, afya, maji, nishati, madini, fedha na mawasiliano yanahitajika.

Bila shaka uwekezaji wa pamoja baina ya nchi wanachama wa EAC utahitajika ili utekelezaji wa mikakati ya aina hiyo uwe wa ufanisi na endelevu.

Hii ina maana kwamba masoko ya fedha, bidhaa na ajira yatakuwa chini ya uratibu wa EAC na hatimaye kujenga msingi imara wa kuunda Shirikisho la Afrika Mashariki.

Vile vile, sekta nyeti kiuchumi hasa fedha, mawasiliano, madini, nishati na viwanda zinatakiwa kumilikiwa na wananchi wa nchi wanachama wa EAC.

Mageuzi ya kiuchumi na kisiasa ya aina hii yanaweza kuanzisha safari ndefu ya kuelekea kwenye ujenzi wa ujamaa wa soko (market socialism) na demokrasia ya wavujajasho (popular democracy).

 Kwa maoni yangu, huu ndiyo mkakati mbadala wa kuziondoa nchi wanachama wa EAC katika makucha ya dola kuu za kibeberu na vibaraka wao. Hata hivyo, haya yote hayawezi kutokea ikiwa ushiriki wa wavujajasho katika uendeshaji wa uchumi na siasa katika nchi wanachama wa EAC utakuwa mdogo kama ilivyo sasa.

 Kwa hiyo, kazi kubwa ya AZAKI ni kuhamasisha wavujajasho wa nchi zote wanachama wa EAC kudai mfumo mbadala wa siasa, uchumi wenye manufaa kwa uhuru, haki na utu wao.

Hata AZAKI zenyewe zinatakiwa kukataa katakata fadhila fedheheshi za mabeberu na vibaraka wao.

(Mwandishi wa Makala haya ni Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) akifafanua kwa undani sehemu ya Mada aliyoiwasilisha kwenye Kongamano la AZAKI juu ya Mtangamano wa Afrika ya Mashariki lililoandaliwa na Foundation for Civil Society (FCS) Desemba 2014, jijini Arusha.)

No comments:

Post a Comment