KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Monday 20 April 2015

SERIKALI KUANDAA MUSWADA UTAKAOWALINDA WATOA TAARIFA

Baadhi ya wanahabari na wahariri waliohitimu mafunzo ya ubobezi katika kuandika habari za dawa za kulevya na uandishi wa habari za maendeleo ya malengo ya milenia wakiwa katika hafla ya kukabidhiwa vyeti. Hafla hiyo ilifanyika ofisi za UN jijini Dar es Salaam juzi.
SERIKALI imesema inaandaa mswada wa sheria ambayo itawalinda watoaji wa taarifa za masuala ya uhalifu ikiwa ni jitihada za kuimarisha mapambano dhidi ya vitendo mbalimbali vya uhalifu nchini Tanzania. 

Kauli hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. George Masaju alipokuwa akitoa vyeti kwa baadhi ya waandishi wa habari waliokuwa katika mpango wa kuandika habari za dawa za kulevya pamoja na mafanikio na changamoto za mpango wa milenia.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyoandaliwa kwa ushirikiano na Umoja wa Mataifa (UN) na Mfuko wa Wanahabari Tanzania (TMF), Masaju alisema kwa sasa ni Sheria ya Makosa ya Rushwa (ufisadi) tu ndiyo inayowalinda watoaji wa taarifa hizo kwani imekataza wao kutajwa tofauti katika maeneo mengine ya sheria.

Alisema katika sheria hiyo mpya inayokusudiwa kutungwa na Serikali itapanua wigo wa ulinzi kwa watoaji wa taarifa kutotajwa endapo watatoa taarifa juu ya makosa yoyote jambo ambalo alisema litasaidia katika mapambano ya uhalifu. 

“Serikali inaandaa muswada wa Sheria ya kuwalinda watoa taarifa wa vitendo vya uhalifu (whistle blowers protection bill) ili kuimarisha mapambano dhidi ya uhalifu wa aina zozote nchini. Kwa sasa ni watoa taarifa wa makosa ya rushwa (ufisadi) tu ndio wanatamkwa katika sheria ya kuzuia na Kupambana na Rushwa, 2007 kulindwa wasitajwe,” alisema Mwanasheria Mkuu.

Aidha alisema Sheria mpya ya Kupambana na Kudhibiti Dawa za Kulevya ya Mwaka 2015 ambayo imepitishwa na Bunge hivi karibuni imetungwa kwa kuzingatia mapungufu ya sheria za nyuma hivyo itakuwa na nguvu zaidi ya kupambana na uhalifu huo tofauti na ilivyokuwa awali.

Alikiri kuwa sheria ya awali ilikuwa na mapungufu kadhaa jambo ambalo lilichangia sheria hiyo kushindwa kufanya kazi kikamilifu katika mapambano.

 Alisema miongozi mwa mapungufu kwa sheria iliyokuwa ikitumika awali ni pamoja na kutotoa adhabu kulingana na ukubwa wa kosa, na haikuainisha masharti bora ya udhibiti wa madawa ya kulevya kama ilivyo kwa sheria mpya.

Alisema sheria mpya imeanzisha Baraza la Taifa la Kudhibiti Dawa za Kulevya ambapo mwenyekiti wake ni Waziri Mkuu wa Tanzania na wajumbe wake watatoka pande zote za Muungano yaani Tanzania Bara na Visiwani, alisema kazi kubwa ya balaza hilo ni kusimamia utekelezaji wa Sera ya Udhibiti wa Dawa za kulevya.

“Sheria iliyopo ina udhaifu wa adhabu, haitoi adhabu kulingana na ukubwa wa kosa kwenye baadhi ya makosa, hivyo kusababisha kukosekana kwa mizania ya haki. Sheria mpya imeweka kima cha kuanzia cha adhabu iwe ni faini au kifungo. …Mfano sheria mpya imeweka adhabu ya faini isiyopungua milioni 50 na isiyozidi milioni 500 au kifungo kisichopungua miaka 7 na kisichozidi miaka 30 au vyote kwa pamoja.” 

Alifafanua Masaju katika hotuba yake.
Jumla ya waandishi wa habari 18 walipata mafunzo ya namna ya kuripoti habari za dawa za kulevya pamoja na kuripoti habari za malengo ya milenia baada ya kuwezeshwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP)kwa kushirikiana na mfuko wa wanahabari Tanzania (TMF) na kukabidhiwa vyeti na mgeni rasmi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Masaju.

No comments:

Post a Comment