KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Saturday 21 May 2016

WABUNGE WANAOTOKA KATIKA MAENEO YA WAFUGAJI WAPANGA KUMKWAMISHA MAGHEMBE


WABUNGE wanaotokea katika maeneo ya jamii ya wafugaji wamepanga kukwamisha Bajeti ya Waziri wa Malisili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe,kutokana na kauli yake ya kudai kuwa mifugo ya Tanzania haifai huku nyama yake ikiwa na sumu.
Mkakati huyo unatarajiwa kufanyika mwanzoni mwa wiki wakati waziri huyo atakapowasilisha hotuba yake ya kuomba kupitishiwa bajeti ya wizara hiyo ya mwaka 2016/17.
Waziri Profesa Maghembe anatarajia kusoma hotuba yake bungeni Juni 24, mwaka huu ambayo itajadiliwa kwa siku mbili huku wabunge wanaotoka mikoa ya wafugaji wakijiandaa kukwamisha bajeti hiyo isipite.
Walisema sababu kubwa ya kukwamisha bajeti hiyo ni kunatokana na kauli yake ya hivi karibuni aliyoitoa kwenye kipindi maalumu kwenye moja ya kituo cha televisheni kuwa mifugo ya Tanzania haina thamani.
Mbunge wa Nzega Mjini, Hussen Bashe (CCM) alisema, waziri huyo amejiweka katika nafasi ngumu kutokana na kutoa kauli ambayo imewaacha wafugaji njiapanda.
Bashe alisema, hakuna maeneo ambayo yanaweza kuwasaidia wafugaji kwa sasa kutokana na ranchi kuhodhiwa na vigogo.
 “Binafsi namheshimu sana Profesa Maghembe, namuomba aombe radhi kwa kauli yake na akishindwa lazima tutabanana huko ndani, kwanza alitoa hoja dhaifu sana kwamba pato la mifugo ni dogo wakati anajua wafugaji hawajawezeshwa,” alisema.
Mbunge huyo alisema wafugaji wamehesabiwa kama wakimbizi katika nchi yao na walibaguliwa tangu mwanzo pale Tanzania iliposema ni ya wakulima na wafanyakazi lakini kundi la wafugaji likaachwa nyuma.
Bashe alisema, haiwezekani kupitisha bajeti ya Profesa Maghembe kwa kuwa kauli yake ni ya kuwabeza wafugaji.
Naye Mbunge wa Monduli, Julius Kalanga (Chadema) alipinga kauli ya Waziri Maghembe ya  kuwataka wafugaji hao kuondoka kwenye hifadhi ifikapo Juni 15 mwaka huu.
Kalanga alisema kuna shida nchini kwa kuwa hakuna sera ya mifugo na mfumo wa utungaji kutokana na Bunge kupitisha sheria zilizotungwa na serikali.
Naye Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi Mwigulu Nchemba, aliwataka wafugaji kutokuwa na wasiwasi kwa kuwa hakuna mtu atakayeondolewa kwenye maeneo yao hadi taratibu zingine zitakapofanyika.
Profesa Maghembe akizungumza katika kipindi hicho alisema kuwa mifugo ya Tanzania inaliingizia taifa pato kidogo kwa hiyo haina faida kubwa ukilinganisha na pato litokanalo na Maliasili na Utalii la wanyama.

No comments:

Post a Comment