MWENYEKITI
wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), Bahame Nyanduga amesema
kuwa jukumu la usimamizi na utetezi wa masuala ya haki za binadamu sio jukumu
la Serikali, Asasi za kiraia wala mtu binafsi, ni jukumu la watu wote.
Nyanduga
aliyasema hayo jana alipokuwa akifunga mkutano wa siku tatu wa wadau wa haki za
binadamu uliofanyika jijini Dar es Salaam kujadili mapendekezo ya tathimini ya
utekelezaji wa masuala ya haki za binadamu.
Katika
mkutano huo, Nyanduga alisema kuwa haki za binadamu zinamuhusu kila mmoja wetu,
hivyo ni muhimu kwa tume na asasi za kiraia kushirikiana kwani wote wanafanya
kazi moja ya kujenga taifa lenye kuheshimu haki za binadamu.
“Tume
haichagui nani wa kushirikiana nae kwa kuwa masuala ya haki za binadamu sio
miliki ya serikali, asasi za kiraia wala mtu binafsi, bali ni jukumu letu sote”
alisema.
Aliongeza
kuwa: “ni muhimu tukashirikiana sisi wote kwa kuwa lengo letu ni kujenga taifa
lenye kuheshimu haki za binadamu”
Aidha,
Nyanduga alisema baada ya kumalizika kwa mkutano huo ni muhimu kwa tume na
asasi za kiraia kukaa pamoja ili kuyapitia vizuri mapendekezo hayo ambayo
wamekubaliana na kuandaa taarifa ambayo wataiwasilisha serikalini kwa ajili ya
kuishawishi serikali iweze kuyakubali mapendekezo hayo ambayo awali iliyakataa.
Awali,
Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), Onesmo
Olengurumwa, aliwataka wanahabari kutumia fursa waliyoipata katika mkutano huo
kuelimisha jamii kuhusu mchakato mzima wa tathimini ya utekelezaji wa masuala
ya haki za binadamu.
“Mkutano
huu umekuwa ni fursa kwenu wanahabari kujua namna mchakato wa tathimini
ya utekelezaji wa masuala ya haki za binadamu unavyokuwa kwa kuwa hamkuwepo
Geneva, lakini kupitia mkutano huu mumeweza kuelewa, hivyo naomba mtumie fursa
hii kuelimisha jamii kuhusu mchakato huo”, alisema Olengurumwa
Olengurumwa
aliipongeza tume kama taasisi ya kitaifa inayosimamia masuala ya haki za
binadamu kwa ushirikiano wao mkubwa ambao wamekuwa wakiendelea kuutoa kwa asasi
za kiraia na aliiomba taasisi hiyo kuendelea kufanya hivyo kwani ndio
njia pekee itakayosaidia kupiga hatua kubwa katika masuala ya usimamizi wa haki
za binadamu kama nchi.
Itakumbukwa
kuwa Juni 27-29 mwaka huu, wadau wa haki za binadamu walikutana jijini Dar es
Salaam kujadili mapendekezo ya tathmini ya utekelezaji wa masuala ya haki za
binadamu nchini ili kupanga mikakati ya kuweza kuishawishi serikali kuyakubali
mapendekezo iliyokataa katika mkutano wa Baraza la Haki za Binadamu uliofanyika
Geneva Mei, mwaka huu. katika Mkutano huo mapendekezo ya jumla yalikuwa
227, serikali ilikubali mapendekezo 130 na kuyakataa 72 na 25 iliyaweka
pembeni.
No comments:
Post a Comment