KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Friday 1 July 2016

NYANDUGA: JUKUMU LA KUSIMAMIA HAKI ZA BINADAMU SIYO LA SERIKALI PEKEE

MWENYEKITI wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), Bahame Nyanduga amesema kuwa jukumu la usimamizi na utetezi wa masuala ya haki za binadamu sio jukumu la Serikali, Asasi za kiraia wala mtu binafsi, ni jukumu la watu wote.
Nyanduga aliyasema hayo jana alipokuwa akifunga mkutano wa siku tatu wa wadau wa haki za binadamu uliofanyika jijini Dar es Salaam kujadili mapendekezo ya tathimini ya utekelezaji wa masuala ya haki za binadamu.
Katika mkutano huo, Nyanduga alisema kuwa haki za binadamu zinamuhusu kila mmoja wetu, hivyo ni muhimu kwa tume na asasi za kiraia kushirikiana kwani wote wanafanya kazi moja ya kujenga taifa lenye kuheshimu haki za binadamu.
“Tume haichagui nani wa kushirikiana nae kwa kuwa masuala ya haki za binadamu sio miliki ya serikali, asasi za kiraia wala mtu binafsi, bali ni jukumu letu sote” alisema.
Aliongeza kuwa: “ni muhimu tukashirikiana sisi wote kwa kuwa lengo letu ni kujenga taifa lenye kuheshimu haki za binadamu” 
Aidha, Nyanduga alisema baada ya kumalizika kwa mkutano huo ni muhimu kwa tume na asasi za kiraia kukaa pamoja ili kuyapitia vizuri mapendekezo hayo ambayo wamekubaliana na kuandaa taarifa ambayo wataiwasilisha serikalini kwa ajili ya kuishawishi serikali iweze kuyakubali mapendekezo hayo ambayo awali iliyakataa.
Awali, Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), Onesmo Olengurumwa, aliwataka wanahabari kutumia fursa waliyoipata katika mkutano huo kuelimisha jamii kuhusu mchakato mzima wa tathimini ya utekelezaji wa masuala ya haki za binadamu.
“Mkutano huu umekuwa ni fursa kwenu wanahabari  kujua namna mchakato wa tathimini ya utekelezaji wa masuala ya haki za binadamu unavyokuwa kwa kuwa hamkuwepo Geneva, lakini kupitia mkutano huu mumeweza kuelewa, hivyo naomba mtumie fursa hii kuelimisha jamii kuhusu mchakato huo”, alisema Olengurumwa
Olengurumwa aliipongeza tume kama taasisi ya kitaifa inayosimamia masuala ya haki za binadamu kwa ushirikiano wao mkubwa ambao wamekuwa wakiendelea kuutoa kwa asasi za kiraia na  aliiomba taasisi hiyo kuendelea kufanya hivyo kwani ndio njia pekee itakayosaidia kupiga hatua kubwa katika masuala ya usimamizi wa haki za binadamu kama nchi.

Itakumbukwa kuwa Juni 27-29 mwaka huu, wadau wa haki za binadamu walikutana jijini Dar es Salaam kujadili mapendekezo ya tathmini ya utekelezaji wa masuala ya haki za binadamu nchini ili kupanga mikakati ya kuweza kuishawishi serikali kuyakubali mapendekezo iliyokataa katika mkutano wa Baraza la Haki za Binadamu uliofanyika Geneva Mei, mwaka huu.  katika Mkutano huo mapendekezo ya jumla yalikuwa 227, serikali ilikubali mapendekezo 130 na kuyakataa 72  na 25 iliyaweka pembeni.

No comments:

Post a Comment