KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Tuesday, 14 April 2015

WATANZANIA WATAKIWA KUWA MAKINI KATIKA MGAWANYO WA MAPATO YA GESI

Mkurugenzi Mkuu wa Repoa, Profesa Wangwe
MTAFITI Mwandamizi wa Taasisi ya Center for Development (CGD), Mujobu Moyo, amesema Tanzania kama nchi nyingine zinazoendelea inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo rushwa na vurugu za kisiasa ambazo zinaweza kusababisha gesi iliyogunduliwa ikashindwa kuwanufaisha wananchi wake.
Kauli hiyo aliitoa wakati wa mkutano wa Watanzania zaidi ya 400 kutoka wilaya mbalimbali nchini, ambao walikutana jijini Dar es Salaam jana, kujadili na kutoa maoni kuhusu ni jinsi gani mapato yatakayotokana na gesi yatawanufaisha wananchi wote nchini bila ya kubagua. 
Mkutano huo unatokana na kugundulika kwa hazina kubwa ya gesi nchini ambayo inategemewa kukuza pato la taifa zaidi ya mara 15 kuliko la sasa.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini jana, Moyo alisema mkutano huo umeandaliwa na taasisi hiyo kwa kushirikiana na taasi ya utafiti ya kuondokana na umaskini nchini Repoa.
“Mkutano huu utakuwa wa kwanza wa aina yake wa kuwashirikisha wananchi wa kawaida katika utafiti unaohusiana na jinsi sera mbalimbali zinavyotungwa na kutekelezwa kwa matakwa ya matajiri katika nchi zinazoendelea bila kuwaangalia wananchi wa kawaida wa hali ya chini,” alisema Moyo.
Moyo alisema ili kuepuka changamoto hizo viongozi wanapaswa kuweka usimamizi mzuri wa mapato ambayo yatatokana na gesi hiyo, yatatoa mustakabali wa nchi katika siku zijazo.
“Wananchi wanapaswa kwanza kueleweshwa juu ya mchakato mzima na kushirikishwa kutoa maoni yao ni jinsi gani mapato yatakayotokana na rasilimali hii yataleta manufaa kwa wote ili kuepuka makosa yaliyojitokeza katika nchi nyingine kwa kosa la kutowashirikisha wananchi katika masuala yanayohusu rasilimali za taifa,” alisema Moyo.
Moyo alisema utafiti huo unalenga kufuta dhana iliyozoeleka kuwa Watanzania wa kawaida hawana haki ya kutoa mawazo katika masuala ya kitaifa kama lilivyo suala hilo la gesi ambalo limekuwa likijadiliwa na wasomi na wanasiasa.
Mkurugenzi Mkuu wa  Repoa, Prof. Samuel Wangwe, alisema kuongezeka ghafla kwa pato kutokana na rasilimali hizo kunaweza kuleta athari mbalimbali kwa taifa badala ya faida kama vile kuongezeka kwa vitendo vya rusha na kuvurugika kwa uchumi.
Athari nyingine ni kuongezeka kwa umaskini na kupunguza kukua kwa demokrasia nchini.
Prof. Wangwe alisema hayo yote yanajitokeza iwapo nchi inakuwa na rasilimali nyingi na kundi la wananchi wa hali ya chini na wasio na elimu kutopewa taarifa sahihi na za kutosha juu ya kinachoendelea.



No comments:

Post a Comment