![]() |
| Katibu wa Chama Cha Mapinduzi Taifa, Kinana |
KATIBU wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kata ya Upanga
Magharibi, Abdul Malilima, amenusurika kipigo baada ya wanachama wenzake kudai
kuwa amevuruga kura za maoni za diwani
na mbunge kwa kwa ajili ya kumsaidia Adnan Kondo aweze kushinda.
Wanachama hao walifikia hatua hiyo baada ya kubaini njama za
katibu huyo ambaye alihamishiwa katika Kata hiyo siku mbili kabla ychaguzi huku
wakidai alipelekwa kwa mkakati maalumu wa kumsaidia mshindi huyo ambaye ni
mtoto wa Waziri wa Jinsia na Watoto Sofia Simba.
Akizungumza na wandishi wa habari, nje ya Ofisi za Kata hiyo
jijini Dar es Salaam leo, Balozi wa Nyumba ‘10’ Ashraf Khan, alisema
wanaopaswa kulaumiwa katika kuvurugika uchaguzi huo ni viongozi wa Ofisi ya
Katibu wa CCM Mkoa.
Alisema, wamefikia hatua hiyo kutokana na kitendo cha katibu
huyo cha kuwanyima haki ya kupiga kura wanachama wa tawi la Upanga Maghari na
Muhimbili huku akitoa nafasi hiyo kwa watu kutoka matawi mengine jijini.
“Kata yetu ina matawi manne lakini cha kushangaza ni matawi
mawili ambayo ni Tambaza na Minazini ndio yafanya uchaguzi ambao ulitawaliwa na
ukiukwaji wa sheria kwani waliopiga kura ya kumchagua Adnani sio wakazi wa
matawi hayo,”alisema Khan.
Alisema, kuwa kura hiyo ya maoni inayodaiwa kufanyika katika
matawi hayo hawaitambui kwa vile wapiga kura wengi walisafirishwa kutoka
Mbagala, Manzese, Mabwepande na wagonjwa (mateja), wanaotumia dawa za Methodine
katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
“Tunawaomba viongozi wa ngazi ya juu wa chama kutambua kuwa
kura za mbunge Azan Zungu zilizopelekwa Dodoma hazikutokana na wanachama wa
Upanga Magharibi kwani siku ya kupiga kura hata kitabu cha orodha ya majina ya
wapiga kura kilifichwa nyumbani kwa katibu huyo,”alisema Khan.
Vurugu hizo zilizidi zaidi pale Katibu huyo alipogoma kutoka
nje ya ofisi ili azungumze na wandishi wa habari, hali iliyowafanya wanachama
hao kutoa kwa nguvu huku wakilazimisha azungumze.
Hata hivyo, Malilima
aliamuwa kuzungumza kwa unyonge aliamua kuyaacha matawi hayo mawili katika kura
hiyo ya maoni kutokana na maelekezo aliyopewa bila kufafanua, yalitoka wapi.
“Mimi nimeamua kuzungumza lakini kwa vile mnafanya vurugu
nafikiri sitakuwa tayari kuzungumza na wahuni,”alisema Katibu huyo.
Baada ya kugoma wanachama hao walimnyang’anya funguo ya
Ofisi na kumfukuza huku wakimwita mwizi wa kura, wakimtaka kutorejea tena
katika ofisi hiyo kwani hata atakaporudi hawako tayari kumpa ushirikiano.
Naye Beatrice Makan, ambaye ni mmoja wa viongozi katika Kata
hiyo, alisema kuwa uchaguzi huo matokeo yake yalipangwa na viongozi wa CCM Mkoa
huo kwa lengo la kumsaidia mtoto wa waziri huyo.
Alisem baada ya uchaguzi huo kuvurugika Agosti Mosi, Ofisi
ya CCM wilaya iliagiza urudiwe lakini cha kushangaza haukurudiwa na baadala
yake matokeo yalipelekwa Dodoma yakionesha kuwa matawi yote yalipiga kura hiyo
wakati sio kweli.

No comments:
Post a Comment