TANZANIA
imefanikiwa kupata teknolojia mpya kutoka nchini China inayosaidia makandarasi
wa majengo kuweza kujenga jengo la ghorofa moja kwa siku 12 badala ya siku
35 kama ilivyokuwa awali.
Makamu
wa Rais Samia Suluhu Hassan, aliyasema hayo juzi wakati wa maadhimisho ya miaka
10 ya kampuni ya Group Six International (GSI) yaliyofanyika jijini Dar es Salaam,
ambayo pia yalihudhuriwa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Charles Mwijage.
Akizungumza jijini Dar
es salaam juzi, wakati wa maadhimisho hayo, Makamu wa Rais, alisema hakuna
taifa lililoendelea bila kuwa na maendeleo kwenye teknolojia jambo ambalo
linasababisha kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.
“Mwekezaji kama huyu ni
mfano wa kuigwa, licha ya kuwekeza nchini kwetu, kaleta teknolojia mpya
inayookoa muda na fedha zao na kaamua pia kuwafundisha watanzania ili nao
watumie teknolojia hiyo,ni jambo la kupigiwa mfano,”alisema.
Makamu
wa Rais, teknolokia hiyo itasaidia kuokoa fedha na muda ambao uliokuwa ukipotezwa
na wajenzi kutokana na kutumia teknolojia za kizamani.
Akizungumzia
suala la elimu, Makamu wa Rais, alisema kuwa kila mwenye uwezo wa kiuchumi anawajibu
wa kuchangia maendeleo ya Tanzania na kuwa hakuna maendelo yoyote yanayoweza
kupatikana kama hakuna wataalamu waliyoelimika.
Katika
maadhimisho hayo Makamu wa Rais alikabidhiwa hundi ya Sh.Milioni 20 ambazo zilizotolewa
na GSI kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya elimu kwenye shule mbili zilizoko
Mikocheni, jijini Dar es salaam.
Akizungumzia
suala la ulipaji kodi, Mwenyekiti wa kampuni hiyo, aliyejitambulisha kwa jina
la Huang alisema kuwa kampuni yake inatambuwa umuhimu wa kodi kwa hiyo wamekuwa
wakilipa kodi bila kushurutishwa na kwamba kwa miaka hiyo 10 waliyowekeza hapa
nchini tayari wamelipa zaidi ya shilingi bilioni 12 kama kodi pekee.
“Tumekuwa tukihakikisha
tunalipa kodi stahiki kwa wakati na kwa uaminifu na bila kushurutishwa kila
uwekezaji wetu tunahakikisha tunafuata sheria zote za Tanzania ili kuwa mfano
kwa wawekezaji wengine hapa nchini,”alisema Huang.
Aidha,
Huang, alimfahamisha Makamu wa Rais, kuwa wamedhamiria kujenga mahusiano mazuri
kati yao na jamii inayozunguka miradi yao, watakuwa na michango endelevu kwenye
sekta mbalimbali ili kuhakikisha Tanzania inasonga mbele kimaendeleo ili
kufikia lengo la kuwa nchi ya uchumi wa kati ifikapo 2020.
Kuhusu
utamaduni, Huang alimwambia Makamu wa Rais, kuwa wamekuwa wakitumia lugha ya
Kiswahili katika mawasiliano baina ya Watanzania na wachina huku pia akisifia
Kiswahili kuwa kimeshika nafasi kwenye vyuo vingi vya China na kuifanya kuwa
lugha inayozumzwa na raia wa China.
No comments:
Post a Comment