MAKALA
BAADA ya mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi kuendelea
kujitokeza kwa kasi ya kutisha, baadhi ya wadau hivi sasa wako katika mchakato
wa kufanya maandamano ya amani.
Maandamano hayo ya amani yanatarajiwa
kufanyika mwanzoni mwa Machi mwaka huu, ambayo yatakuwa ya nchi nzima na
yamelenga kupinga ukatili huo na kuishinikiza serikali kuwachukulia hatua kali
wote wanaohusika.
Kwani tangu kuibuka kwa mauaji
hayo mwaka 2006, hadi hivi karibuni alipouawa mtoto Yohana Bahati, albino 76
wamekwisha kuuawa kikatili na watu wasiojulikana.
Mauaji hayo yanailetea nchi aibu
katika jumuia ya kimataifa na kuifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza
kwa uchawi.
Vitendo hivyo vya mauaji ya albino kwa kiasi kikubwa vinahusishwa
na imani za kishirikina.
Matokeo ya vitendo hivyo, kuendelea kutokea huku kukiwa hakuna
ufumbuzi wa kukomesha ukatili huo umefanya hadi mashirika ya Umoja wa Mataifa
kuingingilia kati.
Shirika ambalo limejitokeza na kupaza sauti ni lile la Maendeleo
(UNDP), ambapo limetaka serikali
kukomesha mashambulio hayo.
Kutokana na tatizo hili kuzidi kuwa sugu wadau hao sasa wameanza
mchakato wa maandalizi ya maandamano ya amani ili kuweza kupeleka kilio chao
kwa rais aweze kushauriana nao kwa ajili ya kupata suluhu ya kudumu
itakayomaliza tatizo hili.
Katika maandamano hayo pia kutafanyika sala maalumu kwa ajili
ya wote waliopoteza maisha yao kwa kuuawa kikatili.
Katika hili ni vema kila mmoja wetu ambaye anaheshimu haki za
binadamu akajitokeza kuwaunga mkono ndugu zetu katika kupinga mashambulizi
dhidi yao.
Sitarajii kama kutakuwa na pingamizi lolote kuhusu maandamano
hayo, ambayo yana ujumbe muhimu.
Nasema hivyo, kwa vile kuna tabia ya Jeshi la Polisi kupenda
kuingilia kati kila yanapotaka kufanyika maandamano tena bila kuangalia
kinachopiganiwa na makundi husika.
Mbaya zaidi jeshi hilo limekuwa likiyapiga marufuku maandamano
siku moja kabla, huku wahusika wakiwa wameshapeleka barua ya kuomba kibali
mapema.
Kwa vile tukio la maandamano ya albino ni tofauti na mengine,
huku wakiwa tayari zaidi ya wiki moja wamekwisha kutoa taarifa, sidhani kama
itakuwa ni busara kwa polisi kusubiri hadi ibakie siku moja ndipo watangaze kuyasimamisha.
Cha msingi ni jeshi hilo kujiandaa katika kuwapa ulinzi wa
kutosha wadau hao ili waweze kufikisha ujumbe wao kwa wanaohusika.
Pia niwatahadhalishe baadhi ya watu ambao mara nyingi hupenda
kuvamia makundi ya maandamano kwa lengo la kuanzisha vurugu ambazo zitawafanya
wapate nafasi ya kufanya uhalifu.
Kwani kama wapo watakaojitokeza kwa nia hiyo watambue wadau hao
wamejipanga kuwaumbua kabla ya polisi hawajawashughulikia.
Huu si wakati wa kuyafanyia dhihaka maandamano haya, kwani yana lengo
la kupigania haki ya utu wa mwanadamu ambao wanaishi kwa mashaka makubwa katika
nchi yao.
No comments:
Post a Comment