VIONGOZI
mbalimbali wa kitaifa na wabunge, wamesema kifo cha mbunge wa Mbinga Magharibi,
Kepteni John Komba ni pigo kwa Taifa hususan kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Komba
alifariki dunia juzi katika hospitali ya TMJ, alipopelekwa baada ya kuzidiwa
ghafla akiwa nyumbani kwake Mbezi Beach, jijini Dar es Salaam.
Wakizungumza
na waandishi wa habari jana nyumbani kwa marehemu, viongozi hao walisema hakuna
aliyetarajia kifo hicho, lakini hakuna wa kumlaumu kwani ni kazi wa Mungu.
Membe
Waziri
wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernad Membe, alisema msiba wa
Komba si wa Watanzania, bali umegusa ukanda mzima wa Afrika Mashariki.
Membe
ambaye pia ni Mbunge wa Mtama, alisema licha ya kuwa nembo ya upendo na
ushirikiano katika chama, lakini pia alikuwa akishirika hata katika masuala ya
kimataifa, kwani alikuwa akitafuta ufumbuzi wa mgogoro wa kugombea mpaka katika
Ziwa Nyasa, uliyojitokeza kati ya Tanzania na Malawi.
“Kepteni
Komba ametoweka haraka kama mshumaa, kwa kweli hili ni pigo ambalo halitaweza
kusahaulika mara moja kwetu sisi Watanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla,”alisema
Membe.
Makinda
Spika wa Bunge, Anna Makinda, alisema
Komba alikuwa mcheshi na muwazi, pindi anapokuwa na jambo analisema hadharani
bila hofu yoyote na ndio maana alipendwa na wabunge wenzake pamoja na wananchi.
Makinda ambaye pia ni Mbunge wa
Njombe Kusini, alisema kifo hicho kimekuwa cha ghafla kutokana na kutokujua
kama alikuwa anaumwa ugonjwa wowote hadi pale umauti ulipomkuta.
“Nimemfahamu muda mrefu sana,
kabla hajawa mbunge, pia mimi ndiye niliyemshauri agombee ubunge nilipokuwa
mkuu wa mkoa, hivyo ni pigo na simanzi kubwa ndani ya chama,” alisema.
Alisema kutokana na Kapteni Komba
kufariki dunia katika kipindi muhimu ambacho chama kilikuwa kikimuhitaji, na
kuomba Mungu awajaalia mtu mwingine atakayeziba pengo lake.
Dk. Slaa
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (Chadema), Dk. Wilbrod Slaa, amesema kifo cha Komba
kimekuwa pigo kubwa kwa taifa, kwani hakuna asiyemjua kutokana na kazi zake.
“Tunapokuja duniani hatuombi wala
hatupigi hodi, pia tunapondoka ni hivyo hivyo hatuwezi kulaumu kazi ya Mwenyezi
Mungu, kwani ameshaamua.
“Nafarijika kwamba ameondoka
akiwa sahihi, kwani amejiandaa vizuri nikiwa na mana kiroho, hivyo Mwenyezi Mungu
atampokea vema anapokwenda,”alisema.
Mwigulu
Naibu
Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, alisema
kifo cha Kepteni Komba hataweza kukisahau kwa vile alikuwa mtu aliyewahi
kumsaidia katika kupata ushindi kwenye jimbo lake.
Nchemba
ambaye pia ni Mbunge wa Iramba Mashariki, alisema nyimbo zake alizoimba wakati wa
kampeni ziliweza kuwavuta kwa wingi na kusikiliza sera za chama chao hatimaye
kupigia kura za ushindi.
“Kaptein
Komba alitengeneza nembo ya chama chetu, kwa kweli ameondoka katika kipindi
muhimu ambacho tulikuwa tukimtegemea,”alisema Nchemba.
Nasari
Mbunge
wa Arumeru Mashariki, Joshua Nasari, alisema msiba huo umemshitua, kwani alikuwa hajui kama Komba alikuwa
anaumwa.
Alisema
hivi karibuni Kamati ya Maendeleo na Jamii ambayo wako pamoja ilikuwa ifanye
ziara nchini Ethiopia, hivyo kutokana na msiba huo ziara hiyo imeahirishwa.
Nape
Katibu
wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alisema baba yake mzazi (Mzee Nnauye)
alishawishi Komba kujiunga na CCM kutoka na ushawishi alikokuwa nao.
“Kifo
hiki kimefanya ziara ya Katibu Mkuu wa CCM iahirishwe hadi Jumatano ijayo,” alisema.
Ngeleja
Mbunge
wa Sengerema, William Ngeleja, alisema taifa limepoteza mpiganaji wa kweli, kwani
Komba alikuwa kiongozi mwenye msimamo katika yale aliyoyaamini.
“Nafikiri
huu ni wakati wa msiba haipendezi kwa baadhi ya watu kufanya mzaha katika
mitandao ya kijamii kwani si ustaarabu
wa Watanzania, kwani sisi sote tutapita njia hii,” alisema Ngeleja.
Migiro
Waziri wa Katiba na Sheria, Asha-Rose
Migiro, alisema kifo hicho ni pigo ndani ya CCM, kwani Komba alikuwa na mchango
mkubwa.
“Marehemu aliunganisha taifa
kupitia nyimbo zake mbalimbali, hasa katika kipindi cha msiba wa Mwalimu Julius
Nyerere, pia alikuwa na moyo wa kujituma,”aisema.
Ratiba
ya mazishi
Mwili
wa marehemu ulifikishwa nyumbani kwake jana jioni na leo kuanzia saa 2 asubuhi ndugu na jamaa watapata
fursa ya kuuaga.
Kwa
mujibu wa ratiba hiyo, saa nne asubuhi, mwili wa marehemu utapelekwa katika
viwanja vya Karimjee, Dar es Salaam kwa ajili ya kuagwa na viongozi wa kitaifa na
wananchi.
Baadaye
mwili huo utapelekwa uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA) majira ya
saa 9:30 kwa ajili ya kusafirishwa kuelekea mkoani Ruvuma kwa mazishi
yatayofanyika kesho kijijni kwake Lituhi, mkoani Ruvuma.
mwisho
No comments:
Post a Comment