KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Friday, 6 March 2015

SALIBOKO NAYE HUYOO AKIMBILIA MAHAKAMANI

OFISA Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA), Philip Saliboko, amepinga kuhojiwa na Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma na baadala yake amekimbilia Mahakama Kuu kuweka pingamizi.

Saliboko anatuhumiwa kupokea mgao wa sh. milioni 40.4 kutoka kwa mmiliki wa kampuni ya VIP Engineering and Marketing Limited, James Rugemalira, kinyume cha sheria ya maadili ya viongozi wa umma.
Mgao wa fedha hizo zinadaiwa kuwa ni sehemu ya fedha zaidi ya sh. bilioni 300 zilizochotwa kifisadi  kutoka akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Hatua ya ‘kukimbilia’ Mahakama Kuu jana, ilichukuliwa baada ya Jaji Hamisi Msumi, kutupilia mbali pingamizi la awali la kuzuia malalamiko hayo kusikilizwa na baraza hilo, yaliyowasilishwa na Saliboko kupitia Wakili wake, Jamhuri Johnson.

Wakili Jamhuri aliwasilisha pingamizi hilo baada ya Wakili wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Hassan Mayunga, kuwasilisha malalamiko hayo dhidi ya Saliboko mbele ya baraza hilo na kuzua malumbano ya kisheria yaliyodumu takribani dakika 30 kati ya mawakili wa pande mbili.

Wakili Jamhuri aliwasilisha pingamizi hilo baada ya Saliboko kukana malalamiko yote yaliyowasilishwa na Wakili Mayunga dhidi yake.

Akiwasilisha pingamizi hilo, Wakili Jamhuri alidai baraza halina uwezo wa kusikiliza malalamiko dhidi ya mteja wake kwa madai kwamba  kuna amri ya zuio iliyotolewa na Mahakama Kuu kwa chombo chochote cha umma kushughulikia suala lolote linalohusu kampuni ya kufua umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) pamoja linalohusu akaunti ya Tegeta Escrow.

Alidai zuio hilo lilitolewa kupitia kesi ya msingi namba 5 ya mwaka 2014 iliyofunguliwa na IPTL na wenzake dhidi ya Waziri Mkuu na wenzake saba na kwamba, baraza lina nakala ya amri hiyo.

Hatua iliyochukiliwa na Saliboko ni kama ile iliyochukuwa na mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge alipofikishwa mbele ya baraza hilo zaidi ya wiki moja iliyopita.

Hata hivyo, wakati Wakili Jamhuri akiendelea kutoa hoja kutetea pingamizi la mteja wake, Jaji Msumi aliingilia kati na kumweleza kuwa katika shauri dhidi ya Chenge, waliona baraza lina uwezo wa kusikiliza kwa sababu baraza si sehemu ya waliopewa amri hiyo ya zuio na Mahakama Kuu.

Kauli ya Jaji Msumi ilijibiwa na Wakili Jamhuri, ambaye alidai amri ya zuio hilo inavihusu vyombo vya umma na kwamba, baraza ni chombo cha umma, ambavyo vimezuiwa kuendelea kushughulikia suala hilo hadi kesi hiyo ya msingi iliyopo Mahakama Kuu itakaposikilizwa na kuamuliwa.
  
Hoja hizo za Wakili Jamhuri zilipingwa na Wakili Mayunga, ambaye alidai baraza limeshaamua pingamizi kama hilo, hivyo haliwezi kuwa na mamlaka tena ya kuamua.
  Wakili Mayunga pia alidai kwa mujibu wa katiba ya nchi, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma ni idara inayojitegemea na kwamba, amri ya zuio hilo la Mahakama Kuu si ya dunia nzima na kwa hiyo, haifanyi kazi dunia nzima.

Hoja hizo za Wakili Mayunga zilipingwa na Wakili Jamhuri, ambaye alidai suala la Saliboko haliwezi kufananishwa na la Chenge kwa kuwa bado halijaongelewa katika baraza na kwa hiyo, uamuzi wa baraza wa kutupa pingamizi, unaweza kufanya kazi katika shauri la Chenge na siyo kwa mteja wake (Saliboko).

Hata hivyo, Wakili Jamhuri hakukubaliana na uamuzi Jaji Msumi wa kutupilia mbali pingamizi la mteja wake, hivyo akaliomba liruhusu waende Mahakama Kuu kuomba marejeo, ili kupata tafsiri sahihi juu ya amri ya zuio hilo.

Jaji Msumi alikubaliana na ombi hilo la Wakili Jamhuri na hivyo, akaamua kusitisha usikilizaji wa malalamiko dhidi ya Saliboko hadi ombi la marejeo ya amri ya zuio hilo la mlalamikiwa litakapotolewa uamuzi na Mahakama Kuu.

Awali, akiwasilisha malalamiko katika baraza hilo dhidi ya Saliboko, Wakili Mayunga, alidai Saliboko alikiuka sheria ya maadili ya viongozi wa umma kwa kuomba fadhila za kiuchumi kutoka kwa Rugemalira.

Alidai mlalamikiwa alipokea zaidi ya Sh milioni 40.4 zilizoingizwa kwenye akaunti yake iliyofunguliwa katika Benki ya Mkombozi, tawi la St. Joseph, jijini Dar es Salaam Februari 5, mwaka jana.

Wakili Mayunga alidai Saliboko, ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Rita, aliteuliwa na Mahakama Kuu kuwa Mfilisi wa muda wa mali za IPTL, iliyokuwa na mkataba na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), ambalo ni taasisi ya umma la kuongeza uzalishaji wa umeme nchini.

Alidai kitendo cha mlalamikiwa kupokea fedha hizo kutoka kwa Rugemalira, ni ukiukwaji wa sheria ya maadili ya viongozi wa umma.
 Wakili Mayunga alidai pia kuwa mlalamikiwa alijipatia manufaa ya kifedha na hakutamka fedha hizo kwa mujibu wa sheria.

Uamuzi wa Munujangoma

Kwa upande mwingine, baraza hilo limekubali pingamizi la kutosikiliza kesi ya Mkurugenzi wa Huduma za Sheria katika Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Rogonzibwa Mujunangoma.

Mujunangoma alifikishwa mbele ya baraza hilo akidaiwa kujipatia manufaa ya kifedha kiasi cha sh milioni 423.4 kwa ushauri anaoutoa katika Kampuni ya VIP na Mabibo Wines and Spirit kinyume cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Pingamizi hilo lilikubaliwa jana  na Mwenyekiti wa Baraza hilo Jaji Msumi, alisema kuwa baraza limepitia hoja za msingi za mlalamikiwa na kujiridhisha.

Jaji Msumi alisema hoja ambayo imeonekana kuwa na msingi wa kisheria iliyochangia kulishawishi baraza kukubali pingamizi hilo ni ukweli kwamba Mujunangoma amefunguliwa mashitaka katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ambayo ndiyo yale waliyomfungulia katika baraza la maadili.


“Sheria inakataa mshtakiwa akiwa na kesi katika sehemu mbili kwa wakati mmoja yenye malengo yale yale kwenye vyombo tofauti inamkosesha nafasi ya kujitetea,” alisema.

No comments:

Post a Comment