KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Wednesday, 22 April 2015

HEKTA 400,000 ZINAPOTEA KILA MWAKA


Makamu wa Rais, Dk. Bilal

HEKTA 400,000 za misitu zimekuwa zikipotea kila mwaka kutokana na uelewa mdogo wa wananchi katika kutumia rasilimali hizo bila kuzingatia matumizi endelevu.
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Dk. Binilith Mahenge, alitoa kauli hiyo wakati akimkaribisha Makamu wa Rais, Dk. Mohammed Gharib Bilal, katika uzinduzi wa Ripoti ya pili ya hali ya Mazingira nchini ya mwaka 2014, uliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.
 Alisema, uharibifu huo umechangiwa na kutozingatiwa sheria na kanuni za hifadhi ya mazingira katika ngazi mbalimbali.
 “Suala la sera, sheria na kanuni za hifadhi ya mazingira kutozingatiwa katika ngazi mbalimbali kumechangia pia katika uharibifu wa mazingira nchini,”alisema Dk. Mahenge.
 Dk. Mahenge, alisema takwimu za uchomaji moto hovyo kwa kipindi cha mwaka 2000 hadi 2014 zimeonesha kwamba,  katika kipindi hicho kumekuwa na matukio ya uchomaji moto takriban hekta 1,123,000.
 Aliitaja mikoa iliyoathirika na moto huo kuwa ni Rukwa, Kigoma, Tabora, Mbeya, Ruvuma, Lindi na Morogoro.
 “Kwa mfano asilimia 50 tu ya miji mikubwa ina mifumo ya majitaka amabayo inahudumia asilimia nane tu ya wakazi wa miji hiyo hali hii inachangia kwa kiasi kikubwa cha uchafuzi wa mazingira,”alisema Dk. Mahenge.
 Dk. Mahenge, alisema athari nyingine zinazotokana na uchafuzi wa mazingira ni pamoja na; kuonezeka kwa magonjwa ya mlipuko kama vile kuhara damu na kipindupindu ambayo huchangia asilimia 60 hadi 80 ya matukio ya magonjwa na kiongezeka kwa gharama za kutibu maji ya kunywa.
 Aliongeza kwa kusema kuwa uharibifu wa rutuba ya ardhi umechangia uvunaji hafifu wa mazao katika mikoa ya Dodoma, Shinyanga, Tabora na Singida.
 Dk. Mahenge, alisema uharibifu huo wa ardhi umechangia pia kuongezeka kwa migogoro ya ardhi inayohusisha jamii za wafugaji na wakulima, ambayo imesababisha maafa makubwa katika jamii hizo ikiwemo vifo.
Aliyataja baadhi ya maeneo yaliyokumbwa na migogoro hiyo ni Rufiji mkoani Pwani, Kilosa na Kilombero (Morogoro), Kiteto (Manyara) na Mbarali (Mbeya).
 Naye  Dk. Bilal, alisema uharibifu wa mazingira katika nchi zinazoendelea ni kati ya sababu zinazofanya nchi hizo ziendelee kuwa masikini.
 Alisema uko uhusiano mkubwa kati ya mazingira na umasikini kwa maana ya kwamba uharibifu wa mazingira unachangia kuongezeka kwa umasikini, hivyo kadri ya hali ya umasikini inavyoongezeka inasababisha pia kuharibika kwa mazingira.
 “Kwa maana hiyo umuhimu wa kulinda na kuhifadhi mazingira nchini unachochewa zaidi na ukweli kwamba mazingira ni muhimu sana katika ustawi wa maisha yetu,”alisema Dk, Bilal.
 Aidha, mazingira ni mhimili wa sekta za uzalishaji kama vile kilimo, utalii, uvuvi na madini.
 Dk. Bilal, alisema changamoto iliyoko ni kuhakikisha mazingira na maliasili hizo zinatumka katika njia endelevu kwa kuzingatia uwiano mzuri.

No comments:

Post a Comment