KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Tuesday, 28 April 2015

MISWADA YOTE ITATIWA SAINI-IKULU


KURUGENZI ya Mawasiliano Ikulu imesema hakuna sababu ya kumzuia Rais Jakaya Kikwete asitie saini miswada ya Sheria ya Makosa ya Matumizi mabaya ya Mitandao na Sheria ya Takwimu kwa kuwa imepitia hatua zote muhimu hadi kupitishwa na Bunge.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Ofisi ya Rais Ikulu, Salva Rweyemamu, alisema Rais Kikwete atatia saini ili kuifanya kuwa sheria na iwapo kutakuwa na matatizo yanaweza kujadiliwa baadaye.
“Kama tunakubaliana kuhusu ukubwa wa matatizo hasa ya ugaidi, mambo mengi ya ugaidi yanapitia katika mitandao.
Ni wazi kwamba hapa kwetu sheria hii imechelewa sana, kwa sababu imefikia hatua watu wanatumia mitandao hii kutukanana, kudhalilishana na kunyanyasana.
Rais atatia saini na kama kuna tatizo, marekebisho yatafanyika baadaye,” alisema.
Alisema ni wazi kwamba sheria hizo hazikulenga kuminya wala kupunguza uhuru wa habari na mawasiliano katika mitandao ya simu na intaneti bali kinachofanyika ni kuweka udhibiti kwa watumiaji, hasa wale wenye nia mbaya ya kutumia visivyo mitandao hiyo, kwa faida ya umma.
Alisema haitakuwa mara ya kwanza kwa sheria hiyo kupitishwa na kufanyiwa marekebisho, kwa kuwa zipo baadhi ya sheria zilizowahi kufanyiwa marekebisho katika baadhi ya vipengele vyake.
Salva alieleza kwamba katika hili, usalama wa nchi ndilo suala namba moja, huku masuala mengine yanayohusu uhuru wa habari yakifuatia, kwa kuwa bila usalama hakuna uhuru wa jambo lolote.
Akizungumzia kuhusu sheria ya vyombo vya habari, alisema serikali ililazimika kusikiliza kilio cha wadau japokuwa ni kweli kwamba muswada huo ulioanza miaka 10 iliyopita umeshapita kwenye mikono ya wadau mara nyingi.
Alisema serikali inatambua kwamba miswada ya sheria za habari zimekuwa zikikandamiza uhuru wa habari, ndiyo maana imeendelea kusisitiza umuhimu wa kupata sheria mpya itakayotoa uhuru zaidi kwa vyombo hivyo na wanahabari.

Ziara ya Rais Jordan

Akizungmzia ziara ya siku moja ya Rais Kikwete nchini Jordan, alisema ujumbe wake ulikwenda nchini humo Aprili 18, mwaka huu kwa mwaliko wa Mfalme Abdulla ili kushiriki katika mkutano wa viongozi wa kidunia uliohusu masuala ya usalama, ulinzi na namna ya kudhibiti ugaidi, ambao ulipaswa kuwa siri.
Alisema ofisi yake haikutoa taarifa kuhusu safari hiyo ya Rais kwa kuwa Jordan iliomba mkutano huo uwe siri kutokana na nchi hiyo kuzungukwa na nchi ambazo si salama, ikiwamo Syria, Iraq, Palestina, Saudia, Israel na Misri.
Wakati huo huo, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, amesema Muswada wa Sheria ya Takwimu uliopitishwa na Bunge hivi karibuni hautawazuia watafiti kufanya tafiti zao kwa ajili ya matumizi yao na taifa.
Waziri Mkuu Pinda alitoa kauli hiyo kutokana na wasiwasi ulioonyeshwa na watafiti kuhusu Muswada wa Sheria ya Takwimu uliopitishwa na Bunge pamoja na Sheria ya Makosa ya Mtandaoni wakati wa kongamano lililoandaliwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS).
Akizungumza katika kongamano hilo lililoanza jana jijini Dar es Salaam na kuwakutanisha wataalamu wa Sekta ya Takwimu wa Bara la Afrika, Pinda alisema sheria hiyo inatokana na mtazamo wa dunia kuwa eneo hilo linapaswa kusimamiwa na vyombo vya serikali.
Waziri Mkuu Pinda alisema sheria hiyo  imetengenezwa kutokana na mifumo ya mazingira ya nchi nyingine duniani, lakini zikijitokeza changamoto huko mbele ya safari kuna uwezekano wa kuboreshwa ili kwenda na wakati.
“Takwimu zinazotolewa lazima ziwe na viwango vya kimataifa kwa ajili ya yeyote atakayezitumia, awe na uhakika, tena bila ya kuhoji,” alisema.
Akizungumzia kongamano hilo, Waziri Mkuu Pinda alisema limezikutanisha nchi zinazozungumza lugha ya Kiingereza na Kifaransa.
Alisema lengo lake ni kuendeleza msukumo wa kuzitaka serikali zote za nchi zinazoendelea kwa kutoa msukumo wa kipaumbele katika sekta hiyo ya takwimu.
Alisema nchi inapokuwa na takwimu sahihi inaweza kupanga mipango yake ya maendeleo kwa uhakika zaidi.
Waziri Mkuu Pinda alisema serikali itaijengea uwezo taasisi yake ili iweze kutoa takwimu zenye ubora na viwango vya kimataifa.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa NBS, Albina Chua, alisema taasisi zote nchini zinaruhusiwa kufanya utafiti lakini lazima ziwe na viwango vinavyotakiwa ili zitumike katika kupanga maendeleo ya nchi.

CHANZO TANZANIA DAIMA

No comments:

Post a Comment