KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Friday, 10 April 2015

TAMESCO YASEMA HAKUNA MGAWO WA UMEME


SHIRIKA la Umeme Tanzania (Tanesco) limetangaza kuwa hakutakuwa na mgawo wa umeme katika maeneo yote ya jiji la Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Tanesco, Felchesmi Mramba, alisema matengenezo yanayoendelea ya kusafisha visima vya gesi asilia Songosongo hayataleta madhara yoyote wala kuwepo kwa mgawo wa umeme.

Alisema ni muhimu wananchi kufahamu kuwa matengenezo hayo yameshaanza na hakuna usumbufu uliojitokeza wa kukatika kwa umeme.

“Naomba wananchi mjue kuwa hatujatangaza mgawo wa umeme, bali kuna matengenezo ambayo yanaendelea hivi sasa ya kusafisha visima vya gesi, hivyo ni kitu cha kawaida wakati matengenezo yakiendelea kutokea matatizo madogo madogo yasiyoweza kusababisha mgawo wa umeme,” alisema.

Mramba alisema hali ya mitambo na miundombinu ya usambazaji wa umeme jijini imechakaa hivyo kwa sasa wanajenga mipya yenye uwezo mkubwa zaidi wa kuhifadhi umeme.

Akivitaja baadhi ya vituo vilivyokamilika kuwa ni Kipawa, Gongo la mboto, Mbagala na Kurasini, ambavyo vimeshaanza kutoa huduma. 

Akizungumzia mvua zilizonyesha hivi karibuni, Mramba alisema zilisababisha baadhi ya nguzo za umeme kuanguka na nyaya kukatika.

“Tulipata matatizo mengi kipindi kile cha mvua, hivyo tumejitahidi kuzirekebisha nguzo zote, ili wananchi wapate huduma kama kawaida,” alisema.

No comments:

Post a Comment