| Baadhi ya vijana waliyokwama bandarini wakienda Zanzibar |
KUNDI la vijana 35 waliokuwa
wakisafirishwa kwenda kufanya kazi za mashamba Zanzibar leo walikwama
bandarini baada ya kukosa usafiri.
Muonekano wa vijana hao wenye umri kati
ya miaka 16 hadi 30 ulikuwa hauna tofauti na ule wa vijana waliokuwa
wakikamatwa nchini wakitokea katika nchi za Ethiopia, Somalia na Eretria.
Vijana hao ambao wametoka Shinyanga,
Simiyu, Mwanza, Tabora na Geita walikwama bandarini hapo baada ya kukosa tiketi
kutokana na meli zote kujaa abiria ambao walikuwa wakienda Zanzibar kwa ajili
ya mapumziko ya Sikukuu ya Pasaka.
Kiongozi wa kundi hilo, Mangu Zizi,
alisema hawakuweza kusafiri kama walivyokusudia kwa sababu walikuwa hawajakata
tiketi mapema na waliambiwa kuwa wangesafiri baada ya siku tatu.
“Hata hivyo, tuliambiwa kama tunataka
kusafiri leo tutoe sh. 50,000 kila mmoja wakati sisi tuna sh. 25,000 kwa kila
mmoja wetu.
“Tumefika hapa tangu asubuhi hadi
sasa (mchana) hatujakula chochote
kutokana na hela tulizo nazo ni kidogo na tukikosa usafiri kabisa tutakwenda
kulala Kituo cha mabasi Ubungo,” alisema Zizi.
Zizi alisema imekuwa ni kawaida kwa
vijana wa Kanda ya Ziwa kusafiri kwenda Zanzibar na kwamba wakifika watatawanyika
kwa wengine kwenda Pemba na wengine kubaki Unguja.
Zizi alimtaja mwenyeji wao kuwa ni
Kassim Kolofwa, ambaye ndiye atakayewapokea wakati watakapofika Zanzibar.
Hata hivyo, alipotafutwa Kolofwa kwa
njia ya simu jana alisema kati ya vijana hao anaowafahamu kuwa ni vijana wake ni watatu ambao ni Mangu
Zizi na mdogo wake Jitu na mwenzao na kusema kuwa wengine hawatambui.
Alisema vijana hao wanapofika huko
wanafikia kwa sheha na kukabidhisha vitambulisho vyao kwa ajili ya kupata
kibali cha kuendelea kuishi visiwani humo.
Kolofwa alisema hiyo si mara ya kwanza
kwa vijana kutoka Bara kwenda Zanzibar kwa ajli ya kufanya kazi za vibarua
mashambani.
Usafiri wa Kwenda Zanzibar tangu juzi
umekuwa mgumu hadi kufanya baadhi ya abiria kulalamikia hali hiyo.
No comments:
Post a Comment