KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Wednesday, 6 May 2015

NAGU: ACHENI KAMPENI MUDA BADO









WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu) Dk. Mary Nagu kuacha kufanya kampeni mapema kabla ya chama hakijatoa tamko rasmi la kuwataka wanachama wake kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi.
        
Dk. Nagu ambaye ambaye pia ni Mbunge wa Hanang’ mkoani Manyara kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), alitoa juzi wakati alipozungumza na wandishi jijini Dar es Salaam juzi.

Alitoa maelezo hayo  kufuatia kutolewa kwa kauli ya kuwataka wakazi wa Hanang, kumuunga mkono mwanasheria wa Kampuni ya FW Law Chambers Advocates ya jijini Dar es Salaam, Duncan Mayomba kama ataridhia ushauri wa Waziri Mkuu mstaafu Frederick Sumaye wa kugombea Ubunge katika jimbo hilo.

Hivi karibuni Sumaye katika mkutano wa hadhara uliofanyika Hanang’ aliwataka vijana wasomi, akiwemo Mayomba, kujitokeza na kugombea Ubunge katika jimbo hilo.
 Waziri Dk. Nagu alisema ni mapema mno kufanya kampeni wakati huu, kwani  kufanya hivyo ni kukiuka maadili na taratibu zilizowekwa na Chama kwa wanachama wake.

Taratibu hizo kwa mujibu wa Dk. Nagu ni  kutokushiriki katika kufanya  kitendo cha aina yoyote  kile kitakachoashiria kufanya kampeni mapema mpaka hapo Chama cha mapinduzi  kitakapotangaza rasmi.
“Ninasikitishwa sana na mambo yanayotokea Hanang’ nashindwa kupata picha halisi kama ni kweli mtu unayemheshimu kufanya vitendo vinavyofanywa na  kiongozi wa  kitaifa kuendesha kampeni ya kuwashawishi wananchi kumchagua mtu anayemtaka yeye kwa maslahi yake na wala siyo kwa maslahi ya watu wote”, alisema Dk. Nagu.
Alisema kuwa haogopi wala hatishwi na matendo yanayofanywa jimboni kwake, lakini kitu kikubwa kinachomfanya  kujiamini  ni pamoja na kutembea kifua mbele kwa wananchi wake kutokana na  jinsi alivyotumia vizuri muda wake mwingi  jimboni humo katika kutekeleza kivitendo Ilani ya (CCM).
Aidha, alisema kuwa kutokana na imani hiyo ndiyo iliyosababisha kuteuliwa kuwa Mjumbe wa Halmashauli Kuu ya (CCM) MNEC.
 Dk. Nagu alisema kuwa wananchi wanahitaji maendeleo na siyo sifa ya mtu, eti kwa sababu kijana au msomi. “Wananchi wanataka maji, shule bora, miundombinu imara na huduma bora za kiafya kama hospitali na dawa ili yawasaidie katika kuboresha maisha yao”, aliongeza.
“Nimeweza kujitahidi kadri ya uwezo wangu kutekeleza mambo yote muhimu yanayohitajika kwa wananchi.

 “Nimetumia nafasi zangu serikalini kuwashawishi wawekezaji kuwekeza jimboni kwangu, nimefanikisha kufanyika kwa miradi mikubwa ukiwemo ule wa kuwapatia wakulima matrekta”.
Kiongozi huyo wa serikali alisema kuwa ameweza kuanzisha vikundi  vingi  vya akinamama vya Kuweka na Kukopa  (VICOBA) pamoja na SACCOS, kuanzisha vikundi vya vijana vya kilimo cha kisasa na kuwapatiwa matrekta na pembejeo.



No comments:

Post a Comment