WAZIRI wa Kilimo, Chakula
na Ushirika, Stephen Wasira, amesema hali ya chakula nchi ni yakuridhisha.
Wasira alitoa kauli hiyo,
juzi wakati wa akipokea msaada wa tani 7,492.7 za mbolea ya urea wenye thamani
y ash. bilioni 5.7 kutoka nchini Japan.
Alisema hivyo kwa vile hadi
sasa nchini kuna zaidi ya tani 300,000 za chakula ambazo zinaweza kusaidia
kuziba pengo katika maeneo mengine ambayo yanaweza kukumbwa na upungufu wa
chakula.
“Unajua kuna kipindi kama
hiki cha mwezi Mei inaweza ikatokea upungufu wa chakula, lakini kinakuwa
kipindi kifupi kwani wakati huo wanajiandaa na msimu wa mavuno,”alisema Wasira.
Wasira, alisema hali ya
chakula mashambani katika mikoa 16 hivi sasa ni nzuri, hivyo basi serikali
inajiandaa wakati ukifika Julai mwaka huu itaanza kununua mazao hayo.
“Kupanda kwa bei ya chakula
kunakuwa kwa muda mfupi hususan katika kipindi cha Mei, mara baada ya kuvuna
Mwezi Julai hali hurejea katika hali ya kawaida,”alisema Wasira.
Akizungumzia msaada huo wa
mbolea, Wasira alisema mbolea hiyo itasambazwa katika maeneo mbalimbali ya
nchini kwa ajili ya kuimarisha hali ya uzalishaji wa chakula.
“Tumekuwa na ushirikiano na
Japan katika miradi mbalimbali ya kilimo tangu mwaka 1978,”alisema Wasira.
Naye Balozi wa Japani
nchini, Masaharu Yoshida, wakati akikabidhi msaada huo, alisema anatarajia kuwa
msaada walioukabidhi, usiishie kusambazwa bali ulete matokeo chanya.
Alisema, msaada huo,
utaongeza kasi ya uzalishaji wa chakula kitendo kitakachosaidia kupunguza
umasikini na kufanya nchini iwe salama zaidi kichakula.

No comments:
Post a Comment