![]() |
| Prof. Kamuzora |
WATANZANIA wametakiwa kutumia mitandao
ya kijamii kupata taarifa mbalimbali na kuzitumia katika maendeleo.
Mjumbe wa Bodi ya Utendaji ya Kituo cha
Ushirikiano wa Kilimo na Maendeleo Vijijini cha nchi za Umoja wa Ulaya, Afrika,
Karebiani na Pasifiki (CTA), Prof. Faustin Kamuzora, alisema taarifa hizo zina
mchango mkubwa katika maendeleo ya sekta za kilimo, usindikaji, biashara na
ukuzaji wa masoko katika ukanda wa Afrika Mashariki na dunia nzima kwa jumla.
Akifungua mafunzo ya mawasiliano ya
mitandao ya kijamii jijini Dar es Salaam jana, alisema kuna kila sababu kwa Watanzania
kutumia mitandao hiyo kuchochea shughuli za uzalishaji na biashara.
“Mitandao hii imekuja kutuongezea
tija...inaokoa muda. Ikitumika vyema ina
faida kubwa,” alisema Kamuzora ambaye pia ni Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu
Mzumbe anayeshughulikia Utawala na Fedha.
CTA na Baraza la Nafaka la Afrika ya
Mashariki (EAGC) wanashirikiana kutoa mafunzo kwa wajumbe kutoka taasisi
mbalimbali kwa ajili ya kuwezesha matumizi ya mitandao ya kijamii.
Aliwataka wanasemina hao kupitia ujuzi
watakaoupata kuusambaza katika taasisi zao na kuwa tayari kuwapa wananchi
taarifa juu ya hali ya hewa, masoko na bei ya mazao ya nafaka, na mifugo
kupitia mitandao kama blogu, facebook na twitter.
Pia aliwataka wanapotumia mitandao hiyo
wakumbuke kufuata sheria inayoongoza katika sekta hiyo ndogo.
Kwa upande wake, Meneja Miradi wa EAGC,
Ikunda Terry, alisema baraza lao limeamua kuandaa mafunzo hayo kwa kushirikiana
na CTA kuwaleta wadau mbalimbali wanaojihusisha na teknolojia hiyo kuwafundisha
namna ya kupeleka ujumbe na elimu kwa jamii.
Wajumbe 30 kutoka taasisi mbalimbali
nchini wananufaika na mafunzo hayo ya wiki nzima.

No comments:
Post a Comment