KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Tuesday, 21 July 2015

GUNINITA, KINGUNGE WAPISHANA

Guninita
ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dar es Salaam, John Guninita amesema ni kosa kwa mwanachama wa chama hicho kupinga uamuzi wa mkutano mkuu  na vikao vingine vya ndani ya chama kwani ni utovu wa nidhamu.
Kauli hiyo ya Guninita inatafsiriwa kuwa ni sawa na kuipa kisogo kambi ya Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa ambayo hadi sasa imekuwa ikipinga uamuzi wa vikao vilivyompitisha mgombea urais kupitia chama hicho, Dk. John Mgufuli.
Hivi karibuni mwanasiasa mkongwe na kada wa CCM mwenye kadi namba 8, Kingunge Ngombale-Mwiru ambaye amekuwa ni miongoni mwa watu wa karibu wa Lowassa, alipinga mfumo uliotumika kuwachuja wagombea wa urais kupitia CCM.
Kingunge alisema Kamati ya Maadili huko nyuma ilikuwa ni chombo cha kuandaa taarifa, ili kuisadia Kamati Kuu katika kuwajadili wagombea lakini katika mchakato wa mwaka huu kamati hiyo imefanya kazi isiyowahusu kikatiba kwa kukata majina ya wagombea.
Alisema Kamati ya Maadili ya CCM yenyewe imekosa maadili ya kuheshimu katiba na taratibu za chama.
Alisema kamati hiyo haikuwa na madaraka ya kupeleka majina matano kwenye kamati kuu, ambayo ilipaswa kuhoji wagombea wote 38 badala yake kuna baadhi ya watu waliamua kuitumia Kamati ya Maadili kuandaa watu wao na kuwakata wengine kwa sababu zao.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana,  Guninita alisema kutokana na kanuni za chama hicho ni kosa kwa mwanachama kupinga uamuzi wa vikao vya chama hicho.
Guninita ambaye alikuwa mmoja wa wanachama waliotia nia kugombea Jimbo la Kilombero, alisema kamwe yeye kama mwanachama hai wa chama hicho hatapinga uamuzi wa vikao vya chama.
Alisema ameamua kujitoa kugombea kiti hicho kwa kile anachodai kuna mizengwe katika kupatikana kwa mgombea ndani ya chama hicho.
“Niliamua kugombea ubunge katika Jimbo la Kilombero, lakini baada ya kutafakari nimebaini kushinda kwangu ni kazi ngumu mno, nimeamua kujitoa kutokana na mchakato unavyokwenda lakini bado ni mwanachama halali wa CCM na nitamuunga mkono mgombea yeyote atakayepita.

“Mtu yeyote atakayepitishwa na chama lazima aheshimiwe, kwani hayo ni maamuzi ya vikao vya chama, kutoheshimu ni utovu wa nidhamu,” alisema Guninita. 


CHANZO TANZANIA DAIMA

No comments:

Post a Comment