KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Wednesday, 19 August 2015

WATU WATATU WAMEFARIKI DUNIA KUTOKANA NA UGONJWA WA KIPINDUPINDU

WATU watatu wamefariki dunia na wengine  34 wamelazwa katika vituo mbalimbali kutokana na kuugua ugonjwa wa kipindupindu jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda, alisema chanzo cha ugonjwa huo ni mkazi wa Ali Maua ambaye alifariki dunia nyumbani kwake Agosti 15 mwaka huu.
“Familia yake ilifanya msiba wa kawaida bila ya kuchukua tahadhari zozote, matokeo yake familia nzima iliambukizwa,” alisema Makonda.
Alisema watu watatu tayari wamefariki dunia na wengine 34 wamelazwa katika Hospitali za Mwananyamala  na Sinza.
Alisema watu 18 wakiwamo watoto 14 na wakubwa wanne wamelazwa katika Hospitali ya Mwananyamala huku Hospitali ya Sinza wagonjwa 16 ambao watatu ni wanawake na wanaume 13.
Makonda alizitaja kata zilizoathirika na ugonjwa huo kuwa ni  Kijitonyama, Kimara, Saranga, Manzese, Tandale, Makumbusho na Mwananyamala.
Alisema Manispaa ya Kinondoni imefungua kambi maalumu kwa ajili ya kuwahudumia wagonjwa  katika Zahanati ya Kijitonyama ambayo ni ya muda yenye uwezo wa kuchukua watu 30 na baadaye watahamishiwa katika kambi ya Mburahati.
“Sisi kama serikali ya wilaya tumejipanga vizuri kukabiliana  kikamilifu na ugonjwa huo, kwani tuna dawa na vifaatiba vya kutosha vya kukabiliana na ugonjwa huo.
“Tumefungua kambi yetu katika zahanati ya Kijitonyama ambayo ina dawa za kutosha na vifaatiba vyote vinayohitajika ,” alisema Makonda.
Makonda alitoa wito kwa wananchi wote kuzingatia kanuni za usafi ikiwa ni kunawa mikono baada ya kutoka chooni, kuchemsha maji ya kunywa, kula chakula cha moto na kuwahi mapema hospitali baada ya kuona dalili zozote za kuharisha au kutapika.

Alisema uzoefu unaonyesha kuwa wagonjwa wengi wanapoteza maisha kwa kuwa wanafika hospitali kwa kuchelewa hivyo kuwa vigumu kuokoa maisha yao.

No comments:

Post a Comment