KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Wednesday, 19 August 2015

WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI YAPIGA STOP USAFIRISHAJI WA BINADAMU

WIZARA ya Mambo ya Ndani kupitia Sekretarieti ya Kuzuia na Kupambana na Biashara Haramu ya Usafirishaji wa Binadamu imezuia zaidi ya taasisi 70 kusafirisha wafanyakazi wa ndani katika nchi za Uarabuni.
Hatua hiyo inatokana na kushamiri kwa biashara hiyo ambapo Tanzania inadaiwa kutumika kama njia ya kusafirisha wafanyakazi kwenda mataifa mengine.
Hayo yalibainishwa jana jijini Dar es Salaam na Katibu wa sekretarieti hiyo, Separatus Fella wakati wa kutoa mafunzo maalum kwa waandishi wa habari kuhusu mikakati na mapambano dhidi ya uharamu huo.
Alisema miongoni mwa taasisi ambazo zimezuiwa kufanya biashara hiyo haramu ni Mtemvu Foundation licha ya kuwa wana vibali halali kuwatafutia Watanzania kazi katika nchi mbalimbali.
“Hili katazo lilitolewa mwezi uliopita kwa sababu kubwa ya kushamiri kwa vitendo viovu wanavyofanyiwa Watanzania katika nchi za Uarabuni, ikiwemo kufanyishwa kazi ngumu na kutumikishwa kingono,”alisema.
Pia alisema hatua hiyo inatokana na taasisi hizo kushindwa kufuatilia taarifa za wafanyakazi hao pindi wanapokuwa katika nchi hizo, licha ya kuwa bado wakikabiliana na ‘vishoka’ ambao bado wanafanya biashara hiyo.
Naye Ofisa Mwandamizi wa sekretarieti hiyo, Alex Lupiya alisema mafunzo hayo yanalenga kutoa elimu kwa Watanzania ili kuzidisha mapambano dhidi ya biashara hiyo.
Alisema serikali imeridhia mikataba mbalimbali ya kimataifa na mwaka 2008 ilitunga Sheria ya Kuzuia Usafirishaji Haramu wa Binadamu ili kuhakikisha watu wanalindwa.
 “Licha ya kushirikiana na wadau wengine likiwemo Jeshi la Polisi na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa ajili ya kutoa elimu, bado tunakabiliwa na tatizo la fedha kwa ajili ya kuendeshea semina na vikao,”alisema.

No comments:

Post a Comment