MAMLAKA ya Usafiri wa nchi Kavu na Majini (Sumatra),
imesema kuwa itatangaza nauli ya Mradi wa Mabasi yaendayo Haraka (DART), kwa
sababu Serikali inataka mradi huo uanze kazi haraka iwezekanavyo. Hivi karibuni
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipinga viwango vya nauli vilivyopendekezwa kwani
alibaini kuwa havikutokana na misingi halisi ya gharama za uwekezaji na
uendeshaji. Viwango hiyo vilikuwa ni Mbezi-Kimara 700 (Mwanafunzi nusu ya nauli
ya hiyo) na Mbezi-Kivukoni 1,200 (Mwanafunzi nusu ya nauli) na Mbezi-Kimara-Ubungo-Mwenge
1,400 (Mwanafunzi nusu ya nauli).
Akizungumza na jijini Dar es Salaam leo,
Msemaji wa Sumatra, David Mziray, alisema hivi sasa wanaendelea kuyafanyia kazi
matakwa ya wadau kutoka pande zote zinazohusika. Alisema, hatua hiyo ya
kutangaza itakuja baada kukamilika ukokotoaji wa maombi yote yaliyofikishwa
katika ofisi yao, ambapo nia ni kutoa viwango vya nauli ambayo itakuwa na
manufa kwa pande zote yaani abiria na mmiliki.“Sisi tunajukumu la kuhakikisha kwamba tunaweka nauli ambayoitamfanya mmiliki aweze kuendelea kutoa huduma kwa sababu, huduma lazima iwe endelevu tusije kuweka ndogo sana kwa sababu ya kumfurahisha abiria na kumkwamisha mwendeshaji,”Mziray, alisema kuwa Sumatra kama Refarii, ni lazima waangaliye pande zote mbili, kwamba mwananchi asiumie, lakini vile vile mtoa huduma naye pia asiathirike hadi akashindwa kutoa huduma kutokana na kiwango kidogo cha nauli. “Tunajitahidi kumaliza haraka lakini chamsingi hatuwezi kuruka baadhi ya vipengere kwa sababu eti unataka kumaliza haraka tunataka kutoa viwango ambavyo vitafanya kazi na kuepuka malalamiko baadae Alisema baaada ya kupitia mikataba na nyaraka mbalimbali imebainika kwamba hakukuwa na Mpango wa Biashara ulioandaliwa na Mwekezaji yaani Kampuni ya UDART iliyopewa jukumu la kutoa huduma za mpito (ISP). Kingine ni gharama za uwekezaji (ununuzi wa magari, vifaa vya kutozea nauli na gharama nyingine) haziko bayana.
Januari 5, mwaka huu Majaliwa, alisema pamoja na kuwepo kwa kasoro hizi kubwa Mwekezaji aliwasilisha kwa Mamlaka ya Kudhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra), ombi la nauli za Mradi huo kama ilivyojionesha hapo juu. Kigezo kikubwa cha kupanga nauli pamoja na mambo mengine ni gharama za uwekezaji (capital costs) na gharama za uendeshaji (operational costs). Hivyo kwa kukosekana gharama halisi za Uwekezaji ni dhahiri kuwa viwango hivyo vya nauli vinavyopendekezwa havina uhalisi.
Waziri mkuu alisema tafsiri ya viwango hivyo vya nauli kwa mtumishi mwenye kima cha chini cha mshahara cha 260,000 kwa mwezi na amabaye ana mke na watoto wawili wanaosoma atatumia zaidi ya robo tatu (75%) ya mshahara wake kwa kulipa nauli. Alisema, Serikali iliyapinga mapendekezo hayo ya nauli kwa sababu gharama za Mwekezaji huyo hazifahamiki na hakuna Mpango wa Biashara unaoeleza mtiririko wa biashara ya Mabasi Yaendayo Haraka.
Kwa kuwa viwango hivyo vya nauli vilivyopendekezwa havikutokana na misingi halisi ya gharama za uwekezaji na uendeshaji na kwa vile watumiaji wa huduma za mabasi hayo wameonesha kutomudu viwango hivyo vya nauli, Serikali hairidhishwi na viwango hivyo kwa kuwa havina uhalisia, hivyo kuiagiza Sumatra kuendelea kujadiliana kuhusu kiwango hicho kilichopendekezwa .
No comments:
Post a Comment