MKUU wa Kituo cha Polisi Nyakanazi wilayani Biharamulo
mkoani Kagerea, ameingia matatani baada ya kudaiwa kuhusika katika kuibwa mbuzi
26 kati ya 33, wa mkazi wa kijiji hicho, Daud Kikwaba.
Tukio hilo linadaiwa kutokea Oktoba 12 mwaka jana katika
kijiji hicho, baada ya watu wanaodaiwa kuwa wezi kuvamia zizi la mwananchi huyo
nyakati za usiku na kuondoka na mbuzi hao.
Akizungumza na mwandishi jijini Dar es Salaam leo, Kikwaba
alimtaja Mkuu huyo wa kituo hicho kwa jina moja la Neligwa, ambaye hivi sasa
amehamishiwa kikazi kwenye kituo kingiene, anapaswa kutoa taarifa za kusaidia
kupatikana mbuzi wake.
Alisema, kuhusika kwake kumetokana na mkuu huyo ni kutoa
kibali kwa watu hao wanaodaiwa kuwa wezi ili waweze kusafirisha mbuzi hao,
ambao alikuwa akijua fika kwamba walikuwa wa wizi kwani mmoja wa wawezi hao
alikuwa anashikiliwa kituoni hapo.
“Kabla ya Mkuu huyo kutoa kibali, wezi hao walikwenda
kuomba kibali kwa Menyekiti wa Kitongoji cha Nyakanazi kwa ajili ya
kuwasafirisha kusikojulikana lakini mwenyekiti huyo aliwakatalia kutokana na
kuwatilia shaka watu hao.
“Mkuu huyo wa kituo anahusika kupotea kwa mbuzi hao 26 kwa
vile siyo muadilifu kwani baada ya kubaini kuwa mbuzi wale walikuwa wa wizi kwa
hiyo akaona hawana mwenyewe ndipo
alipoamua kushirikiana na wezi hao kuwachukuwa mbuzi hao 26 kisha kubakiza
mbuzi saba kituoni hapo,”alisema Kikwaba.
Kikwaba, alisema baada mkuu huyo kukamilisha mchezo huo
mchafu, aliamua kumuita kituoni hapo kwa ajili ya kuwatambua mbuzi waliokuwa
wakishikiliwa hata hivyo, alipofika alikuta mbuzi saba kati ya 33, huku polisi
wa kituo hicho wakimshikilia mtu mmoja kwa madai ya kuhusika na wizi huo.
Hata hivyo, Kikwaba alishangazwa na vitisho alivyopewa na
mkuu huyo wa kituo miongoni mwa hivyo ni pale alipolazimishwa kumhudumia
mtuhumiwa wa wizi huo kwa kumpeleka hospitali kutibiwa majeraha aliyopata baada
ya kushambuliwa na wananchi.
“Nilijaribu kukataa lakini nilipewa vitisho kwamba endapo
ningetaa kumhudumia mahabusu huyo kwa kumpeleka hospitali na kupatia huduma ya
chakula basi wangenishughulikia kutokana na vitisho hivyo ilinibidi
nikubali,”alisema Kikwaba.
Alisema pamoja na yote hayo, mkuu huyo wa kituo aliamua
kumuachia mtuhumiwa huyo, kitendo ambacho kimesababisha kukwama kwa kesi aliyofungua
Mahakamani Januari mwaka huu.
“Utaona ubabaishaji wa mkuu huyu wa kituo, kwani January 9
mwaka huu alimleta mahakamani mtu mwingine ambaye hahusiki jambo ambalo hakimu
aliwataka polisi warudi wakamlete muhusika kwa hiyo hadi leo hawajampeleka
hivyo kuendelea kuchelewesha kupatikana haki yangu,”alilalamika Kikwaba.
Alisema, licha ya malalmiko yake hayo kuyafikisha kwa
diwani, mbunge na Mkuu wa Wilaya, ambao nao walitoa magizo ya kupatiwa haki
yangu lakini cha kushangaza hadi leo polisi hao hawaja chukuwa hatua zozote za
kunisaidia zaidi ya vitisho.
Kikwaba, alisema mara ya mwisho, alipofika kituoni hapo
alielezwa kuwa asikanyage tena kituoni hapo kwani mhusika hivi sasa amehamishwa
kikazi kwenda kituo kingine kwa hiyo mkuu wa kituo aliyopo ni mpya, halifamu
shauli hilo.
“Hata Mkuu wa Kituo wilayani Biharamulo anazo taarifa
zangu, naiomba serikali inisaidie kuwapata mbuzi wangu kwani naamini kabisa
mkuu huyu wa kituo (Neligwa), anafahamu mbuzi wangu waliko kama hahusiki
asingeweza kumuachia mwizi ikiwa ni ishara ya kutaka kupoteza ushahidi,”alisema
Kikwaba.
Kikwaba, alisema kwamba kuna haja ya kusaidiwa kwa vile
malalamiko yake yamechukuwa zaidi ya miezi mitatu sasa bila ya kuonesha ishara
yeyote ya kupatiwa haki yake kutoka kituo hicho cha polisi.
Alipotafutwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Augstino
Ollomi, ili kutoa ufafanuzi, alisema kuwa anaomba kukutana na mlalamikaji huyo
kwa ajili ya kusikiliza madai yake kisha aweze kuyatafutia ufumbuzi.
“Naomba nisaidie namba ya huyo mlalamikaji ili nipate kumpigia,
ni msikilize ili kuona kama ni kweli hayo anayoyasema tuweze kumchukulia hatua
mhusika,”alisema Kamanda Ollomi.
Hata hivyo, Kamanda Ollomi, alisema endapo Kikwaba,
atabainika kuwa ametoa taarifa za uongo basi atambue kuwa polisi watamchukulia
hatua za kisheria.
No comments:
Post a Comment