CHAMA Cha Kijamii (CCK),
kimeshangazwa na tamko la Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha
Salim Jecha, kwa kukitaja chama hicho kwenye orodha ya vyama vitakavyoshiriki
uchaguzi wa marudio Machi 20, mwaka huu.
Kauli hiyo ya CCK imekuja
baada ya ZEC juzi kuvitaja vyama vitakavyoshiriki katika uchaguzi huo wa
marudio unaotarajiwa kufanyika Machi 20, mwaka huu.
Akizungumza na wandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana Katibu Mkuu wa CCK, Renatus Muhabhi, aliitaka
ZEC kuheshimu uamuzi wa chama chake ambacho kinaongozwa na katiba moja.
Muhabhi, alishangazwa na
uamuzi huo kwa kuwa chama hicho tayari kimekwisha kutangaza msimamo wake ambao
ni kutoshiriki uchaguzi huo wa marudio.
Alisema hawakubaliani na
tamko hilo la Jecha, kwa kuwa vikwazo vilivyokwamisha uchaguzi wa awali bado
vipo, hivyo hakuna haja kwa chama chao kushiriki uchaguzi huo ambao matokeo
yake yanafahamika.
“Tamko hilo la Jecha
amelitamka yeye, sisi tutakutana na tutalitolea tamko, kama unavyojua kuhusu
uchaguzi huo tumekubaliana na baadhi ya makatibu wakuu wa vyama kukutana kisha
tutatoa tamko la pamoja,” alisema.
Muhabhi alisema Jecha hana
haki ya kulazimisha fikra zao na kuwazungumzia watu, kwa kuwa vyama ni taasisi,
vina kanuni na taratibu zake za kujiendesha.
“Anatangaza kuwa tunashiriki
wakati anajua fika kwamba kuna hoja zetu tulizowaandikia ambazo hadi sasa
hajazijibu, kwa hiyo tutakutana haraka kutoa tamko letu kuhusu tamko lake,” alisema.
Aliwataka ZEC kutambua kuwa CCK ni chama kimoja,
uamuzi ukipitishwa ni wa nchi nzima na hakuna wa kuugeuza.
No comments:
Post a Comment