KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Tuesday, 29 March 2016

HAKIMU LAWAMANI MALI ZA URITHI

WASIMAMIZI wa mirathi wa familia ya marehemu Salum Malingumu, wamemlalamikia Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Masanze, wilayani Kilosa, Mororgoro, Shadrack Mlewa, kwa kushirikiana na mke wa marehemu, Mariam Malingumu, kujinyakulia magari mawili kati ya matatu ya marehemu huyo kinyume cha sheria za mirathi.
Hata hivyo, Mlewa, amesema malalamiko hayo hayana ukweli na iwapo wasimamizi wa mirathi wameona kuna tatizo walipaswa kumlalamikia kwa hakimu wake wa wilaya ili ikiwezekana amchukulie hatua badala ya kukimbilia kwenye vyombo vya habari.
Mmoja wa wanafamilia hao, alisema malalamiko yanatokana na hakimu huyo kuonekana akiwa na magari hayo mawili aina ya Hiace, akiyamiliki kama mali yake.
Akizungumza na Tanzania Daima hivi karibuni jijini Dar es Salaam, mwanafamilia huyo aliiomba serikali kuingilia kati mgogoro huo wa mali za mirathi ambao umeazishwa na Mariam.
“Mlewa aliivuruga kesi hii na kufanya kila mara kubadilishiwa mahakimu, hata hivyo tulishashinda baada ya kusikilizwa na hakimu mwingine na hatimaye yule mama akaondolewa kwenye nafasi ya usimamizi wa mirathi baada ya kuhamisha mali za marehemu bila ya ridhaa ya warithi wengine,” alisema.
Mwanafamilia huyo alisema mashahidi hao pia walikiri mahakamani kwamba mali nyingine tayari zimegawiwa kwa warithi wote, huku magari matatu ambapo mawili ni yale yanayodaiwa kunyakuliwa na hakimu huyo bado hayajagawanywa.
Mlewa akizungumzia tuhuma hizo, alisema kuwa ameshangazwa na malalamiko hayo, ambayo amedai kuwa hayana ukweli wowote kwani hana magari ya familia hiyo.
“Siwezi kuzungumzia kwa undani suala hilo, kama ni kulizungumzia ni lazima nipewe ruhusa na kiongozi wangu ambaye ni hakimu wa wilaya,” alisema Mlewa.
Mlewa alisema kama kuna kitu hakikuwaridhisha walipaswa kufikisha malalamiko hayo kwa mkuu wake wa kazi au kwenye bodi ya wilaya ili kusikilizwa, ili kubaini tatizo liko upande upi kati yao,” alisema Mlewa.
Kwa upande wake, Mariam, alikana magari hayo kuchukuliwa na hakimu, bali wanayo wenyewe.
Alisema baada ya kusikia magari hayo yanapaswa kuuzwa ili fedha zigawanywe, kitendo hicho kikawaudhi na kuamua kuyanyofoa vifaa vyote na kuyaacha magari hayo kubaki kama chuma chakavu, isitoshe wao ndio wanajua yaliko.
“Tangu amefariki dunia mume wangu nimekuwa nikiishi kwa shida, kwani sina msaada wowote kutoka kwao wakati wanajua nimeachiwa watoto wawili ambao wanasoma na kuhitaji msaada,” alisema Mariam.
Pia alipinga kuhusika na nyumba iliyoko Morogoro na kusema anachofahamu nyumba hiyo wamekwisha kuiuza na sasa wanataka kumtoa kwenye nyumba anayoishi na wadogo zake ili nayo waiuze.

CHANZO TANZANIA DAIMA

No comments:

Post a Comment