WAKAZI wa Mtaa wa Zingiziwa, Wilaya ya
Ilala, Dar es Salaam, wamemeomba Mkuu wa
Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kufikisha kilio chao kwa Rais John Magufuli
ili aangalie uwezekano wa kulifutia hatimiliki shamba lenye kubwa wa ekari 10
ambalo Manispaa ya Ilala wameshindwa kuliendeleza.
Wakazi hao walidai shamba hilo, ambalo
lilitengwa na manispaa hiyo kwa ajili ya hifadhi ya wanyama (Zoo),
limetelekezwa kwa muda mrefu na hivyo kusababisha ongezeko la nyoka aina chatu
ambao wamekuwa tishio kwa maisha yao.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na
waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana,
wananchi hao walisema Manispaa ya Ilala ilitenga shamba hilo kama
hifadhi, tangu mwaka 2005 hata hivyo, tangu kipindi hicho halijaendelezwa.
“Kutoendelezwa kwa muda mrefu kumefanya
matokeo yake kiwe kichaka cha kujifichia majambazi huku baadhi ya watu wakishambuliwa na nyoka wakali,” alisema
mmoja wa wakazi hao.
Mohamed Kaunda, alisema ni wakati mwafaka
kwa Rais Magufuli kulifutia hatimiliki
shamba hilo, ili lirudishwe serikalini kwa ajili ya matumizi mengine ikiwemo kuanzishwa
miradi ya maendeleo kama zahanati.
Mwenyekiti wa Mtaa huo, Ally Mkwanda,
alisema katika mtaa wake wapo watu wanaomiliki ekari kuanzia tano hadi 10 za mashamba lakini wanashindwa
kuziendeleza.
“Kikwazo kikubwa katika mtaa wangu wamiliki wa
maeneo hawayafanyii usafi, yamekuwa
kichaka cha wezi na kuwa na majoka makubwa ambayo ni hatari,” alisema Mkwanda.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Manispaa
ya Ilala, Isaya Mgurumi alikiri kuwepo kwa mpango wa kutengenezwa hifadhi ya
wanyama katika eneo hilo na kwamba
mpango huo utaanza hivi karibuni.
Alisema katika mwaka huu wa fedha,
bajeti inaonyesha Sh.Milioni 100 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi huo, hivyo
kuwaomba wakazi wa eneo hilo kuondoa hofu kwani ujenzi unatarajiwa kuanza muda si
mrefu toka sasa.

No comments:
Post a Comment