WAZIRI wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk.
Harrison
Mwakyembe, amesema wabaya wake wameanza kumchafu kwa kutoa porojo za
kisiasa wakimhusisha na kashfa ya mabehewa feki ya TRL.
Katika taarifa yake iliyosanbazwa kwa vyombo
vya habari jijini Dar es Salaam leo, Dk Mwakyembe, alisema kuna watu ambao
wamekuwa wakipeleka taarifa za uzushi kwenye vyombo vya habari zenye lengo la
kumchafua hususan katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa
kufanyika Octoba mwaka huu.
Alisema watu hao wamekuwa wakimhusisha kwenye
mchakato wa zabuni ya TRL ambao kwa kawaida waziri hana mamlaka nao kikanuni na
kisheria.
Dk. Mwakyembe, alisema wakati akiwa waziri mwenye
dhamana wa uchukuzi, baada ya kupokea
malalamiko kuhusu mabehewa yaliyonunuliwa kutokuwa na viwango
vinavyokubalika, alichukua hatua za awali za kuunda tume.
Alisema tume ilianza kazi ya kuchunguza suala
hilo mara moja, ili kujiridhisha na kutafuta ukweli wa jambo hilo.
“Baada ya kupokea taarifa ya awali ya uchunguzi
uliyofanywa na tume hiyo, nilichukua uamuzi wa kuiagiza Bodi ya Wakurugenzi ya
TRL kuivunja Bodi ya Zabuni.
Dk. Mwakyembe alisema baada ya bodi hiyo ya
zabuni kuvunjwa, aliagiza Bodi hiyo ya wakurugenzi ya TRL iwasimamishe kazi maofisa waandamizi wote wa TRL waliyohusika
katika mchakato wa manunuzi wa mabehewa hayo ili kupisha uchunguzi uliyokuwa
ukiendelea kufanywa na tume.
“Niliiagiza wizara na Bodi ya wakurugenzi ya
TRL kuiomba Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), ifanye
uchunguzi wa kina wa mkasa mzima, kazi ambayo nafahamu inaendelea kufanyika
hadi sasa.
“Kwa msingi huo habari zinazosambazwa kwenye
vyombo vya habari na kunihusisha na kashfa ya sakata hilo imenishtua na
kunishangaza kwa kuwa kama ningekuwa na husika kwa namna moja au nyingine
nisingeweza kuchukua hatua nilizozieleza,”alisema Dk. Mwakyembe.
Kuhusu
mabadiliko ya Baraza la Mawaziri
Dk Mwakyembe, alisema kuhusu mabadiliko ya
Baraza la Mawaziri yaliyofanywa na Rais Jakaya Kikwete, ambayo yamefanya
ahamishiwe katika Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwamba ni kwa
sababu ya kuepushwa na kadhia ya kashfa hiyo ya ununuzi wa mabehewa feki.
“Hilo ni jambo la kushangaza na uelewa mdogo wa
baadhi ya waliyotoa taarifa hizo, kwa kutoelewa namna Serikali inavyofanya
kazi,”alisema Dk. Mwakyembe.
Dk. Mwakyembe, alisema uamuzi wa kuhamishwa
wizara, ulifanywa na Rais kwa sababu tofauti kabisa na hizo za kusadikika zilizoandikwa kwenye
baadhi ya vyombo vya habari .
Alisema kama Rais aliona ana dosari, hangekuwa
na sababu kabisa ya kumteua ili amsaidie kuendesha Jumuiya ya Afrika Mashariki
(EAC), katika kipindi hiki ambacho nchi imepata fursa ya kuwa mwenyekiti wa
Jumuiya hiyo.

No comments:
Post a Comment