KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Tuesday, 10 March 2015

WAKAZI WA MADALE WATAKA KAMATI YA MAJI IWAJIBISHWE KWA UBADHIRIFU

Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni Mussa Natty
BAADHI ya Wananchi wa Mtaa wa Madale Kata ya Wazo wilayani Kinondoni mkoani Dar es Salaam wametaka  uchunguzi ufanyike haraka na kuwafikisha  mahakamani watu wote waliohujumu mradi wa maji wa Madale.

Pia wametaka mradi huo ulirudishwe katika Kampuni ya Majisafi na Majitaka (Dawasco).

Wakizungumza katika mkutano wa hadhara Dar es Salaam jana, wananchi hao walisema inasikitisha kuona kuwa Dawasco inawauzia uniti moja ya maji kwa sh.1200 lakini wao wanauza uniti moja ya maji kwa sh.5000 

Walisema maji yaho yamekuwa yakiwanufaisha wachache huku mamilioni ya shilingi yakiliwa na watu wachache ambapo Kamati ya awali iliyokuwa ikisimamia maji imefanya ubadhirifu mkubwa huku.


Walisema licha ya kamati hiyo kufanya ubadhirifu bado wapo baadhi ya Viongozi ambao wamekuwa wakiwakingia vifua awali, lakini sasa wamechoka na wameamua kuteua Kamati mpya. 


Wananchi hao walisema wakati mradi huo unaanzishwa katika eneo hilo, walishiriki kuchimba msingi na hadi ukamilike ulihitaji sh. milioni 500 lakini Mwenyekiti wao kwa kushirikiana na viongozi wengine waliendesha harambee na kufanikiwa kupata fedha kwa asilimia 95.

Walisema ni lazima ukaguzi ufanyike juu ya Kamati iliyopewa jukumu la kusimia mradi huo na kisha wakabidhi nyaraka zote na wakibainika kuhusika na hujuma dhidi ya mradi huo basi ni lazima wafikishwe mahakaman

Walisema licha ya kujitahidi na kufanikisha suala hilo lakini bado wanapata maji mara moja kwa wiki  au mbili wakati wenzao wengine wanapata maji kila siku hivyo kuanzia siku hiyo hawaitaki tena Kamati hiyo na sasa wanakamati mpya inayoongozwa na Amina Kawawa.


"Cha kushangaza zaidi wanaonufaika na maji ni wageni ambao hata shilingi hawajachangia lakini waliochimba mitaro hawana hata tone la maji na kwa haya maji yapo kilomita 50 tu kutoka yalipo lakini bomba hilo hilo linapeleka maji.


Kigamboni  na wao wananunua kwa bei rahisi kabisa iweje sisi hapa"alisema Mkazi mmoja wa eneo hilo aliyejitambulisha kwa jina Rashid Mkali.

Mkazi mmoja wa eneo hilo aliyejitambulisha kwa jina moja la Mlay alisema yeye alitoa zaidi ya sh. 400,000 kwa Kamati ya Maji ya Madale lakini tangu amelipia hajawahi kupata maji hayo hadi leo hiizaidi ya kutoka mara mbili jambo ambalo linamshangaza.

"Hawana hata huruma wamekuja nimewapa zaidi ya sh.400000 ili waniunganishie maji lakini cha ajabu maji hayatoki na kila mwisho wa mwezi wanakuja kusoma bili yao sasa nawauliza tangu mnifungie bomba hapa zaidi ya miezi mitano iliyopita sijapata maji leo mnakuja kusoma nini hapa"alisema Mlay.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa huo Grasian Mbelwa alisema wao walifanya kazi kubwa kwa kushirikiana na Waziri Mkuu Mstaafu Rashid Kawawa kuhakikisha kuwa watu wa Madale wanapata maji lakini mradi huo umehujumiwa kwa kiasi kikubwa.

"CCM haiwapendi watu wanouumiza wananchi bali inataka watu wanaoleta maendeleo katika jamii hivyo basi kwa kuwa wananchi wenyewe ndio mmewapendekeza watu wanaounda Kamati Mpya ya Maji basi mimi kama Serikali ya Mtaa nitatoa ushirikiano wa kutosha kuhakikisha kuwa Kamati hii inafanya kazi yake alisema Mbelwa.

Mkutano huo ulihudhuriwa na Viongozi mbambali wa Vyama vya Siasa kikiwemo Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na Chama cha Wananchi (CUF) huku wananchi hao wakimpongeza Mwenyekiti huyo kwa kuitisha mikutano ya hadhara na wananchi kupata fusra ya kuzungumzia fursa za maendeleo katika mtaa wao.


No comments:

Post a Comment