KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Monday, 23 March 2015

HOSPITALI ZAKABILIWA, UHABA WA DAMU SALAMA

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Michael Mhando
BAADHI ya wananchi wameitaka serikali kuwachukulia hatua za kisheria watendaji wa hospitali wanaojihusisha na vitendo vya kuwauzia damu wagonja.

Walisema hivyo jiji Dar es Salaa jana wakati wakitoa maoniyao kuhusu uhaba wa damu salama uliojitokeza katika hospitali nchini.

Walisema hali hiyo imekuwa kikwazo kikubwa kinachowafanya baadhi yao waone kuwa hakuna haja ya kuchangia damu.

Wanachi hao walisema wamekuwa wakijitolea katika kuchangia damu kwa ajili ya wagonjwa, lakini wagonjwa wanapopelekwa katika baadhi ya hospitali wahudumu huwauzia damu hiyo, kitendo ambacho kinawashangaza.

Walisema wakati umefika sasa kwa serikali ikishirikiana na wakuu wa hospitali hizo kuweka mkakati wa kuzuia vitendo hivyo ili kurudisha imani kwa wachangiaji damu.

Wakati hali ikiwa hivyo,  Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na Ustawi wa Jamii kupitia Mpango wa Taifa wa Damu Salama, utaendesha shughuli ya upimaji wa afya na kukusanya damu salama katika mikoa sita.

Kwa mujibu wa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Michael Mhando, hatua hiyo inalenga kupunguza uhaba wa damu salama kwa matumizi ya wagonjwa nchini na wakati huo huo kuwawezesha wananchi kujua afya zao na hivyo kuchukua hatua stahiki mapema.

Mhando alisema hatua hiyo imefikiwa baada ya kuwepo kwa uhaba wa damu salama katika vituo mbalimbali vya matibabu nchini, ambavyo vingi vinahudumia wanachama wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya. “Tumetaarifiwa na wenzetu wa Damu Salama kuwa mahitaji ya damu salama nchini ni chupa 400,000 hadi 450,000 kwa mwaka ambayo ni sawa na wastani wa chupa 106,000 za damu kwa robo mwaka,” alisema Mhando na kuongeza:

“Hata hivyo, kutokana na kutofikia kiwango hicho, Mpango wa Damu Salama Tanzania ulijiwekea lengo la kukusanya chupa 150,000 kwa kipindi cha mwaka jana ambayo ni sawa na lengo la kukusanya chupa 37,500 kwa mwaka.

 “Hili ni suala la dharura na linahitaji hatua za haraka na ushirikiano miongoni mwa wadau wa sekta ya afya na wananchi kwa ujumla,” aliongeza mkurugenzi huyo wa NHIF. Alisema takwimu zinaonesha kuwa kiasi cha chupa 19,000 za damu salama zilikusanywa katika kipindi cha robo mwaka cha Oktoba - Desemba 2014, wakati ambapo chupa 150,000 zimekusanywa kwa kipindi cha kuanzia Januari 2015 hadi sasa.

“Hii inaonesha wazi kuwa upo uhaba mkubwa wa damu kulinganisha na uhitaji uliopo hasa katika vituo vikubwa mfano Muhimbili ambapo zinahitajika chupa 50 hadi 60 za damu kwa siku,” aliongeza Mhando.

Alisema kutokana na umuhimu wa suala hilo, NHIF umeona ni vyema kuunga mkono juhudi za Serikali katika kipindi cha uhaba mkubwa wa damu salama kwa kushirikiana na Taasisi ya Mpango wa Damu Salama na wadau wengine kwa kufanya zoezi la ukusanyaji wa damu kutoka kwa uchangiaji wa hiari wa wananchi.
Alisema shughuli hiyo itaanza Machi 23, mwaka huu kwa muda wa siku tano katika mikoa ya Dar es Salaam ambayo itakuwa katika vituo vya stendi ya Gongo la Mboto, Mbagala, Banana, Buguruni, Karume Sokoni na Mlimani City.

Mikoa mingine na vituo vyao katika mabano ni Mwanza (stendi ya Igoma, Pasiansi, Nyegezi, Buswelu Center, Buhongwa Center), Mbeya (viwanja vya shule ya msingi ya Mwegeishi na Gombe, Mbata na Rundazove, stendi ya Mbalizi na Uyole), Kilimanjaro, Moshi (stendi Mwika, Soko la Chekereni (Kahe), Kwa Sadala (Hai), Soko la Lawate (Siha) na Soko la Kwa Mangula (Rombo).

Mingine ni Tabora (viwanja vya Ndala TTC, Urambo Center, Urambo Center, Kaliua Center, Usoke Center na Town Center na Mtwara (Hiyari Center, Nanyamba Center, Naliendele Center na Umoja na Mikindani Center).

Kwa mujibu wa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, wanatarajia kuwa wananchi 6,000 watajitokeza kuchangia damu na wao wenyewe katika Mfuko huo watakuwa miongoni mwa washiriki wa kwanza kuchangia.


Kwa upande wake, Meneja Masoko na Mawasiliano wa Mpango wa Taifa wa Damu Salama, Rajab Mwenda alisema uchangiaji wa damu hauna madhara yoyote na kuwataka Watanzania kujenga utamaduni wa kuchangia damu ili kuokoa maisha ya wenzao wenye uhitaji wa damu ili kuokoa maisha yao.

No comments:

Post a Comment