KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Wednesday, 8 April 2015

CHADEMA YAINGILIA KATI MGOGORO WA MAGEREJI TEGETA



KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibrod Slaa, amesema chama hicho kipo hatua za mwisho kufungua kesi ya madai dhidi ya mtu anayedaiwa kumiliki eneo walipo Umoja wa Mafundi Gereji, Tegeta, jijini Dar es Salaam.

Eneo hilo maarufu kama Tegeta Magereji  limeingia katika mgogoro kati ya mafundi hao na mtu anayedaiwa kuwa mwekezaji baada ya kudai kuwa eneo hilo ni lake.

Hata hivyo, mafundi hao wanapinga kuondoka katika eneo hilo kwa madai wanatambulika kisheria.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, Dk. Slaa alisema kwa sasa wanaendelea kulifuatilia suala hilo na kwamba wahusika wakuu ni wanasheria wa chama hicho.

“Ni kweli tunaendelea kulifuatilia kwa kina suala hilo na kwa sasa tumewaachia wanasheria wetu hasa Mallya (John Mallya) ambaye ndiye anashughulikia suala hilo kisheria,” alisema.

Kwa upande wake, Mwanasheria wa Chadema, John Mallya, alisema wamekamilisha kila kitu na wanachosubiri ni baadhi ya masuala kukamilika ili wafungue kesi ya madai Mahakama Kuu.

“Tutafungua kesi ya madai Mahakama Kuu kwani wateja wetu si walioshitakiwa mahakamani na sisi tumepitia kila kitu na tumejiridhisha kuwa wao hawakupaswa kufunguliwa kesi, sasa sisi tutafungua kesi ya madai dhidi ya wahusika,” alisema Mallya.

Mafundi hao zaidi ya 4,000 wanatakiwa kuhama eneo hilo kutokana na mtu anayedaiwa kumilikia eneo hilo kufungua kesi mahakamani ambapo alishinda kesi hiyo.

No comments:

Post a Comment