KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Wednesday, 8 April 2015

NGURUMO AAGA WASOMAJI WAKE RASMI




Mhariri Mtendaji wa gazeti hili, Neville Meena (kushoto), akisalimiana na Mhariri Mtendaji aliyemaliza muda wake, Ansbert Ngurumo, baada ya makabidhiano ya ofisi zilizopo makutano ya mitaa ya Mkwepu na Makunganya jijini Dar es Salaam jana. (Picha na Loveness Bernard).


MHARIRI Mtendaji Mstaafu wa Kampuni ya Free Media, inayochapisha magazeti ya Tanzania Daima na Sayari, Ansbert Ngurumo, leo aliwaaga rasmi wafanyakazi wa kampuni hiyo, huku akiwaasa kuendelea kutetea haki za wanyonge bila kujali itikadi za kidini au za kisiasa.

Ngurumo, ambaye ni mmoja wa wahariri waanzilishi wa gazeti hili, amekaa katika kampuni hii kwa miaka 10 na miezi miwili; aliwaasa waandishi wasiyumbe na kuacha dhima ya kuwasemea wananchi wasio na sauti, na kutetea wanaodhulumiwa haki zao, kazi ambayo imelitambulisha Tanzania Daima katika jamii.

Ngurumo, ambaye ni mmiliki wa Kampuni ya Vox Media na mwandishi wa safu ya Maswali Magumu katika Tanzania Daima Jumapili, aliwataka waandishi kuandika habari kwa weledi na ujasiri, bila kuonea au kuogopa mtu yeyote, kwani kazi wanayofanya ina mkono wa Mungu.

Alisema gazeti la Tanzania Daima linaaminika kwa kusimamia ukweli na kutetea wanyonge ambao hawana pengine pa kukimbilia.
“Naamini gazeti hili litaendelea kuwepo na kutetea wanyonge wasiokuwa na fedha wala madaraka bila ya kujali itikadi; lakini pia litetee wenye uwezo na madaraka wanaoonewa na mifumo,” alisema.
Akizungumza katika ofisi za gazeti hili, Ngurumo alisema awali alipanga kuwaaga wafanyakazi hao Januari 7, mwaka huu, lakini alichelewa kutokana na mazingira magumu aliyokuwamo kifamilia na kiafya, hasa baada ya kufiwa na binti yake mwishoni mwa mwaka jana.

Ngurumo, alikuwa anasumbuliwa na maumivu ya mgongo kiasi kwamba asingeweza kusafiri kwa muda mrefu kutoka Kamachumu hadi Dar es Salaam, hadi alipopata nafuu.

“Siondoki ghafla, lazima na hili lieleweke. Nimeondoka baada ya mipango ya muda mrefu, na kwa kuwa huu ni mwaka wa uchaguzi, ilibidi nichague moja kati ya mawili; nikaamua niache ofisi ili nikajiandae kwa uchaguzi,” alisema Ngurumo.

Akizungumzia maisha yake nje ya chumba cha habari, Ngurumo alisema kwa sasa anafanya kazi ya ushauri wa kitaalamu katika habari na mawasiliano, biashara na intelijensia ya kisiasa.

Kuhusu sisasa

Ngurumo alisema alianza kuandaa chama kwa uchaguzi tangu Juni mwaka 2011 katika jimbo la Muleba Kaskazini, akishirikiana na viongozi na wanachama katika kuinuia chama kilichokuwa kimedorora.

“Nilikuta chama kimedorora, hakifanyi vikao vya ndani; hakifanyi mikutano ya hadhara katika maeneo mengi, hakina msingi hata mmoja, hakina uongozi uliochaguliwa... sasa hivi kina misingi zaidi ya 200, kina uongozi uliochaguliwa kikatiba jimbo zima, mikutano mikubwa ya hadhara inafanyika tangu mwaka 2012.

“Na katika matokeo ya uchaguzi, tumegawana jimbo na CCM. Miongoni mwa vijiji 64, tumechukua 27, na miongoni mwa vitongoji 285, tumechukua 147. Kwa hiyo, nakwenda kushirikiana na wenzangu kuimarisha msingi tuliokwisha kuujenga ili tufanye vizuri zaidi katika Uchaguzi Mkuu,” alisema.
Aidha, alisema kwa vile ameamua kuingia kwenye siasa, ameamua kwenda kujikita jimboni ili aweze kushirikiana na wananchi kuimarisha shughuli zake za kisiasa.

Ingawa hajatangaza rasmi, Ngurumo anatarajiwa kuwania ubunge katika Jimbo la Muleba Kaskazini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), na anasubiri mchakato rasmi ili atimize azima yake hiyo.

Alisema katika Jimbo la Muleba Kaskazini mchuano ni kati ya CCM na Chadema, kwani vyama vingine havina mizizi.
Alimshukuru Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, kwa ushauri na malezi mazuri aliyompa kibiashara na kisiasa, kwa zaidi ya miaka 10 mfululizo, na kwamba atatumia stadi hizo kufanya siasa za kizalendo, zenye msimamo na kwa uaminifu mkubwa.
Pamoja na siasa, Ngurumo anajiandaa kuchapisha kitabu cha Maswali Magumu, ili kusaidia wananchi kutathmini utendaji wa Serikali ya Awamu ya Nne, chini ya Rais Jakaya Kikwete, kama sehemu ya elimu ya uraia kwa Watanzania. CHANZO TANZANIA DAIMA

No comments:

Post a Comment