KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Wednesday, 29 April 2015

DK. MAGUFULI: BARABARA ZA MRADI WA BRT ZILIZOKAMILIKA ZIFUNGULIWE



Mbunge wa Ilala, Mussa Azan Zungu kushoto, katikati Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli na Mkuu wa Mkoa Dar es Salaam, Meck Sadik kwa pamoja wakiweka jiwe la upanuzi wa Barabara ya Uhuru hadi Buguruni Malapa jijni, leo.
WAZIRI wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, amemuagiza Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara nchini (Tanroads), Injinia Peter Mfugale, kuzikabidhi barabara zilizokamilika za mradi wa mabasi yaendayo haraka (BRT) ili ziweze kufunguliwa na kutumika.
Dk. Magufuli alisema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati wa sherehe za kuweka jiwe la msingi kwa ajili ya upanuzi wa Barabara ya Uhuru pamoja na kufanya ukaguzi wa ujenzi wa miundombinu ya mabasi hayo katika barabara ya Morocco – Magomeni - Fire hadi Kariakoo.

Dk. Magufuli alisema wakazi wa jiji hilo wana hamu ya kuona barabara hizo zilizokamilika zinafunguliwa na kutumika ili kupunguza msongamano wa magari yaliyomo katika jiji hilo.

“Sisi kazi yetu ni kujenga lakini wenye majukumu ya kuzifungua ni Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), sasa namuagiza mtendaji mkuu wa Tanroads kukabidhi barabara zote zilizokamilika ili waweze kuzifungua kwa kuzingatia masharti yake ya kuingiza mabasi makubwa,” alisema.

Dk. Magufuli aliitaka Kampuni ya ujenzi wa mradi huo (Strabag), kuanzia sasa ifanye kazi usiku na mchana ili kukamilisha sehemu ya ujenzi huo kwa ajili ya barabara hiyo kufunguliwa na Rais Jakaya Kikwete kabla hajamaliza muda wake mwishoni mwa mwaka huu.

Alisema kwa kuwa Rais Kikwete aliahidi kuwaachia mradi huo ukiwa umekamilika hivyo halitakuwa jambo jema kama ataondoka kabla haujakamilika.

Akizungumzia upanuzi wa Barabara ya Uhuru hadi Buguruni Malapa, Dk. Magufuli alisema barabara hiyo ina urefu wa kilomita tatu ambapo itakuwa ya njia nne.

“Hii ni barabara yenye historia ndefu na ambayo imekuwa na matumizi makubwa ikiwemo kutumiwa na viongozi mbalimbali wa ndani na nje wanapofanya ziara nchini,” alisema.

Alisema ujenzi wa barabara hiyo kuwa ya njia nne utasaidia kupunguza adha ya foleni iliyopo sasa.

Mkuu wa Mkoa, Said Meck Sadik, alikemea vitendo vya uchafu unaofanywa na wakazi wa jiji hilo, ambapo baadhi yao wamevigeuza vituo vya mabasi vya mradi huo kuwa ‘guest’.

 Aliwataka wananchi kuwa wazalendo kwa kuilinda miundombinu hiyo, kwani ujenzi wake umetokana na kodi zao.


No comments:

Post a Comment