KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Wednesday, 29 April 2015

WAISLAM SASA KUANDAMANA KUTOKANA NA POLISI KUVAMIA MISIKITI



JUMUIYA na Taasisi za Kiislam Tanzania zimesema zitafanya maandamano ya amani ifikapo Mei 15 mwaka huu iwapo serikali itashindwa kutekeleza madai yao.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Jumuiya na Taasisi za Kiislam Tanzania, Musa Kundecha alisema, serikali inapaswa kuwaombe radhi  waislam kutokana na vitendo vya unyanyasaji vinavyofanywa na jeshi la polisi nchini.
Kundecha alisema kuwa jeshi hilo limekuwa likiwahujumu waislam kupitia madrasa ambazo ndiyo kiini cha elimu ya dini ya kiislam na maadili mema kwa jamii.
“Serikali iache mara moja kuvamia na kuziandama madrasa na kuwaweka mahabusu watoto wadogo kwa kisingizio cha vyuo hivyo kutosajiliwa ili hali hakuna sheria wala sera ya elimu inayotaka madrassa zisajiliwe,” alisema
 Sheikh Kundecha alisema kuwa Serikali inapaswa kutoa dhamana kwa masheikh walioko mahabusu kama inavyofanya kwa maaskofu na wachungaji walioshitakiwa mahakamani.
“Jeshi la Polisi liwaachie au kuwapa dhamana mashekh, maustadhi na maimamu waliokamatwa sehemu mbalimbali nchini na ambao wako katika mikono ya Polisi kwa muda mrefu bila kufikishwa mahakamani,” alisemaKundecha alisema baadhi ya viongozi wa serikali ngazi za wilaya, mikoa na taifa wamekuwa wakiungana na jeshi la Polisi katika harakati hizo ambazo zina athari kwa waislamu nchini.
 “Tuhuma wanazotoa Polisi kuhalalisha harakati za uvamizi na kamatakamata ni pamoja na madrassa na masheikh kufundisha dini ya Kiislam kinyume cha sheria, kukusanya watoto na kuwafundisha elimu ya dini kinyume cha sheria na katika mazingira yasiofaa,”alisema.
Alisema kuwa polisi wamekuwa wakidai kuwa madrasa hizo zimekuwa zikifundisha na kufanya mazoezi yanayoendana na ugaidi kinyume na sheria, kuwepo kwa taarifa za watu wenye milipuko miskitini na kutuhumiwa kujihusisha na vitendo vya kigaidi.
 Akitolea mfano huko Kilombero mkoani Morogoro alisema watu wengi waliingia msikitini saa tisa za usiku na muda mfupi baadae polisi wakaja na kuvamia msikiti kwa namna ambayo inatia shaka.
Alihoji kuwa Polisi walifahamu watu hao wametoka wapi au walihusika kwa nia ya kuchafua hadhi ya msikiti na uislamu.
“Watu waliokamatwa sio wenyeji wala wakazi wa eneo linalotumia msikiti huo, hilo halikutajwa na Polisi wala kiongozi yeyote wa serikali,”alisema.
 Alisema Polisi wamekuwa wakikiuka haki nyingi za binadamu, haki za kikatiba, na kisheria huku wakichangia na kusababisha waislam kuonekana kuwa sio waaminifu na watu wanaochukia amani hatua inayosababisha wachukiwe na jamii.
 Naye Katibu wa Jumuiya hiyo Rajab Katimba alisema, anashangazwa na Polisi kuwakamata  masheikh na maustadhi  kwa kisingizio cha vituo kuwa na hali duni huku wakishindwa kuwakamata walimu wanaofundisha shule zenye ukosefu wa vyoo.

No comments:

Post a Comment