WADAU wa Mamlaka ya
Usimamizi Bandari nchini (TPA), wameshauri taasisi zinazotoa huduma kwa mizigo kupitia
bandari ya Dar es Salaam kutoa huduma hizo katika kituo kimoja, ili kuiongezea ufanisi
bandari hiyo.
Ushauri huo ulitolewa hivi
karibuni jijini Dar es Salaam na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Awadh Massawe,
alisema katika vikao vya wadau wa
mamlaka hiyo.
“Katika mkutano wetu,
wadau wa bandari wamependekeza kuwa taasisi hizo zisogeze huduma zao karibu na
bandari kuongeza ufanisi wa kazi,” alisema Massawe ambaye pia ni Mwenyekiti wa
Kamati ya vikao vya wadau wa mamlaka hiyo.
Mapendekezo hayo
yamekuja kutokana na mikutano ya kawaida ya kamati ya vikao vya wadau wa TPA
ambayo hufanyika kila mwezi katika juhudi za kuimarisha huduma za bandari.
Alizitaja baadhi ya
taasisi hizo kuwa ni Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Shirika la Viwango
Tanzania (TBS), Ofisi ya Mkemia Mkuu na wakala wa Mizani na Vipimo.
Alisema wadau wa
bandari wamebaini kuwa kitendo cha taasisi hizo kuwa mbali na eneo la bandari
imekuwa ni kikwazo kwao na kuchangia kusababisha mizigo kukaa bandari muda
mrefu.
Alisema wadau wa
bandari wangependa kuona shughuli zote zinakuwa katika kituo kimoja, ili kuleta
ufanisi wa kazi na kuiwezesha bandari hiyo kuwa moja ya bandari shindani katika
ukanda huu na barani Afrika kwa jumla.
Pia alisema kwa sasa
TPA inajenga jengo la ghorofa ambapo taasisi au kampuni zinazohusika na masuala
ya huduma za bandari zinaweza kuomba, ili huduma nyingi ziwe katika kituo
kimoja kurahisisha utendaji kazi bandarini.
Kwa upande wake, Rais
wa Chama cha Wakala wa Mizigo Tanzania (Taffa), Stephene Ngatunga, alisema
kumekuwa na ucheleweshaji mkubwa wa kuondoa mizigo bandari kutokana na taasisi
hizo kuwa mbalimbali.
“Kwa utaratibu ulivyo,
Mamlaka ya Mapato (TRA) haiwezi kutoza kodi bila ya taasisi hizi kumaliza kazi
zake...hii inaleta changamoto,” alisema.
Mwisho
No comments:
Post a Comment