CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kinadaiwa kuvunja Sheria na kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa, kwa kujihusisha na vitendo vya rushwa ili kuwashawishi wananchi wa Kijiji cha Mtambani Kata ya Bwiringu, Chalinze mkoani Pwani, kukichagua chama hicho.
Kijiji hicho kinatarajiwa
kufanya uchaguzi mdogo wa serikali za mitaa kesho, baada ya ule uliyofanyika
Desemba 14 na 21 mwaka jana kukumbwa na dosari lukuki zilizosababisha kuahirishwa
kwa uchaguzi huo.
Akizungumza na wandishi
wahabari leo, kwa njia ya simu kutokea katika jimbo hilo la Chalinze jana,
Katibu wa Operesheni, Mikakati, Propagandi na Mafunzo Mkoa wa Pwani wa Chama
cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Juma Mwipopo, alisema wanafuatilia kwa
karibu ukiukwaji huo wa sheria.
Aliitaja sheria hiyo kuwa ni
ile ya uchaguzi na kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa na vitongoji sura
namba 287 kifungu cha 201(A), tangazo la serikali namba 320 la 5/9/2014 pamoja
kifungu cha 18.
Mwipopo, alisema kifungu
hicho cha 18 kinaeleze masharti ya mgombea au chama kutojihusisha na kampeni zinazoashilia
vitendo vya rushwa, kashfa, matusi, ubaguzi wa kijinsia, udini na ukabila.
Alisema pamoja na sheria na
kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa kuwa wazi, Mei 11 mwaka huu CCM
kilizindua kampeni zake, ambapo walitoa fulana, jezi na mipira katika shule na
wananchi ikiwa ni kuwashawishi ili waweze kukichagua chama hicho kwenye
uchaguzi huo.
“Pia waliendelea kuvunja
kanuni hizo kwa kuwaambia wananchi wa kijiji cha mtambani kwamba wakikichagua
Chadema watawafukuza wafugaji wote, niwaombe wafugaji kuzipuuza kauli hizo
kwani Chadema ni chama makini ambacho kazi yake kubwa ni kupigania haki za
wananchi wote bila ya kubagua popote pale nchini,”alisema Mwipopo.
Alisema Chadema siyo chama
cha kibaguzi wala kikabila bali ni chama cha wananchi kutoka maeneo yote ya
Jamhuri ya Muungano, hivyo wanaokifananisha na udini na ukabila ni watu
waliofilisika kisiasa.
Katibu huyo, alisema kuwa
wananchi wa Mtambani hawahitaji fulana, mpira bali wanahitaji barabara, maji na
huduma bora za afya, ambazo CCM, imeshindwa kuwafikishia tangu nchi ilipopata
uhuru mwaka 1964.
No comments:
Post a Comment