KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Friday, 15 May 2015

KATIBU MKUU TAMISEMI, SAGINI ASISITIZA UIMARISHAJI WA ELIMU

DSC_0069
Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) Tanzania, Bi. Zulmira Rodrigues akisalimiana na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na. Serikali ya Mtaa (TAMISEMI), Jumanne Sagini alipomtembelea ofisini kwake mjini Dodoma wakati wa ziara ya kikazi ya siku moja ya kukutana na wadau wa elimu walioshiriki mkutano wa kutathmini sekta ya Eimu nchini kwa mwaka 2014 uliofanyika katika kumbi za mikutano Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).
……………………………………………….
(Habari -Picha zote na Zainul Mzige wa modewjiblog).

KATIBU Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali ya Mtaa (TAMISEMI), Jumanne Sagini  amesema elimu ya sasa inaelekezwa zaidi katika kumwezesha mtu kujitegemea.
Kauli hiyo ameitoa katika mahojiano maalum na mtandao wa habari wa modewjiblog kuhusu maendeleo na changamoto kwenye sekta ya elimu nchini katika wiki ya maadhimisho ya elimu inayofikia tamati leo mjini Dodoma.
Alisema katika mahojiano hayo kwamba mfumo sasa unawaondoa watu kwenye  ajira ya serikali na kutokana na hilo uimarishaji wa elimu ndio kitu cha msingi kabisa.
Alisema katika maadhimisho ya elimu watu wanajifunza usimamizi kama msingi mkubwa wa maendeleo ya elimu nchini.
Alisema kuna mambo mengi ambayo yanastahili kuangaliwa kwa sasa kutokana na vigezo vya ufanisi wa elimu kuonesha changamoto zinazokabili sekta hiyo pamoja na kuimarika kwake.
Alizitaja changamoto hizo kuwa ni pamoja na kupungua kwa uandikishaji wa watoto na mdondoko.
Alisema viongozi, wazazi pamoja na walezi wamesahau wajibu wao na kumwachia mwalimu pekee katika kumlea mwanafunzi kimasomo na hii ndio chanzo kikubwa cha mdondoko na ufaulu mbaya.
Alisema ni vyema watu wakajiuliza hawa wanaondoka wanakwenda wapi na wanafanya nini.
“kuna sheria ambapo viongozi wa kata wanaruhusiwa kuwachukulia hatua na kuwafikisha mahakamani wazazi wanaokwamisha elimu, lakini watu hawachukia sheria hiyo” alisema.
Aidha alisema ubora wa elimu  una vigezo vingi ikiwa ni pamoja na kujituma kwa walimu katika ufundishaji na kuwa na dhamira ya kuwapa watoto vitu vyenye maana.
Alisema kuna mambo mengi yanatakiwa kufanywa kuinua elimu  na usimamizi unapokuwa mkali  na wahusika kuadhibiwa ndio  ufanisi unafanyika na mdondoko kuangaliwa.
Alisema ipo haja kubwa ya kuwekeza kwenye elimu kwa viongozi na wadau kutimiza wajibu wao.
Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi , Makuru Petro akitoa tathmini ya sekta ya elimu kwa wadau wa sekta ya elimu alisema pamoja na ongezeko la ufaulu ndani ya miaka miwili ipo haja ya kutathimini uimara wa mfumo katika kutoa huduma ya elimu.
Alisema pamoja na ufanisi kuwapo kwa idadi kubwa ya watu wanaokacha shule kunaonesha mfumo kuwa na kasoro na lazima uangaliwe.
Aidha alisema sekta ya elimu wamepokea asilimia 97 ya bajeti yake na kwamba asilimia 70 imeenda kwenye halmashauri ambako ni watekelezaji wa miradi ya elimu.
Tathmini hiyo inayowakilisha wizara zote zinazoshughulikia elimu kama TAMISEMI, Elimu na Maendeleo ya jamii na wadau wengine wa elimu ni sehemu ya shughuli inafanywa kila mwaka kwa lengo la kutambua kilichofanyika, changamoto na namna ya kukabiliana na tatizo hilo.
Hata hivyo walisema kwamba ndani ya miaka miwili  kumekuwepo na maendeleo makubwa katika sekta ya elimu hasa ufaulu na ubora  wa elimu.

No comments:

Post a Comment