KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Thursday, 21 May 2015

NBS YATOA UFAFANUZI KUHUSU SHERIA YA TAKWIMU


Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Dk. Albina Chuwa akitoa ufafanuzi kwa waandishi wa habari kuhusu ujio wa sheria mpya ya Takwimu  ya mwaka 2015 iliyopitishwa na Bunge Mwezi Machi mwaka huu leo jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi wa Takwimu za Uchumi wa Ofisi hiyo, Morrice Oyuke.
23
Wadau mbalimbali na waandishi wa habari wakimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Dk. Albina Chuwa wakati akitoa ufafanuzi kuhusu ujio wa sheria mpya ya Takwimu  ya mwaka 2015.
BAADA ya sheria mpya ya takwimu kulalamikiwa na wadau mbalimbali, ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), imetoa ufafanuzi  kuhusu sheria hiyo na kusema haina uhusiano na haitahusika katika uchaguzi mkuu.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya  Takwimu, Dk. Albina Chuwa, alisema: “Hatuna uhusiano na hatushiriki katika uchaguzi mkuu. NBS imetoa takwimu kuwa wapigakura ni milioni 24”.
Kauli hiyo ya Dk. Chuwa imetokana na swali aliloulizwa na waandishi wa habari iwapo sheria hiyo inavibana vyombo vya habari vitakavyoripoti matokeo ya awali ya uchaguzi mkuu.
Mbali na hilo alisema  sheria hiyo haizuii au haihusiki na taasisi au mtu binafsi kufanya utafiti.
Alisema taasisi za utafiti zina sheria na kanuni za kufanya tafiti ikijumlisha kukusanya na kusambaza matokeo ya tafiti zao.
“Kwa mujibu wa sheria hii kila taasisi au chombo chochote cha utafiti hakizuiwi kuendelea na utaratibu wake wa utoaji wa takwimu kulingana na tafiti wanazofanya. Kwa wanafunzi wa vyuo vikuu na vinavyolingana sheria hii haihusiki na “Thesis au dissertation” zao wanasimamiwa na wahadhiri wa vyuo vikuu. Ipo sheria inayowalinda na matokeo hayo na  husambazwa kwa utaratibu uliowekwa na sheria zilizoanzisha vyuo vikuu.
Hata hivyo, alisema jambo la msingi linalopaswa kuzingatiwa ni iwapo taasisi au mtu binfasi anataka takwimu alizokusanya  zitumike katika mipango ya maendeleo ya nchi na kusema kuwa atalazimika  kutoa  takwimu hizo kwa kuzingatiia misingi ya takwimu rasmi.
Dk. Chuwa alisema takwimu rasmi  ambazo huzalishwa na wizara, idara na taasisi za serkali hufuata kanuni  10 na misingi zilizotolewa na Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ya Tamwimu.
Pia alisema vyombo vya habari vitakavyopotosha takwimu rasmi, vitakuwa vimekiuka kifungu cha 37(4) na (5) cha sheria hiyo, hivyo kitashughulikiwa kwa mujibu wa sheria.
Alisema kwa mujibu wa kifungu hicho  kinalenga kuwa takwimu rasmi inayotangazwa ieleze chanzo chake  na kutoa mfano kama chombo cha habari kitatangaza kuwa mfumuko wa bei uliotolewa na NBS ulikuwa asilimia 3.0 baada ya asilimia 4.5, chombo hicho kitastahili kupewa adhabu.
“Napenda kutumia fursa hii, kuwaomba kuendelea kutangaza taarifa hizi kwa usahihi, ili kusaidia wananchi na wadau wote wa ndani na nje ya nchi kutoa mawazo yaliyojengeka kuwa sheria hii ni kandamizi…. Ikumbukwe kuwa serikali ina wajibu wa kuandaa mipango ya maendeleo kwa wananchi wake. Vilevile wananchi tuna wajibu wa kutoa taarifa sahihi kwa serikali.Takwimu bora husaidia serikali yoyote ile duniani kupanga mipango ya  maendeleo ya wananchi  wake. Kutofanya hivyo, serikali haitaweza kupanga mipango yoyote ya maendeleo kwa wananchi wake,” alisema.
 Alisema  makosa ya jinai yaliyoainishwa katika sheria hiyo  ni endapo watumishi wa NBS watatumia taarifa za kitakwimu rasmi kwa manufaa binafsi, kutoa taarifa za kitakwimu rasmi bila kibali,  kudai taarifa tofauti na zilizoruhusiwa kukusanywa na kuomba malipo au ujira.
Alieleza kuwa vitendo vyote hivyo ni makosa ya jinai na mhusika akipatikana na hatia atapewa adhabu isiyopungua mezi sita au kulipa faini isiyopungua sh. milioni 2 au vyote kwa pamoja.
Mkurugenzi mkuu huyo alisema mtu atakayetoa taarifa zilizopatikana isivyo halali,  kwa mujibu wa sheria atapewa adhabu ya kifungo kisichopungua miezi 12 au faini isiyopungua sh. milioni tano au vyote kwa pamoja.

Mbali na hilo, alisema mtu akikataa kutoa ushirikiano katika zoezi la kitakwimu adhabu  ni kifungo kisichopungua miezi sita au faini ya sh. milioni moja.

No comments:

Post a Comment