KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Friday, 5 June 2015

JANUARY MAKAMBA KUTANGAZA NIA YA KUOMBA RIDHAA CHAMA CHAKE, KESHO


MBUNGE wa Bumbuli, January Makamba anatarajia kutangaza nia ya kuomba ridhaa ya kuteuliwa na Chama chake Cha Mapinduzi (CCM), kuwa Mgombea wa nafasi ya urais katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.
Sherehe hiyo ya kutangaza itafanyika kesho kwenye Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Makamba ambaye pia ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, alisema baada ya kutangaza nia anatarajia kuchukua fumu urais mjini Dodoma Jumanne ijayo.
Alisema katika kutangaza ni yake hiyo ataelezea mambo mbalimbali yanayogusa maisha ya wananchi kila siku.
 Makamba, aliitaja falsafa inayomtaka Rais wa Serikali ya Awamu ya Tano awe na “kesho nyingi” zaidi kuliko aliyeona “jana nyingi”. 
 Falisafa hiyo itamfanya awe na uwezo wa kupambana na changamoto za mahitaji ya ulimwengu wa leo wa kidigitali na siyo analogia ambao walioona “jana nyingi” katika hali yoyote hawawezi kuzimudu.
 Hadi sasa waliokwisha jitokeza ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Profesa Mark Mwandosya; Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wassira; Balozi wa Umoja wa Afrika katika Umoja wa Mataifa mjini New York, Marekani, Amina Salum Ali na Mbunge wa Afrika Mashariki kutoka Tanzania, Makongoro Nyerere. Tayari wana CCM waliochukua fomu au waliotangaza nia ya kuingia katika mbio hizo wamekuwa wakiongezeka kila kunapokucha, idadi ambayo inatarajiwa kuwa zaidi ya mara mbili ya wanachama 11 waliofanya hivyo mwaka 2005 au maradufu ya 17 ambao walijitosa mwaka 1995. 
Mbali na Profesa Mwandosya, Wassira, Makongoro na Amina, orodha ya mwaka huu ina majina mengine kama la Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohammed Gharib Bilal; Waziri Mkuu wa sasa, Mizengo Kayanza Pinda;
Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye na Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa kashfa ya Richmond, Edward Lowassa.
 Wengine waliomo katika orodha hiyo ni mawaziri ambao ni pamoja na Benard Membe (Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa), Samwel Sitta (Uchukuzi), Dk. Titus Kamani (Mifugo na Uvuvi) na Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli.
Wamo pia Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba; Mbunge wa Kuteuliwa, Profesa Sospeter Muhongo; Mbunge wa Nzega, Dk. Khamis Kigwangala; Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja; Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina na kadhalika.

No comments:

Post a Comment