KATIBU Mkuu wa Chama Cha Kijamii (CCK), Renatus Muhabhi
amesema chama hicho kinatarajia kwenda Mahakamani juma lijalo kuiwekea zuio
Tume ya Taifa ya Uchaguzi ili kuzuia kutoa fomu kwa mgombea urais wa Chama
Chama Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli.
Alisema kuwa zuio hilo linatokana na NEC kushindwa
kumchukulia hatua za kisheria Dk Magufuli na chama chake kutokana na kuanza
kampeni kabla ya wakati.
Akizungumza na wandishi wa habari jijini jana, Muhabhi,
alisema licha ya kuiandikia NEC, barua bado hawaani kama kuna lolote jipya
linaloweza kufikiwa na tume hiyo.
Alisema, wamechukua uwamuzi huo kutokana na CCM pamoja na
mgombea wake kukiuka sheria na kanuni za uchaguzi huku tume ya uchaguzi ikikaa
kimya.
“CCK inapiga kelele kwa vile tunataka lazima kuwe na uwiano
wa vyama katika shughuli zote zinazohusiana na demokrasia ya vyama vingi
nchini.
“Tunashangazwa na kauli za tume kwamba haihusiki katika
kinachoendelea ndani ya CCM bali itawajibika hadi pale itakapotoa fomu kwa
kauli hizo inaonesha tume inakilinda chama hicho,”alisema Muhabhi.
Muhabhi, alisema kuwa sheria na kanuni za uchaguzi
zinaelekeza kwamba hakuna chama chochote kitakachoanza kamepeni kabla tume
haijatoa fomu, kinyume chake chama kitakachofanya hivyo kinaweza kuzuiwa
kugombea.
Alisema kwa ukinya wa tume katika hili inaonesha kuwa
inaanza kukiuka maadili ya uchaguzi kabla hayajasainiwa na wadau wote wa
uchaguzi.
Hivi karibuni Mwenyekiti wa NEC, Jaji Lubuva alikaririwa na
vyombo vya habari ikisema mambo yanayoendelea ndani ya CCM kuhusiana na
Mikutano, tume haiwezi kuyaingilia.
Alisema tume itaanza kuingilia masuala ya uchaguzi kuona
kama kuna kanuni na sheria za uchaguzi zinakiukwa baada ya uteuzi wa wagombea
wa vyama vyote kufanyika.
No comments:
Post a Comment