KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Wednesday, 20 January 2016

MWALIMU AZABWA MAKOFI KWA KUCHELEWA SEMINA

MWALIMU wa shule ya msingi Ikombolinga Peter Emma, ameeleza masikitiko yake ya kudhalilishwa na Ofisa Elimu wa shule ya msingi, Mohammed Msongo, wilaya Chamwino kwa kuzabwa makofi na mwalimu huyo mbele za walimu wenzake. Mwalimu Emma alisema udhalilishaji aliofanyiwa na Ofisa elimu huyo kwa kupigwa makofi mbele za walimu wenzake unatokana na kuchelewa kufika katika semina ya mafunzo ya KKK licha ya kuwa mwalimu huyo alikuwa anatoka mbali na alikuwa hajalipwa fedha za nauli. Akielezea tukio hilo mwalimu Emma alisema   kwa mujibu wa ratiba ya mafunzo ambayo yalianza 16 Januari mwaka kuu yalitakiwa kuanza saa mbili kamili lakini yeye na wenzake zaidi ya 20 walifika saa 2:40 asubuhi. Akiendelea kuzungumza na waandishi wa habari mwalimu huyo alisema, kwamba yeye na walimu wenzake waliochelewa na walimkuta Ofisa Elimu Msingi, Mohammed Msongo, ambaye aliwazui kuingia darasani kutokana na kuchelewa kwao. Alisema Ofisa huyo aliendelea kuwakaripia na kuwataka waandike majina yao kwa malengo kwamba wasihudhurie mafunzo hayo KKK ambayo yalikuwa yanawahusu walimu wote wa darasa la kwanza na la pili. "Wakati najitetea kuwa tunatoka mbali na usafiri ni wa shida huku hatukuwa na hela Ofisa Elimu alinizaba makofi na kunisukuma ukutani. "Kitendo hicho kweli kimeniumiza na kunidhalilisha sana hata hapa najifunza lakini sina amani natamani kurudi nyumbani. "Tuliandika majina ya waliochelewa sijui tutalipwa au la maana tunatakiwa kulipwa sh. 55000 kwa kila siku nne pamoja na nauli lakini mpaka sasa hatujalipwa mimi sielewi kwakweli nimefadhaika sana.
"Kama uongozi ni wa ubabe hivyo hakika kazi itakuwa ngumu sana kwani hali hii inavunja moyo"alisema Mwalimu Emma. Kwa upande wake Kaimu mkurugenzi wa Chamwino Richard Masimba alipotafutwa ofisini kwake alisema taarifa hizo hawana na watazifuatilia. Masimba alisema ofisi haina taarifa ya mwalimu kupigwa vibao na kusukumwa ukutani na iwapo itathibitika hatua za kisheria na kinidhamu zitafanywa.

Akizungumzia suala hilo, Ofisa Elimu Msingi wilaya ya Chamwino, Mohammed Msongo, alikana na kukataa kata kata kwamba  yeye hajampiga kibao wala kumsukuma ukutani mwalimu huyo. "Jumla ya walimu 348 wanapatiwa mafunzo kazini na mafunzo hayo ni kwa shule za msingi serikali 119.
"Ila ni kweli wapo walimu waliochelewa badala ya kufika saa 2:00 kama tulivyo kubaliana wao wamefika saa 2:40 hivyo walipoteza dakika 40 za kipindi."Kutokana na hali hiyo nililazimika kukaa na walimu wote waliochelewa yakiwa makundi mawili na kuwapa maelekezo ili wasiendelee kuchelewa kwani kwa kufanya hivyo hawawezi kufaidika na hayo masomo"alijieleza Msongo. 
Hata hivyo Msongo alisema siku ya tukio ambalo inadaiwa alimpiga mwalimu huyo alimshika shati kwa nyuma na kumvuta ikiwa ni hatua ya kutaka asijichanganye na kundi lingine lisilo muhusu lakini siyo kumpiga.Kwa upande wake Katibu wa Chama cha Walimu (CWT), wilaya ya ChamwinoJames  Puya alisema analaani vikali kitendo cha Ofisa Elimu msingi kumzaba mwalimu vibao."Kitendo hicho kinawafanya watumishi kukosa morali wa kufanya kazi kwa ufasaha na wakati mwingine kuhamishia hasira kwa watoto."Mimi nimepata taarifa za mwalimu kupigwa na nasema kama kiongozi wa CWT wilaya ya Chamwino kulikotokea hili tatizo naomba tume ya Haki za Binadamu, Mkurugenzi na Utumishi kuingilia kati suala hili."Unyanyasaji huu usipokomeshwa haraka itakuwa mwendelezo wa viongozi wa ngazi ya juu kuwanyanyasa watumishi wa ngazi ya chini jambo ambalo ni hatari"alisema Puya.

No comments:

Post a Comment