SERIKALI imetoa taarifa juu ya kuzama kwa kivuko cha Mto kilombero ambapo watu 30 wameokolewa kati ya 31 waliokuwemo katika kivuko hicho.
Licha ya kutoa taarifa hiyo imeelezwa kwamba jopo la waokoaji limepelekwa kwa lengo la kutafuta ufumbuzi wa haraka wa kuokoa maisha ya watu, mali zao pamoja na kuunganisha mawasiliano ya mtandao wa barabara ambayo yamekatika.
Muhagama alisema kazi kubwa ni kuhakikisha wanarejesha kwa haraka mawasiliano ya barabara yalipo baina ya wilaya ya Kilombero na Ulanga yanapatikana.
Hali hiyo ya kukatika kwa mawasiliano inatokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha na kusababisha kivuko cha mto Kilombero kuzama.
Akitoa taarifa ya awali ya serikali kuhusiana na tukio hilo jana, bungeni mjini Dodoma, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Ajira na Walemavu Jenista Muhagama alisema kwamba sasa tume za kazi za kiutendaji zipo kazini kuweza kuona namna wanavyoshirikisha jeshi la polisi katika kazi hiyo.
Alisema serikali ilipata taarifa ya awali usiku wa kuamkia leo na kwamba kivuko hicho kilikuwa kimebeba abiria 31 magari 3 na bajaj 2 ambapo mpaka sasa kwa taarifa walizonazo ni kwamba abiria 30 wameshaokolewa.
Hata hivyo aliwasihii wananchi kutulia kwak uwa serikali toka ilipopokea taarifa hiyo imekuwa ikishughulikia ili kuona nini kifanyike na kwa wakati gani.
Muhagama alitoa wito kwa watanzania kuchukua tahadhari ya kujinusuru na mvua kwa sababu kwa mujibu wa watabiri wa hali ya hewa wametabiri nchi kuwa na mvua nyingi na upepo na dhoruba kali.
No comments:
Post a Comment