KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Saturday, 5 March 2016

LULUVI: VIGOGO, MATAJIRI MSIJARIBU KUINGILIA MPANGO WA URASIMISHAJI MAKAZI HOLELA



WAZIRI wa Ardhi, Maendeleo na Makazi, William Lukuvi, ameonya baadhi ya vigogo wenye mawazo ya kuingilia mpango wa kurasimisha makazi holela kwa lengo la kuwadhulumu viwanja wakazi wamaeneo husika watambue kuwa watakuwa ni sawa na jipu.
Lukuvi, aliyasema hayo wakati wa uzinduzi wa mpango rasmi wa kitaifa wa kurasimisha makazi holela, unaotarajiwa kuanza Machi 9 mwaka huu na  uzinduzi huo uliyofanyika katika Mtaa wa Kirungure, Kimara wilayani Kinondoni jana jijini Dar es Salaam.
Alisema wananchi wanatakiwa kutambua kuwa urasimishaji utaumiza baadhi ya watu hivyo wanachi hao lazima wawe tayari kujitolea na kushiriki mpango huo.
Uzinduzi huo, pia ulifanyika katika vijiji vya Chasimba, Chatembo na Chachui maeneo ambayo yanadaiwa kuwa wanaishi wavamizi wa Ardhi.
Lukuvi, alisema hayo kwa vile maeneo hayo yanawahusu wakazi masikini ambao walikuwa wakiishi katika makazi hayo holela, kwahiyo yanapimwa ili wakazi hao waweze kutambulika kihalali na kupatiwa huduma za kijamii na wala haiwahusu vigogo wakiwemo matajiri kutoka maeneo mingine.
"Nawaonya wanasiasa na baadhi ya matajiri kuacha kufikiri kwamba huu ndiyo wakati wao wakuja hapa kujipatia nyarubanja kama ulikuwa unaishi Kariakoo au sehemu nyingine endekea kuishi huko huko, lakini hapa marufu,"alionya Lukuvi.
Alisema, yeyote atakayejaribu kukwepesha mpango huo kwa kuwadhulumu wakazi ambao walipaswa kunufaika na urasimishwaji huo, basi ajue serikali haitamvumilia na hatua kali dhidi yake zitachukuliwa.
“Mpango unatarajia kuanza Machi 9 mwaka huu, utasaidia katika kuwafanya wakazi wote waliyokuwa wamejenga bila ya kufuata taratibu za mipango miji kutambulika kutoka makazi holela hadi makazi halali,” alisema Lukuvi.
Lukuvi, alisema mpango huo wa upimaji umekwishaanza katika maeneo hayo na unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi mitatu Kisha Hati za umiliki wa viwanja hivyo vilivyopimwa zitagawiwa kwa wananchi ndani ya mwezi mmoja.
Hata hivyo, Lukuvi alisema katika kulipia Hati hizo kwa mwenye uwezo anaweza kulipia Hati hiyo ndani ya mwezi mmoja na kwale ambao hawana uwezo watalipia hati hiyo kidogo kidogo ndani ya mwaka mmoja.
“Nisisikie kuna mwanasiasa ambaye hakuwa anaishi hapa kesho na kesho kutwa anakujakutaka eneo hapa kwani tunajua wazi kuwa maeneo haya yana wenyewe na mkimuona mtu asiyehusika toeni taarifa,”alisema Lukuvi.
Lukuvi alionya kwa yeyote atakayejiingiza kinyume cha taratibu atambuye kuwa yeye ndiyo anapitisha Hati hizo  hivyo akibaini jina la mtu asiyehusika ataliondoa.
Pia aliwataka wananchi wa kimara kuwa na ushirikiano kwani mpango huo umeanzia kwao huku akiwataka wawe mfano wa kuigwa.
Urasimishaji huo utasaidia kata zao kuwa na barabara inayoeleweka,shule,zahanati,maji pamoja na soko katika maeneo hayo.

Chasimba, Chachui na Chatembo

Aliwataka wakazi wa vitongoji hivyo kuhakikisha kuwa mpango huo wa urasimishaji huo unafanikiwa kwa vile eneo hilo siyo lao bali wanaishi hapo wakiwa wavamizi wa eneo la Twiga Cement.
Alisema mpango wa upangaji,upimaji,ugawaji na umilikishwaji wa eneo utazikatia sensa iliyofanyika mwaka 2012 ambapo kulikuwa na wakazi 4000.
Lukuvi alisema hata watambua wale walioenda kujenga na kununua viwanja maeneo hayo baada ya sensa kupita.
Pia alimtaka mmiliki wa kiwanda cha  Twiga simenti aweke uzio katika maeneo yote ili wanachi wasiendelee kuvamia eneo hilo na kuepuka madhara yatakayo jitokeza kwani wanalipua baruti.
Alisema wakazi wa maeneo hayo watambue kuwa gharama zote zitakazo hitajika katika kupima maeneo hayo watalipa wenyewe kwasababu ni wavamizi.
“Gharama za kumlipa mwenye kiwanda serikali itawasaidia ili tupate hekta 224 zitakazo watosha ninyi wote”alisema Lukuvi.
Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea akizungumza kwa nyakati tofauti akiwa Kirungure na kwa niaba ya mbunge wa Kawe Halima Mdee katika vitongoji hivyo vitatu alishauri wakazi hao kukubali mpango huo  uaze mara moja kwa sababu unalengo la kubadili maisha yao.
“Mkiruhusu mpango huu usimame tu kwa ajili ya mvutano juu ya kamati ambayo mnadai ichaguliwe nyingine kuna hatari mpango huo ukachukua miaka mingi hadi kuanza kwake tena,”alisema Kubenea.
Alisema, utakapokamilika utaweza kuwasogezea huduma zote za kijamii ikiwemo hospitali, masomo na Shule na kwamba watoe ushirikiano kwa Kamati ya vitongoji hivyo, na inayosimamia mpango huo.

No comments:

Post a Comment