KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Monday 2 March 2015

JK ASHINDWA KUJIZUIA ABUBUJIKWA NA MACHOZI



RAIS Jakaya Kikwete leo alishindwa kujizuia na kujikuta akibubujikwa na machozi wakati wa hafla ya kuuga mwili ya Marehemu, Mbunge  Mbinga Magharibi, Kapteni John Komba.
Mbali ya Rais Kikwete baadhi viongozi mbalimbali waandamizi wa vyama vya siasa na Serikali walimwaga machozi kumlilia Kapteni Komba aliyefariki dunia juzi wakati akipatiwa matibabu katika hospitali ya TMJ, jijini Dar es Salaam.
Hali hiyo ilijitokeza leo katika viwanja vya Karimjee ambao ulitawaliwa na majonzi, vilio na huzuni wakati maelfu ya wakazi wa jijini la Dar es Salaam na mikoa jirani walipojitokeza kuuaga mwili wa Kapteni Komba.
Walioibua vilio na hisia za kifo cha Kapteni Komba ni wasanii wa muziki wa dansi wakiongozwa na mwanamuzii mkongwe King Kiki walipoimba wimbo na ‘Nani Yule’
Wimbo huo ulitungwa na Kapteni Komba wakati wa kifo cha Baba wa Taifa mwaka 1999, Mwalimu Nyerere, lakini jana wimbo huo huo ulibadilishwa baadhi ya maneno na kuingiza jina la Marehemu Komba.
Baadhi ya wasanii walioimba wimbo huo, Jose Mara, King Kik na wengine kwa kushirikiana na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye waliimba kwa hisia kali na kusababisha baadhi  ya wananchi waliohudhuria hafla hiyo akiwemo Rais Kikwete, kububujikwa na machozi.
Mbali ya Rais Kikwete, viongozi wengine walioshindwa kujizuia ni pamoja na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Yusuf Makamba ambaye baadaye alisema  chama hicho kimepoteza jino la dhahabu na kubaki na pengo ambalo haliwezi kuzibika tena.
Baadhi ya viongozi waliohudhuria shughuli hiyo ni pamoja na Makamu wa Rais Dk. Mohamed Ghalib Bilal, marais wastaafu Ali Hassan Mwinyi na Benjamini Mkapa, Katibu Mkuu Kiongozi Ombeni Sefue na wake zao pamoja na
Wengine ni mawaziri mbalimbali wa sasa na zamani akiwamo Hussein Mwinyi (Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa), Sophia Simba (Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto), Aggrey  Mwanri (Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu-Tamisemi).
Alikuwepo pia Asha Rose Migiro (Sheria na Katiba), Lazaro Nyalandu (Maliasili na Utalii), Jenister Mhagama (Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi), Januari Makamba (Naibu Waziri Sayansi na Teknolojia), Mwigulu Nchemba (Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi) na wengine.
Baadhi ya wabunge waliokuwapo katika hafla hiyo ni Edward Lowassa (Monduli) Iddi Azzan (Kinondoni), Christopher Ole Sendeke (Simanjiro) Steven Ngonyani (Korogwe  Vijijini), Mussa Zungu (Ilala) na wengine wa viti maaluma.
Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Damian Lubuva, Meya wa Jiji la Dar es Salaam Didas Masaburi, Meya wa Ilala Jerry Silaa na viongozi wengine wa kiserikali.
Pia walikuwamo viongozi wa taasisi binafsi akiwemo Mwenyekiti Mtendaji wa Makapuni ya IPP,  Dk. Reginald Mengi, Mkurugenzi wa Msama Promotion Alex Msama na wengine.
Shughuli ya kutoa heshima za mwisho kwa Marehemu Kapteni Komba,  ilianza majira ya saa tatu asubuhi.
Viongozi mbalimbali wa serikali na vyama vya siasa na wananchi  waliwasili kwa nyakati tofauti na kuchukua nafasi zilizotengwa kwa ajili yao.
Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nasari, ambaye alimwakilisha Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe alifika katika viwanja hivyo majira ya saa 4:33 asubuhi.
Spika wa Bunge, Makinda aliwasili majira ya saa 4:39 asubuhi na kufuatiwa na Makamu wa Rais Dk. Mohammed Gharib Bilali aliyewasili majira ya  saa 4:50 asubuhi.
Ilipotimu majira ya saa 5:15 asubuhi, Rais Kikwete aliwasili katika viwanja hivyo akiambatana na mkewe, Mama Salma Kikwete.
Mwili wa Kapteni Komba, uliwasili baada ya Rais Kikwete kufika uwanjani hapo, ukiandamana na familia ya marehemu pamoja na ndugu wa karibu na majirani.
Watumishi wa idara, taasisi na mashirika ya umma na binafsi, nao walifika kuuaga mwili wa Kapteni Komba na kusababisha shughuli mbalimbali katika ofisi hizo kusimama.
Baada ya mwili kuwasili, kulikuwa sala fupi iliyoendeshwa na Padri wa Kanisa la Kikatoliki, Parokia ya Bikira Maria Mpalizwa ya jijini Dar s Salaam, Florian Tindwa.
Wananchi wamzungumzia
Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Joseph Butiku alisema Kapteni Komba atakumbukwa kwa kuwa msanii na kiongozi mahiri kupitia nyimbo zake.
“Wakati wa uhai wake, hakuteteleka katika shughuli zake za kisanii hata alipokuwa bungeni kwani alikuwa na uwezo wa kusimamia ukweli.
Vituko
Katika hali isiyo ya kawaida wapiga picha kutoka kutoka vyombo mbalimbali vya habari, walijengewa uzio uliyowafanya washindwe kufanya kazi zao kwa uhuru.
Hali hiyo iliwafanya washindwe kupata picha nzuri na baadala yake kupata za upande mmoja.
Rais Kikwete alipoona hali hiyo, aliagiza waandishi hao waachiwe waendelea na kazi yao vila kuwekewa kizuizi.
Kepteni Komba alifariki dunia Februari 28 katika Hospitali ya TMJ  alipokimbizwa  kupata matibabu ya ugonjwa wa kisukari.
Mwili huo ulisafirishwa jana kwenda Songea kwa ndege maalum ya Serikali na mazishi yanatarajiwa kufanyika leo katika kijiji cha Lituli alikozaliwa.

No comments:

Post a Comment