KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Wednesday 25 October 2017

TCU yatangaza tarehe rasmi ya wanafunzi kufika vyuoni


WANAFUNZI ambao tayari wamekidhi vigezo na kupitishwa kujiunga na elimu ya juu wanatakiwa kuripoti chuoni ili kuanza masomo ifikapo Oktoba 30, amesema hayo leo kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), Profesa Eleuther Mwageni .
Prof. Mwageni ameyasema hayo leo wakati anatoa ufafanuzi juu ya tarehe ya kufunguliwa kwa vyuo kutokana na mkanganyiko ambao wameupata baadhi ya wanafunzi kuhusu muda sahihi wa masomo kuanza kwa mwaka wa masomo 2017/18 hususani wale ambao wameomba nafasi kwenye awamu za pili na tatu za Udahili.
“Tarehe ya Kalenda ya masomo haijabadilika iko palepale ambayo ni Oktoba 30 wanafunzi wanatakiwa kuanza masomo ya elimu ya juu kwa mwaka 2017/2018”, amesema Mwageni.
Aidha Prof. Mwageni ameeleza kuwa zaidi ya wanafunzi 450,000 tayari wameshapata vyuo hivyo kinachosubiriwa katika awamu ya tatu ni kupitisha wanafunzi wengine 12,000 ili kufikia malengo ambayo ni wanafunzi 57,000.
Awamu ya tatu ambayo ilianza Oktoba 18 hadi 22 imefikia hatua nzuri ambapo vyuo vinawasilisha TCU majina ya waombaji ambao vimewapitisha ili tume iweze kujiridhisha kisha wanafunzi waliochaguliwa katika awamu hiyo wajiunge na vyuo na waanze masomo kwa wakati.
Mapema mwaka huu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli alishauri TCU iweke utaratibu wa wanafunzi kuomba nafasi chuoni moja kwa moja ili waende vyuo wanavyotaka wao tofauti na awali ambapo zoezi la kupanga vyuo lilikuwa linasimamiwa na tume hiyo.

WAKAZI UTETE WALILIA MIKUTANO

WAKAZI wa Kitongoji cha Nyanda Katundu Kata ya Chemchem iliyoko katika Hamashauri ya Mji Mdogo Utete mkoani Pwani wamelalamikia kitendo cha viongozi kushindwa kuitisha mikutano ya vitongoji, kujadili maendeleo kwa muda wa mwaka mmoja sasa.

Hatua hiyo imekuja baada ya wakazi hao kukabiliwa na kero mbalimbali ikiwemo wakulima kushindwa kujua wapi watakwenda kuuza mazao yao baada ya kukosa masoko.

Akizungumza katika Ofisi za gazeti hili jijini Dar es Salaam juzi, Mwenyekiti wa Kitongoji hicho cha Nyanda Katundu, Omari Ngatima, alisema hafahu sababu has a inayo kwamisha vikao hivyo ambavyo ni mhuhimu kwa maenelo ya wananchi.

"Wananchi wanahitaji mikutano ya wenyeviti wa vitongoji ifanyika kwani wanaamini kuwa hao ndiyo wawakilishi waatakaofikisha kero za kwenye vikao vya ngazi ya juu ili ziweze kupatiwa ufumbuzi,"aliasema Ngatima.

Alisema, wakazi hao hao wanahitaji mikutano ya viongozi hao, kwani wanaamini kufanyika kwake ndiyo kutakuwa suluhu ya kumaliza matatizo yao yanayo wakabili hivi sasa.

"Kukosekana kwa vikao hivyo ambavyo vinatakiwa kufanyika maranne kwa mwaka kunarudisha nyuma maendeleo ya vitongoji vyote vilivyoko katika Kata zote tatu ambazo ni Chemchem, Utete na Ngalambe,"alisema Ngatima.

Ngatima, alisema kutokana na kukosekana na vikao hivyo, vitongoji hivyo vimeshindwa kujiletea maendeleo pia kudhibiti makusanyo ya kodi inayotokana na afanyabiashara wanaofika katika huko kukusanya mazao mbalimbali ikiwemo matikiti maji.

Aliongeza kuwa kukosekana na mikutano hiyo kunasababisha wananchi kushindwa kujua bajeti inayotengwa kwa ajili ya maendeleo ya jamii katika vitongoji hivyo.

Mwenyekiti wa Mji Mdogo wa Utete, Said Nassoro, akitolea ufafanuzi kuhusu madai hayo, alisema sababu kubwa zilozokwamisha vikao hivyo, zianafahamika na kila mmoja.

Alisema sababu kubwa ambazo zimekwamisha mikutano hiyo na usazalishaji mali katika maeneo ya Rufiji, Kibiti na Mkuranga ni kutokana na kukosekana usalama wa kuaminika kwa viongozi wa vijiji, vitongoji na wananchi.

Nassoro, alisema viongozi wa serikali na wale wa vyama vya siasa waliacha kuitisha mikutano hiyo kutokana na mauaji ya baadhi ya viongozi yaliyotekelezwa na watu wasiyojulikana.


"Hao wananchi wanasema tu, unaona wenzako wanakufa halafu unataka na mimi niitishe mkutano kwa kweli kwa hilo hakuna atakayekuwa tayari kwa ujumla viongozi wote katika maeneo hayo hawakuwa salama hali iliyowafanya wakimbie makazi yao,"alisema Nassoro.

Kamwelwe ataka upatikanaji maji ya uhakika



NA ASHA MWAKYONDE, DODOMA

WAZIRI wa Maji na Umwagiliaji, Mhandisi Isaac Kamwelwe, ameziagiza mamlaka za maji kote nchini kuhakikisha ifikapo mwishoni mwa Juni 2018, upatikanaji wa maji safi na salama unafikia asilimia 86.
Akizungumza juzi mjini Dodoma alipokuwa akifungua kikao cha wizara hiyo na watendaji wakuu wa mamlaka za maji safi na usafi wa mazingira Tanzania Bara, Kamwelwe alisema kwamba vi vema viongozi hao wakahakikisha kuwa katika miji mikuu na midogo upatikanaji wa maji safi na salama unafikia wastani usiopungua asilimia 70 ifikapo mwishoni mwa Juni 2018.
“Kama mnavyofahamu ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya 2015-2020 inatuagiza tuhakikishe kuwa ifikapo mwaka 2020 upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi unafikia asilimia 95 kwa miji mikuu ya mikoa, asilimia 90 kwa miji mikuu ya wilaya, miji midogo na maeneo yanayohudumiwa na miradi ya maji ya kitaifa na asilimia 85 maeneo ya vijijini,” alisema Kamwelwe.
Aliongeza kuwa ili kufikia malengo hayo lazima kuwe na tabia ya kujipima kila mwaka ili kujua wanapiga hatua kiasi gani kufikia lengo kuu.
Aidha, alisema kuwa katika kufikia malengo hayo wanatakiwa kuhakikisha kuwa changamoto ya upotevu wa maji wakati yakisafirishwa kumfikia mlaji inapatiwa ufumbuzi.
Naye Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Juma Aweso, aliwataka wakurugenzi wa mamlaka za maji safi na usafi wa mazingira nchini kutoa ushirikiano ikiwa ni pamoja na kufanya kazi kwa bidii ili kuweza kufikia malengo.


Meatu, Busega kukopa Bil. 17/-



NA COSTANTINE MATHIAS, SIMIYU

BARAZA ya Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega na Meatu mkoani hapa wameridhia kukopa Sh. Bil. 17.1 kutoka Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB), kwa ajili ya kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo.
Maazimio hayo yalifikiwa katika kikao cha dharura cha baraza la madiwani vilivyofanyika kwa nyakati tofauti, ambapo Halmashauri ya Wilaya ya Busega imepanga kukopa Sh. Bil. 10.7 kwa ajili ya kutekeleza mradi wa umwagiliaji.
Akiwasilisha taarifa ya Maendeleo ya Mpango wa Kilimo cha Umwagiliaji wilayani Busega, Ofisa Mipango wa Wilaya hiyo, Josephat Joseph, alisema kuwa kazi za upimaji wa mashamba na njia ya kupita bomba la maji, kupima udongo, kusanifu mfereji mkuu kwenye chanzo, sehemu ya kuchukulia maji, nyumba za pampu, mifereji ya kuingiza na kutolea maji, kuandaa michoro na gharama za mradi zimeshakamilika.
Aliongeza kuwa katika utekelezaji wa mradi huo halmashauri ndiyo msimamizi mkuu na itajenga miundombinu na kuingia makubaliano na wakulima wa Mwamanyili kupitia umoja wao watakaounda. 
Kwa upande wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, imepanga kukopa Sh. Bil. 6.4 kwa ajili ya upanuzi wa kiwanda cha Maziwa Meatu (Meatu Milk).
Akizungumzia upanuzi wa kiwanda hicho, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Fabian Manoza, wamekusudia kuongeza idadi ya wafugaji wanaopeleka maziwa kiwandani kutoka 45 wa sasa kufikia 400 wanaofuga ng’ombe wa kisasa.
Aliongeza kuwa mikakati mingine ni kununua mtambo mpya wa kuchakata maziwa lita 15,000 kwa siku, kununua mitamba 1,000 na kuandaa shamba la malisho lenye miundombinu muhimu pamoja na kuongeza soko. 

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka, alisema kuwa wamejipanga kutafuta majawabu ya changamoto za wafugaji kwa kuwasaidia kufuga kisasa, ikiwa ni pamoja na kuwashauri kupima maeneo yao na kuyawekea miundombinu muhimu kama mabwawa, visima, majosho na mashamba ya malisho.

Lugola: Tanesco, NEMC tunzeni bonde la Kihansi

NA MWANDISHI WETU, KILOMBERO

NAIBU Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Kangi Lugola, amelishauri Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kushirikiana na Baraza la Taifa la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kutunza mazingira katika bonde la Kihansi.
Akiwa katika ziara ya siku moja kutembelea eneo hilo hivi karibuni, Lugola alisema ni wakati wa kuondoa dhana kuwa linapotajwa bonde la Mto Kihansi watu wanafikiria vyura adimu wanaopatikana katika bonde hilo tu duniani bali kuna masuala mengi yanayozunguka eneo hilo, ikiwemo vyanzo vya maji yanayotumika kuzalisha umeme.
“Mita moja ya ujazo ya maji inazalisha megawati saba za umeme, maana yake mkiyakosa haya maji hamtaweza kuzalisha umeme kama mnavyojisifia. Hivyo shirikianeni kwa pamoja kuhakikisha eneo hili la kilomita za mraba 580 mazingira yake hayaharibiwi, katika eneo hili kuna nyani, mbega na vipepeo wazuri lazima tuwalinde,” alisema Lugola.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa NEMC, Dk. Vedast Makota, alisema kazi kubwa wanayoifanya ni kutoa elimu kwa wananchi wanaozunguka eneo hilo la Kihansi juu ya umuhimu wa kuhifadhi mazingira kwa sababu kila kilichokuwamo kina faida na kinategemeana katika ukuaji.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa kituo cha kuzalisha umeme cha Kihansi ya Chini (Lower Kihansi), Mhandisi Mathew Bundala aliishukuru NEMC kwa namna walivyokuwa karibu nao kuwaeleza baadhi ya masuala ya utunzaji wa mazingira na umuhimu wake, ameahidi kuyazingatia maagizo ya Naibu Waziri Lugola ili waendelee kunufaika na maji ya bwawa hilo.

Ugatuaji madaraka waongeza kasi ya kazi

NA HAMIDA RAMADHANI, DODOMA

IMEELEZWA kuwa dhana ya ugatuaji madaraka kwa watumishi wa umma imeleta mafanikio na mabadiliko katika utendaji kazi.
Akizungumza jana wakati akifungua mkutano wa tathmini ya maboresho ndani ya utumishi wa umma, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (TAMISEMI), Selemani Jafo, alisema kuwa watumishi wa sekta ya umma wanapaswa kuelewa na kusimamia dhana ya ugatuaji wa madaraka hayo na kwamba tathmini itakayofanyika ilete malengo mazuri katika utendaji kazi kwa kujitoa kuwatumikia wananchi.
“Nategemea tathmini mtakayoifanya italeta malengo mazuri katika utendaji wenu ili kuleta maendeleo kwa nchi yetu hasa kipindi hiki ambacho tunafanya jitihada za kuelekea uchumi wa kati wa viwanda,” alisema.
Mbali na hayo Jafo alisema watumishi wa umma wanapaswa kuzingatia vipaumbele vya utumishi kwa kuhakikisha kwamba wanajituma kwa bidii na kuleta mafanikio kwa wananchi.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza, aliishukuru serikali kwa kufikia hatua hiyo ya ugatuaji na kwamba kwa kuzingatia vipaumbele vya utumishi watahakikisha wanatimiza malengo ya tathmini hiyo.

Mwisho

Friday 1 July 2016

WAKAZI 65, WA BONDE LA MKWAJUNI WAOMBA MSAADA KWA RAIS MAGUFULI

WAKAZI 65 ambao wamebomolewa nyumba zao katika bonde la Mkwajuni wilayani Kinondoni jijini Dar es Salaam, wameiomba serikali ya Rais John Magufuli, iwapatie msaada wa kibinadamu.
Wakazi hao wanahitaji msaada ikiwa ni pamoja na mahitaji ya kijamii kwa vile tangu nyumba zao zilipobomolewa kimakosa ni zaidi ya miezi sita huku wakiishi katika vibanda bila ya msaada wowote kutoka serikalini.
Wakizungumza na wandishi jijini jijini, kwa nyakati tofauti, wakazi hao walisema wamekuwa wakiendelea kuishi katika mazingira hayo magumu, kwa sababu ya kuasubiri uamuzi wa serikali ambayo iliahidi kwa wale waliyokuwa wamejenga kutokana na vibali walivyopewa na maofisa wa serikali wangefidiwa.
Miongoni mwa wakazi hao ni Sabrina Hilal (63), alisema wamefikia hatua hiyo kwa vile wakati nyumba zao zinabomolewa wakazi hao walikuwa na hati halali hivyo kuahidiwa kuwa wangelipwa fidia kwa ajili ya kwenda kuanza maisha mapya sehemu nyingine.
“Tunamuomba Rais Magufuli, atusaidie kwani tunadhani yeye ndiyo mtu wa mwisho ambaye anaweza kutuokoa katika maisha haya magumu kwenye hivi vibanda tunamoishi, atusaidie tuondoke hapa,” alisema Sabrina.
Alisema, tangu opeaheni ya bomoabomoa ya nyumba zilizojengwa katika maeneo ya mabondeni na hatarishi ni zaidi ya miezi sita sasa lakini walipopewa hadi kwamba wangefidiwa hakuna kitingozi yoyote wa serikali aliyewatembelea kuja kujua hatima ya maisha ya wakazi hao.
“Sisi tumebomolewa nyumba zetu lakini tuna hati ambazo tulipewa na Manspaa Kinondoni huku tukilipa hata kodi zaajengo, leo tunashangazwa na ukimnya wa Manispaa yetu”alisema.
Alisema kuwa haki ya kuishi katika vibanda hivyo kumekuwa na madhara makubwa sana ikiwemo watoto kubanwa na kifua kutokana na hali ya hewa ya kipupwe.
Mwanaidi Idd, alisema kwa vile Rais Magufuli ameaikika mara kwa mara nia ya serikali yake ni kusaidia wananchi hivyo anaamini kuwa atalishugulikia suala hilo ili haki ipatikane.
Alisema wanamuomba Rais Magufuli, afanye ziara ya kushtukiza ili kwenda kujionea maisha wanayoishi wananchi wake waliyompigia kura katika uchaguzi mkuu uliyofanyika mwaka jana.

Aidha, Mwanaidi, alishauri serikali kuwachukulia hatua za kishwria kwa maofisa wote wa manispaa ya Kinondoni, ambao walihusika katika utoaji wa vibali vya ujenzi katika maeneo hayo huku wakijua ni hatarishi.