KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Thursday 2 April 2015

JWT YAITUHUMU MAMLAKA YA MAPATO TANZANIA

      MWENYEKITI WA JWT, Minja akizungumza na wandishi wa habari hako pichani
JUMUIYA ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT), imeituhumu Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa kuendesha vitendo vya ufisadi bandarini kwa kushirikiana na wakala wanaohusika na forodha.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo, Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Johnson Minja, alisema kuwa sheria ya ulipaji kodi haiwapi  nafasi wafanyabiashara kujua kiwango halisi cha ulipiaji mzigo bandarini.

Alisema wafanyabiashara wanapoaingiza kontena moja hulipia shilingi milioni 40 huku risiti ikionyesha kuwa kontena hilo limelipiwa shilingi milioni 10.

Minja alisema kuwa serikali inapoteza mapato kupitia mikono ya watu wachache walioaminiwa na serikali kuifanya kazi hiyo.
“Sheria haikupi nafasi ya kujua ni  kiwango gani unatakiwa kulipia, hapo unalazimika kumfuata wakala wa forodha ambaye anakupangia bei ya kulipia,” alisema.

Minja alisema  wafanyabiashara walianza kupinga kitendo hicho cha ulipaji kodi usioeleweka kwa muda mrefu lakini serikali haikuwasikiliza.

“Tunataka serikali iweke mfumo ulio wazi wa ulipaji kodi kwa wafanyabiashara kama ilivyo kwa ulipaji kodi wa magari ili iweze kunufaika, tofauti na ilivyo sasa ambapo kwa sasa wanaonufaika ni watu wachache, tuna nia ya dhati ya kulipa kodi  kwa serikali yetu,” alisema Minja.

Aliongeza kuwa migorogo ya wafanyabiashara na serikali inatokana na kutosikilizwa kilio chao cha muda mrefu, hivyo wanataka kulipa kodi halisi kwa serikali ili iweze kupata pato.
Minja alisema  serikali itilie  mkazo jambo hilo ili kuondokana na mambo yanayosababisha migogoro ya mara kwa mara baina yao na  wafanyabiashara.

Alisema kuwa ataendelea kutoa elimu kwa wafanyabiashara na kuishauri serikali juu ya mfumo wa ulipaji kodi utakaozidi kuinufaisha Tanzania, ambayo inaingiza fedha nyingi kuliko nchi za jirani zinavyoingiza kupitia kodi.

“Lazima tufike mahali tuangalie kwa dhati suala hili ili kuweza kuepuka migogoro isiyo na tija kwa taifa letu,” alisema.
Minja aligusia kufutwa kwa dhamana yake ya awali kuwa kulitokana na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George  Masaju, hakupitia faili lake vizuri kabla ya kufuta dhamana hiyo.
Alisema amemsamehe Masaju na hana kinyongo pia hatadai fidia kwa mambo yaliyotokea.

Alisema sababu ya kufutiwa dhamana yake ya awali ni kutokana na wafanyabiashara wengi kufika mjini Dodoma kusikiliza kesi yake.
Minja alipewa dhamana juzi ya masharti ya kuwa na mdhamini mmoja ambaye ni mfanyakazi wa serikali anayeishi Dodoma, aliyesaini bondi ya shilingi milioni nne.

Minja alifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Dodoma Januari 28, mwaka huu kwa kosa la uchochezi na kuwashawishi wafanyabiashara wasilipe kodi kwa kutumia mashine za kielektroniki (EFDs).
Kesi hiyo itaanza kusikilizwa kwa maelezo ya awali Aprili 9, mwaka huu kutokana na ushahidi wa kesi hiyo kukamilika.

Akijibu malalamiko hayo, Ofisa Mkuu wa Huduma na Elimu wa TRA, Julius Mjenga, alisema kuwa wafanyabiashara wana vyama vyao hivyo kama kuna jambo linawatatiza wanaweza kuonana na Kamishna wa Forodha ili watafute ufumbuzi.

Alisema kuwa wanafanya kazi na wakala waliosajiliwa kisheria na kwamba sheria zao zipo wazi.

Aliongeza kuwa sheria ya bidha haiwezi kuwa sawa na ili ya magari, kwa kuwa wafanyabiashara wanatakiwa kuonyesha nyaraka za mizigo waliyoingiza.

Aliwataka wafanyabiashara kushirikiana na TRA kufuatilia na kamishna atachukua hatua sitahiki.


 Juzi wakati akitoa hotuba ya kuahirisha Bunge, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alitoa wito kwa wabunge na viongozi wengine nchini kushirikiana na serikali kuwaelimisha wananchi na wafanyabiashara kuhusu manufaa ya matumizi ya mashine za kielektroniki za EFDs.

Pinda alisema elimu hiyo itasaidia kujenga tabia ya kufanya biashara kwa kutunza kumbukumbu za mauzo ili Tanzania iweze kufikia maendeleo endelevu kwa  wananchi kulipa kodi stahiki.

No comments:

Post a Comment