SERIKALI imesema kuwa maandalizi
ya Sherehe za Miaka 51 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar
yamekamilika na kwamba sherehe hizo zitafanyika katika uwanja wa Uhuru
Aprili 26 mwaka huu.
Akitoa ufafanuzi kuhusu kukamilika
kwa maandalizi ya sherehe hizo kwa niaba Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam
leo, Mkuu wa Wilaya ya Temeke Bi. Sophia Mjema amesema maadhimisho ya
mwaka huu yatapambwa na Kauli Mbiu isemayo Miaka 51 ya Muungano,
Tudumishe Amani Na Umoja ,Ipigie Kura ya Ndiyo Katiba inayopendekezwa na
Kushiriki Uchaguzi Mkuu.
Amesema Tanzania katika kipindi
cha miaka 51 ya Muungano imepata mafanikio makubwa katika Nyanja
mbalimbali za maendeleo ya jamii, uchumi, Siasa,Ulinzi, Usalama na
Uhusiano wa Kimataifa.
Bi. Mjema amefafanua kuwa
maadhimisho hayo yataongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Dkt. Jakaya Kikwete ambaye atakuwa mgeni rasmi na kupambwa na michezo ya
Halaiki, ngoma za asili, vikundi vya burudani na Gwaride la heshima
litakalohusisha vyombo vya ulinzi na usalama.
Pia yatapambwa na Wimbo maalum
utakaoimbwa na vijana wa halaiki na ndege vita za Jeshi la Wananchi wa
Tanzania (JWTZ) zitakazopita mbele ya mgeni rasmi Kama sehemu ya
shamrashamra ya sherehe hizo.
Ametoa wito kwa wananchi
wajitokeze kwa wingi kuhudhuria maadhimisho hayo na kufafanua kuwa
milango ya uwanja wa Uhuru itakuwa wazi kuanzia saa 12:30 asubuhi ili
kuwawezesha wananchi kuingia kushuhudia sherehe hizo.
Aidha, ameutaka uongozi wa SUMATRA
na wamiliki wa vyombo vya usafiri (Daladala) kuelekeza magari yao ya
abiria kwenda uwanja wa Uhuru ili kurahisisha huduma ya usafiri kwa
wananchi.
No comments:
Post a Comment