KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Sunday 3 May 2015

MADEREVA WANAGOMA KESHO



UMOJA wa Vyama vya Madereva Tanzania, umetangaza kufanya mgomo usio na ukomo wa nchi nzima kuanzia leo, kw amadai kwamba serikali imepuuza ombi lao la kukutana walilotoa siku nne zilizopita ili kujadili madai yao ya msingi.
Akitoa tamko la mgomo huo jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa Umoja wa madereva hao, Rashid Salehe, alisema kuwa kauli za dharau kutoka kwa baadhi ya viongozi ndizo zilizowasukuma kugoma.
Alisema, hivi karibuni Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta alikaririwa na baadhi ya vyombo vya habari akisema kuwa madereva wapo wengi hivyo wasifanye migomo ya mara kwa mara isiyo na madai ya msingi.
Saleh, alisema Waziri huyo alitoa kauli ya dharau isiyowaridhisha na kuwakatisha tamaa katika taaluma yao kwa kusema madereva wapo wengi na kwamba hupatikana kwa urahisi kuliko wasichana wa kazi za ndani.
"Tumechaka na kauli za kisiasa za viongozi wetu. Sasa tumaeamua hatutayatoa magari hadi serikali itakapoamua kukaa meza moja na kusikiliza madai yetu," alisema.
Alisema kauli za kisiasa ambazo hazitekelezeki, zimewachosha kwani wamekuwa wakiahidiwa kwa muda mrefu bila ya madai yao kupatiwa ufumbuzi na badala yake wamekuwa wakipigwa dana dana.
Aliongeza kuwa leo watakuwepo katika kituo cha mabasi yaendayo mikoani na nje ya nchi ili kuendelea na mijadala yao ya kutathimini maamuzi yao baada ya kuona wamepuuzwa na serikali.
Naye mwenyekiti wa umoja huo Clement Masanja, alisema kuwa kinachofuata baada ya mgomo huo ni kurudisha leseni sehemu husika ili wakalime.
"Hatuwezi kufanya kazi bila kuwa na mikataba inayotambulika kisheria, tunarudisha leseni zetu ili wanaotaka kufanyakazi bila mikata waende wakachukue nafasi hizo," alisema.
Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Madereva wa malori Tanzania, Shaban Mdemu aliwatahadharisha baadhi ya dereva wenye leseni kwamba kwamba kwa siku ya leo  wasijaribu kutoa magari hadi mgogoro huo utakapopatiwa ufumbuzi.
"Tumenyanyasika vya kutosha tunawaomba Kamanda wa kikosi cha usalama Barabarani na Kamanda wa Kanda Maalumu Kamanda Suleiman Kova kutupatia ulinzi kwa usalama wetu lakini sio kutubuguzi," alisema Mdemu.
Mgomo huo unafanyika baada ya siku nne zilizotolewa na uongozi wa umoja huo ulikutana Aprili 29 mwaka huu kutoa mrejesho baada ya kukutana na Naibu Waziri wa Kazi na Ajira, Dk. Makongoro Mahanga, Aprili 18, mwaka huu, kwa madereva wenzao na kuyajadili majibu waliyoyapata kwa Naibu Waziri huyo.
Mrejesho huo ni kwamba katika kikao walichokutana na Naibu Waziri Dk. Mahanga kulikuwa hakuna jipya zaidi ubabaishaji.

Mgomo wa awali
Aprili 9 mwaka huu madereva hao waligoma wakiitaka serikali kuweka mfumo mzuri wa ajira na kupinga kujerejea katika mafunzo kila baada ya mika mitatu.
 Mafunzo hayo yalitokana na Serikali kuifanyia marekebisho Sheria ya Usalama Barabarani kwa kuingiza kipengele kinachowataka madereva kwenda Chuo cha Usafirishaji (NIT), kwa mafunzo ya muda mfupi mara kila wakati leseni zao zinapoisha ili kupata sifa ya kupata leseni nyingine.
 Utaratibu huo uliotangazwa Machi 30 mwaka huu, ulipingwa vikali huku madereva wakidai kuwa hawakushirikishwa katika kuuandaa.
 Madai hayo ni pamoja na kuondolewa kwa ulazima wa kusoma kila baada ya miaka mitatu na kujilipia gharama za mafunzo ambazo walidai ni Sh560,000 kwa magari ya kawaida na sh. 200,000 kwa magari ya abiria.
 Madereva hao pia wanadai kuwa hawawezi kuhudhuria mafunzo hayo wakati hawana mikataba ya ajira inayoweza kuwahakikishia kazi zao zinalindwa hadi wanapomaliza mafunzo.
 Madai mengine ni kuondolewa kwa faini ya sh.300,000 kwa kila kosa la barabarani, Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchikavu (Sumatra) kuhakiki uhalisi wa dereva anayeandikishwa na mmiliki wa chombo husika.





No comments:

Post a Comment