KILIO kikubwa cha wafanyabiashara wanaoendesha biashara zao katika Uwanja wa maonyesho wa Sabasaba mkoani Morogoro ni kunyang’anywa vibanda vyao na Chama cha Mapinduzi (CCM), wilayani humo.
Wakizungumza na mwandishi wa makala hii mkoani humo,wafanyabiashara hao wanasema waliingia makubaliano na chama hicho, kujenga ukuta wa uwanja huo ikiwa fidia ni kujenga mabanda yao ya kuendeshea biashara zao.
Mmoja wa wafanyabiashara hao, Robert Mluge anasema mwaka 1989 walijenga vibanda hivyo kwa shinikizo la Manispaa ya Morogoro kwamba endapo watajenga uzio wa uwanja huo vibanda watakavyojenga watamiliki wao wenyewe kwa kufidia gharama walizojengea ukuta huku manispaa ikimiliki sehemu ya uwanja.
“Manispaa ilitutafuta wenyewe kwa kutushawishi kupitia Ofisa utamaduni wa Manispaa ya Morogoro aliyejulikana kwa jina moja la Ntemo”anasema Mluge.
Anasema mwaka 2007 Chama cha Mapinduzi (CCM),Wilaya ya Morogoro walithitaji wajenzi hao kulipa kodi ya pango ya shilingi 150,000 kwa kila kibanda kwa madai kuwa wao ndio wamiliki halali wa uwanja huo.
Mluge anasema walikataa hatua hiyo ya kutakiwa kulipa kodi ya pango kutokana na wao walijenga kwa nguvu zao na kwa makubaliano.
Anasema baada ya CCM kuona wajenzi hao wamekataa kulipa kodi, iliwashitaki wajenzi hao mara kadhaa katika mahakama na mabaraza ya ardhi ambapo hukumu zilionyesha kuwa wajenzi wanahaki hivyo kukitaka chama cha CCM kuwarudishia vibanda na kuwalipa mali zao walizoziuza.
Mluge anasema alitaja mali zao zilizouzwa kuwa ni pamoja na mashine na majokofu ambazo ziliuzwa kwa bei ya mnada na dalali aliyejitambulisha kutumwa na CCM, aitwaye G. Mwambogela kutoka Majembe Auction Mart.
Kwa mujibu wa hukumu iliyotolewa na msajiri wa mahakama kuu kitengo cha ardhi L, M Mlacha, imeeleza kuwa maombi yaliyotumwa na CCM kwa ajili ya utekelezaji wa kuwafukuza na kufunga milango madai hayo hayana msingi wa kisheria, ni potofu na iwalipe gharama.
Mluge anasema baada ya hukumu hiyo Wajenzi walimuandikia Katibu Mkuu wa CCM kumtaka amuamuru Katibu wa wilaya wa chama hicho kurudusha maeneo yao lakini mpaka sasa hawajajibiwa.
Barua hiyo ilikuwa imeandikwa
Kamati ya wenye
Vibanda Sasaba
Morogoro
Katibu Mkuu wa CCM
Makao Makuu ya CCM
S.L.P 50
DODOMA.
Mheshimiwa,
YAH :KUMUAMURU KATIBU WA CCM WILAYA YA MOROGORO MJINI ALI ISSA ALI KURUDISHA VIBANDA VYA BIASHARA VYA UZIO WA u UWANJA WA SABASABA KWA WENYEWE.
Rejea kichwa cha habari hapo juu:
Tunakuarifu kuwa kesi namba 199/2010 baina ya wenye vibanda tajwa hapo juu dhidi ya wadhamini wa CCM yenye kichwa cha habari,John Michael and Other (Plaintiffs)versus Board of Trustees of CCM(Respondent)imehitimishwa ,kwa CCM,pamoja na kakaza hukumu mara kadhaa mahakamani kukosa uhalali wa kisheria nakuvihodhi.
Pamoja na kukwama huko kwa CCM,tokea tarehe 26 Machi 2013 hadi sasa katibu wa CCM Ally Issa Ally ameipuuza Mahakama hususan amri anayomkataza CCM kuwatoa wenye vibanda (eviction)na kufungua milango(unlocking doors) ya vibanda kwa kujikita kwenye ufisadi kutumia mgongo wa CCM na cheo chake kujineemesha zaidi yeye binafsi na wapambe wake wachache wa uwanjani hapo, huku akikwepa kujibu tuhuma dhidi yake kwa wanahabari ili kunyima umma kupata ukweli bila uhalali wa kisheria.
Amejimilikisha vibanda hivyo kwa kulazimisha wenye vibanda kulipa kodi CCM,kuwaridhi kwa hila wapangaji wa wenye vibanda na kuwaongoa kuwa wa CCM na kwa wale wenye vibanda waligoma kulipa kodi hiyo haramu basi vibanda vyao vilifungwa kisha kuvunjwa na mali kuporwa kwa kutumia dalali feki.
“Kiukweli ni muda mrefu tunateseka sisi na familia etu kiuchumi na kisaikolojia juu ya amali zetu hivyo basi katika kuenzi utawala bora hasa kwa viongozi ,muamuru mara moja katibu huyu aliyechini yako kutii sheria bila shuruti na kwa kuzingatia mashart yaliyoainishwa kwenye ilani ya wakili Nyoronyo tunamini amani itatamalaki vibandani sabasaba kwenye kipindi hiki cha mpito,huku tukiendelea na michakato ya kupata suluhu ya kudumu.
Kwa upande wake Katibu mkuu wa CCM Wilayani humo,Ally Issa Ally akijibu malalamiko hayo anasema wajenzi hao wamejenga vibanda katika eneo la serikali na makubaliano yalikuwa wajenge uzio na baada ya hapo watafidia kwa kujenga mabanda yao ya biashara ambayo walitakiwa kuyamiliki kwa muda wa miaka kumi.
Anasema baada ya kumiliki kwa miaka hiyo walitakiwa wayarudishe kwa CCM ili wayakodi tena kimikataba kwa wale watakao kubali, na kwa wale wasiokubali wayaache yakiwa mikononi mwa CCM ili ipangishe wapangaji wapya.
Anasema baadhi yao walikubali na wengine walikataa na baada ya kukataa masharti hayo wajenzi hao waliamua kukodisha wapangaji wengine na baadhi yao wakafunga mabanda hayo kwenye mageti yao kwa kuchomea na moto ili wapangaji wasifungue na kuendesha biashara zao.
Ally Issa Ally anasema wajue wanafanya kosa kwa wapangaji wa Chama cha CCM ambao ni halali waliopangishwa kisheria mwaka 2013 wasihangaike kutafuta haki ambayo sio yao .
“Tulikubaliana kuwapa mikataba na wakishindwa wanarejesha mabanda hayo kwetu kwa hiyo wameshindwa ndio maana tumeyachukua kwani eneo walilojenga mkataba wao umeisha”anasema Ally Issa Ally.
zawadichogogwe@yahoo.com
No comments:
Post a Comment