KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Thursday 16 July 2015

POLISI WALIOUAWA WAAGWA

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, akitoa heshima za mwisho mbele ya majeneza ya askari wawili mioongoni mwa wanne waliouawa na majambazi Julai 12 mwaka huu katika Kituo cha Polisi Stakishari, Ukonga jijini Dar es Salaam. (Picha na Francis Dande).
SIKU chache baada ya Kituo cha Polisi cha Stakishari jijini Dar es Salaam kuvamiwa na watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi, Jeshi la Polisi nchini limeunda kikosi maalumu chenye askari waliopata mafunzo ya ziada kupambana na matukio ya aina hiyo.
Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) Ernest Mangu, wakati wa kuaga miili ya askari waliouawa kwenye tukio hilo kwenye Kituo cha Polisi cha Kilwa Road jijini Dar es Salaam jana, Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema kikosi hicho kimeundwa maalumu kutokana na aina ya matukio ambayo yanaonekana ni zaidi ya ujambazi.
"Tukio lile ni zaidi ya ujambazi na ni tukio kubwa kufanyika hapa jijini Dar es Salaam, majambazi kwa kawaida huwa wanavamia sehemu ambayo kuna fedha au mali na huwa hawazidi watano, lakini kwenye tukio lile walikuwa majambazi 16," alisema.
Askari walioagwa jana ni D6752, Adam Nyamhangwa (50) ambaye atasafirishwa leo kwenda kuzikwa kijijini kwao Korotange Tarime na E 1279 Coplo Peter Sabuni (51), ambaye mwili wake utasafirishwa kwenda mkoani Mwanza.
Kamanda Kova alisema jeshi hilo limejipanga kupambana kwa mbinu zote kuhakikisha wahalifu waliohusika na tukio hilo wanakamatwa  na kwamba kikosi kilichoundwa na IGP kimekabidhiwa magari ya kufanya kazi usiku na mchana.
Hata hivyo, ibada hiyo ya kuaga marehemu hao haikuhudhuriwa na viongozi wa ngazi ya juu wa jeshi hilo na Wizara ya Mambo ya Ndani kutokana na kile kilichoelezwa na Kamanda Kova  kuwapo kwenye vikao kulifanyia kazi tukio hilo.
"Sisi si wanasiasa bana! Nataka niwahakikishie kuwa tumefikia hatua nzuri ya upelelezi kwenye tukio hili na si muda mrefu tutawaeleza hatua tuliyofikia lakini kwa sasa niishie hapo maana nikiendelea nitaharibu uchunguzi unaoendelea," alisema.
Kova aliwataka askari kufanya kazi yao bila woga, kwani wanatakiwa kuwajibu wahalifu hao kwa vitendo na wakae tayari kwa kujibu mapigo.
Awali , Kamanda wa Mkoa wa Ilala, SACP Lucas Mkondya, alisema anataka tukio hilo liwe la mwisho kwenye mkoa wake na amewataka wahalifu kutolilaumu Jeshi la Polisi kwa hatua watakazozichukua.
Kituo cha Polisi Stakishari kilicho Ukonga jijini Dar es Salaam kilivamiwa na majambazi Julai 12 mwaka huu na kuwaua askari wanne na raia watatu.

CHANZO TANZANIA DAIMA


No comments:

Post a Comment