KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Wednesday 27 April 2016

MAGUFULI AWASAMEHE WAFUNGWA 3,551



RAIS John Magufuli amewasamehe wafungwa 3,551, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 52 ya Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar, ambao umeasisiwa Aprili 26 mwaka 1964.
Lengo la serikali katika msamaha huo ni kuona wafungwa walioachiliwa huru wanarejea tena katika jamii, kushirikiana na wenzao katika ujenzi wa Taifa na kwamba watajiepusha kutenda makosa ili wasirejee tena gerezani.
Katika taarifa yake hiyo kwa vyombo vya habari na kusainiwa na Meja Jenerali Projesta Rwegasira, alisema msamaha huo wa Rais hautawahusu wafungwa waliohukumiwa kunyongwa, kifungo cha maisha, makosa ya dawa za kulevya, rushwa na wale waliyojihusisha na mashambulizi, ukatili dhidi ya watu wenye ualbino na waliyowapa mimba wanafunzi.
Alisema Rais Magufuli ametumia madaraka yake aliyopewa chini ya Ibara ya 45 (1) (d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Rwegesira, alisema wafungwa hao wapatao 3551 watafaidika na msamaha huo, baada ya kupunguziwa moja ya sita ya vifungo vyao ambapo 580 wataachiliwa huru na wengine 2,971 watanufaika na kubaki gerezani wakitumikia sehemu ya kifungo chao kilichobaki. 

Aliwataja wafungwa waliyonufaika na msamaha huo kuwa ni pamoja na wagonjwa wa Ukimwi, Kifua Kikuu (TB) na saratani.
“Wafungwa hawa ni wale ambao wamethibitishwa na Jopo la waganga chini ya uenyekiti wa Mganga Mkuu wa Mkoa na wa Wilaya,”alisema.
Wengine ni wazee wenye umri wa miaka 70 au zaidi, wanawake waliyoingia gerezani huku wakiwa wajawazito pamoja na wale waliyoingia na watoto wanaonyonya na wasiyonyonya.
Pia, aliwataja wengine kuwa ni kundi la watu wenye ulemavu wa mwili na akili.
Aidha, alisema msamaha huo wa rais hautawahusu wafungwa wanaotumikia kifungo kwa makosa ya unyang’anyi na unyang’anyi wa kutumia silaha.
Kundi lingine ni wanaotumikia kifungo kwa makosa ya shambulio la aibu kama vile kunajisi, kubaka, na kulawiti, au akujaribu kutenda makosa hayo.
Rwegasira alisema wafungwa wanaotumikia kifungo chini ya Sheria ya Bodi ya Parole (Act. No. 25/1994) na Sheria ya Huduma kwa Jamii (Act.No.6/2002) na wale waliopatikana na hatia na kuhukumiwa kifungo kwa makosa ya kutumia vibaya madaraka yao nao hawahusiki na msamaha huo.

No comments:

Post a Comment