KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Sunday 19 April 2015

NAPE: NEC WEKENI MAZINGIRA MAZURI KWA VIJANA



KATIBU wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye, ameitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuwawekea vijana mazingira bora ya uandikishwaji katika daftari la kudumu la mpigakura, ili washiriki uchaguzi mkuu ujao.

Akizungumza katika Uwanja wa Stakishari wakati wa tamasha la vijana lililoandaliwa na Mfuko wa Elimu wa Bonnah,  Dar es Dar Salaam jana, Nape alisema tume hiyo ichukue hatua ya kuwaangalia vijana na kuwawekea mazingira bora ili wasipoteze haki yao ya msingi.

“NEC iandae dawati maalumu la vijana kwa lengo la kuwarahisishia kujiandikisha katika daftari hilo na pia waepuke kuwauliza maswali magumu ambayo yatawakatisha tamaa na kushindwa kujiandikisha,”alisema.

Nape aliongeza kuwa ni vyema wajumbe wa NEC wakaangalia ratiba ya vijana kwa ajili ya kujiandikisha na kwamba itawafanya wajitokeze kwa wengi kujiandikisha katika daftari hilo.

Alisema wanasiasa wamekuwa wakiwatumia vijana kwa masilahi yao binafsi bila kuangalia kwa kina  kuwa ndiyo tegemezi kwa taifa.
Nape aliwataka vijana kutojiingiza katika makundi  ya ushabiki na badala yake washirikiane na kushawishiana kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapigakura.

Kwa upande wake, Diwani wa Kipawa, Bonnah Kaluwa alisema vijana ndiyo nguvukazi inayotegemewa na taifa katika kufanya uamuzi wenye tija ukiwamo wa kujiandikisha katika daftari la kudumu la mpigakura.

Alisema kujiandikisha katika daftari la kudumu la mpigakura ni haki ya kila mtu ili asipoteze nafasi ya kuwachagua viongozi wanaofaa kumwongoza katika uchaguzi mkuu ujao.

Kaluwa, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Mfuko wa Elimu wa Bonnah alisema lengo la tamasha hilo ni kuwakusanya vijana pamoja  na kuelezana juu ya umuhimu wa kujiandikisha katika daftari la kudumu la mpigakura.

“Mfuko wa Elimu wa Bonnaha umeona kuna haja ya kuwaleta vijana sehemu hii ili kukumbusha umuhimu wa kujiandikisha katika daftari la kudumu la mpigakura na hatimaye kuweza kupata nafasi ya kushiriki katika uchaguzi mkuu ujao,”alisema Kaluwa.

No comments:

Post a Comment